Sunday, November 4, 2018

BITEKO KUTATUA MGOGORO BAINA YA KIJIJI CHA NGULA NA MMILIKI WA ENEO LA UCHIMBAJI WA MADINI YA DHAHABU WA NYATI RESOURCE

Na Rhoda James - Geita

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko ameuagiza mgodi wa Nyati Resources ltd uliopo katika kijiji cha Ngula kata ya Bujula mkoani Geita kutolipa gawio Serikali ya kijiji cha Ngula kuanzia tarehe 2 Novemba, 2018 ili kutoa nafasi ya uchunguzi kujua ni nani mmiliki halisi wa eneo hilo la mgodi.

Ametoa agizo hilo wakati wa ziara ya kikazi ya siku mbili kuanzia tarehe 2 hadi 3 Novemba, 2018 iliyolenga kukagua machimbo ya madini katika Mkoa wa Geita.

Pamoja na ukaguzi huo, Biteko ameeleza kuwa, ametembelea machimbo hayo ili kutatua mgogoro wa ardhi uliopo baina ya Kijiji cha Ngula na mkazi wa kijiji hicho Mindi Masasi. Akizungumza katika kikao hicho, Biteko ameutaka Mgodi huo wa Nyati Resources ltd kutolipa gawio kwa kijiji hicho kwa kuwa kuna malalamiko kutoka kwa mkazi wa kijiji hicho ambaye ni Mindi Masasi.

Biteko ameeleza kuwa mgodi huo umeanza uzalishaji tangu Desemba, 2017 na umekuwa ukimlipa Mindi Masasi gawio kwa zaidi ya mwaka kwa kuwa wakati wanaanza uzalishaji wa dhahabu wamemkuta katika ardhi hiyo ambayo amekuwa akiishi tangu mwaka 1954 lakini sasa kijiji kinadai kuwa ardhi hiyo ni mali yao na wao ndio wenye haki ya kulipwa gawio hiyo.

Pamoja na maswali mengi yanayojitokeza, Biteko amesema ni vyema tuachie mamlaka husika kufanya uchunguzi kuhusiana na suala hili “Zaidi ya mwaka Masasi amekuwa akilipwa gawio na mgodi huu, je serikali ya kijiji cha Ngula ilikuwa wapi, mbona serikali ya kijiji haizungumzii eneo lingine isipokuwa eneo la mgodi,” aliuliza Biteko.

Wakati huo huo Biteko ameutaka Mgodi wa Nyati Resources ltd kutoa maelezo ni kwa nini tangu mwaka 2017 Desemba walipoanza uzalishaji wa dhahabu wamelipa Mrabaha wa kiasi cha Shilingi 200,000/- tu wakati mapato yao ni zaidi ya milioni 50.

“Huo ni ukiukwaji wa ulipaji wa kodi za Serikali, haiwezekani tangu mwaka jana hadi leo mmefanikiwa kulipa Mrabaha wa laki mbili tu,” alisema Biteko. Aliongeza kuwa lazima wazawa kuonesha mfano mzuri wa kulipa kodi ili hata wawekezaji kutoka nje ya nchi wakija waone umuhimu wa kulipa kodi.

Kwa upande wake Meneja wa Mgodi wa Nyati Resource ltd, Christopher Nilla amekiri kuwa kweli kumekuwepo na mapungufu katika ulipaji wa kodi za Serikali lakini na kuahidi kubadilika na kulipa sawasawa na sheria ya madini na kubainisha kuwa wanamiliki mgodi mwingine ambapo zaidi ya Tsh milioni kumi zimelipwa serikalini. 


Mkazi wa kijiji cha Ngula, Mindi Masasi (kushoto) akimsikiliza Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko (hayupo pichani). Katikati ni Mtoto wa Mindi Masasi, Makanika Chalo pamoja na Mwenyekiti wa kata ya Bujula (jina halikupatikana)
Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko akihutubia wananchi wa kijiji cha Ngula na wachimbaji wadogo wadogo wa mgodi wa Nyati Resources Ltd (hawapo pichani) katika mkoa wa Geita tarehe 2 Novemba, 2018
Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko akizungumza na wananchi wa kijiji cha Ngula mara baada ya kukagua Mgodi wa Nyati Resources Ltd uliopo katika kijiji cha Ngula kata ya Bujula mkoani Geita.

No comments: