Saturday, November 3, 2018

DKT.TULIA ATOA RAI KWA MIKOA NA WILAYA NCHINI KUIGA MKOA WA PWANI KWA KASI YA UWEKEZAJI

NA MWAMVUA MWINYI,PWANI

NAIBU Spika wa Bunge ,Dkt .Tulia Ackson amewataka wakuu wa mikoa na wilaya nchini kuiga mfano wa mkoa wa Pwani ,kuvutia wawekezaji pamoja na kutenga maeneo ya uwekezaji ili kwenda na kasi ya ujenzi wa viwanda .

Akitembelea maonyesho ya bidhaa za viwandani ,Pichandege Kibaha Mkoani Pwani ,Dkt.Tulia alisema mkoa wa huo una viwanda vikubwa 109 ambavyo ni vingi kwenye mkoa mmoja .Alieleza ,mikoa mingine ardhi zimefinywa bado hawajaona fursa hii, hivyo watenge maeneo na kuweka mipango mkakati ili kuwarahisishia wawekezaji kupata maeneo .

"Nimepita kwenye mabanda mengi ya wenye viwanda kwenye maonyesho haya ,wameonyesha nia ya kukuza viwanda vyao kwa maana ya kwamba kwenda kwenye kanda mbalimbali ,wanataka kuendeleza zoezi hili sehemu nyingine ""Tunaweza kujiiuliza kwanini viwanda vinaenda Pwani lakini kumbe wamesharahisisha kwa kutenga maeneo mengi na kujiwekea mipango na kuboresha miundombinu " alifafanua Dkt.Tulia .

Aidha ,alisema wataishauri serikali namna ya kufanya navyo kazi viwanda vya nguzo za umeme za zege kwani matumizi ya kusogeza huduma ya umeme bado ni makubwa hivyo zikitumika itasaidia tofauti na nguzo za miti ambazo zinagusa suala la athari za kimazingira .

Akiwa katika banda la kampuni inayojishughulisha na uingizaji wa dawa za kutibu maji nchini (Junaco),Dkt.Tulia aliambiwa na ofisa uendeshaji wa kampuni hiyo ,Edwin Magere kuwa,wameanza mchakato wa kujenga kiwanda kingine cha kutengeneza mita za maji wilayani Bagamoyo .

Alieleza ,kikikamilika kitasaidia kuwarahisishia wananchi kulipa bill zao kulingana na matumizi .Magere alisema ,Junaco imeingia ubia na kampuni ya Baylan kutoka nchini Uturuki pamoja na kiwanda cha Serbia Dinamic kutoka Malaysia kwa ajili ya kutengeneza mita za maji na mchakato unakwenda vyema .

Alibainisha ,Junaco inatarajia kuzalisha ajira 1,200 baada ya kukamilisha ujenzi wa viwanda vyake eneo la Msufini huko Mlandizi ,Kibaha na Mapinga wilayani Bagamoyo .Nae mkuu wa mkoa wa Pwani ,mhandisi Evarist Ndikilo alisema maonyesho hayo ni mwanzo ,na wamejipanga yatakuwa ni endelevu .
Ndikilo alisema ,mara ya mwisho kufanyika maonyesho ya aina hiyo ilikuwa 1984 ,miaka 34 iliyopita) hivyo imekuwa kama kitu kigeni kwa wananchi .
 NAIBU Spika wa Bunge ,Dkt .Tulia Ackson ,alipotembelea maonyesho ya bidhaa za viwandani ,Pichandege Kibaha Mkoani Pwani (picha na Mwamvua Mwinyi)
 Banda la kampuni inayojishughulisha na uingizaji wa dawa za kutibu maji nchini (Junaco), (wa katikati)ni ofisa uendeshaji wa kampuni hiyo ,Edwin Magere.(picha na Mwamvua Mwinyi)

No comments: