Wednesday, October 3, 2018

SERIKALI YAWAPA WAKULIMA MIKOPO YA SH. BIL. 56.45-MAJALIWA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akihutubia katika Maadhimisho ya Miaka 25 ya Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (MVIWATA) kwenye uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro, Oktoba 3, 2018.
 
Baadhi ya washiriki wa Maadhimisho ya Miaka 25 ya Mtandao wa Vikundi vya Wakulima (MVIWATA) wakimsikiliza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kwenye uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro, Oktoba 3, 2018. 
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Balozi wa Uswiss nchini, Florence Tinguely Mattli katika Maadhimisho ya Miaka 25 ya Mtandao wa Vikundi vya Wakulima (MVIWATA) kwenye uwanja wa Jamhuri Mjini Morogoro, Octoba 3, 2018. 
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa mkulima wa uyoga, Maria Shindika wa Mvomero (kulia) kabla ya kuhutubia katika Maadhidhimisho ya Miaka 25 ya Mtandao wa Vikundi vya Wakulima (MVIWATA) yaliyofanyika kwenye uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma, Oktoba 3, 2018. 
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kuhusu unga na bidhaa mbalimbali zinaotokana na zao la soya kutoka kwa Julie Bwire wa Mvomero (kushoto) kabla ya kuhutubia katika Maadhimisho ya miaka 25 ya Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania kwenye uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro, Oktoba 3, 2018. 
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimina na Mlezi wa Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (MVIWATA) na Mkuu wa Mkoa Mstaafu, Stephen Mashishanga wakati alipowasili kwenye uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro kumwakilisha Rais, John Pombe magufuli katika Maadhimisho ya Miaka 25 ya MVIWATA, Oktoba 3, 2018. Wapili kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dkt. Stephen Kebwe. Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu

*Asema zaidi ya wakulima wadogo 527,000 katika Mikoa 13 wamenufaika 


WAZIRIMKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali imetoa mikopo yenye thamani ya sh. bilioni 56.45 kwa ajili ya miradi mbalimbali ya kilimo katika mikoa 13 hapa nchini.

Amesema mikopo hiyo imetolewa katika kipindi cha kuanzia Agosti 2015 hadi Septemba 2018, kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB).Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatano, Oktoba 3, 2018) kwenye maadhimisho ya miaka 25 ya Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (MVIWATA) mjini Mororogo.

Mikopo hiyo imewanufaisha wakulima wadogo zaidi ya 527,000 waliopo kwenye mnyororo wa thamani wa mazao ya kahawa, karafuu, mahindi, mbogamboga na mazao mengine.Amesema Serikali inatekeleza mipango mbalimbali kwa lengo la kutatua kero zinazowakabili na kuwawezesha wakulima wadogo kujikwamua kiuchumi kupitia kilimo. 

Amesema Juni 14, mwaka huu Rais Dkt. John Magufuli, alizindua Awamu ya Pili ya Programu ya Kuendeleza Kilimo hapa nchini (ASDP II) yenye lengo la kuboresha sekta ya kilimo.Waziri Mkuu amesema ASDP II inalenga kuhakikisha sekta ya kilimo inapewa kipaumbele stahiki ili iweze kuleta tija kwa wakulima wenyewe na Taifa kwa ujumla.

“Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha sekta ya kilimo ikiwemo kutoa mikopo kwa wakulima wadogo; kuondoa baadhi ya tozo zenye kufifisha uzalishaji.” Pia kuweka mipango mizuri ya matumizi bora ya ardhi na kutafuta masoko pamoja na kuongeza thamani kwenye mazao ya kilimo ili kumuongezea tija mkulima.

Kadhalika, Waziri Mkuu ameongeza kuwa mchango wa wakulima wadogo umewezesha Taifa kujitosheleza kwa chakula na hata kuuza nje ya nchi mazao ya kilimo. Hivyo, Waziri Mkuu ametoa rai kwa viongozi na watendaji wa Serikali kujenga utamaduni wa kuhudhuria wa kukutana na kuzungumza na wakulima kuhusu mahitaji hayo.

“Tunafahamu kwamba wakulima mna changamoto nyingi zikiwemo za kisera, kirasilimali na kiutendaji kwenye masuala ya ardhi, masoko, mitaji na hata kero za tozo na ushuru.”Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameagiza Wakala wa Vipimo nchini (WMA) waendesha msako utakaowanasa wafanyabiashara wanaowaibia wakulima kwa njia ya udanganyifu wa kutumia vipimo visivyo sahihi.

Waziri Mkuu amesema mfanyabiashara yeyote atakayebainika kuwaibia wakulima kwa kutumia vipimo visivyo rasmi achukuliwe hatua za kisheria. 
“Utaratibu wa kutumia vipimo visivyo rasmi ambavyo vimepewa majina ya lumbesa, kangomba, umejileta mwenyewe na mengine mengi lazima ukomeshwe.”

Waziri Mkuu ameuagiza uongozi wa WMA kwa kushirikiana na halmashauri zote nchini wahakikishe mazao ya wakulima yanauzwa kwa kutumia vipimo rasmi ili wasiendelee kupunjwa.Akizungumzia kuhusu kero ya ardhi, Waziri Mkuu amesema Serikali itawapa wananchi ardhi inayotwaliwa kutoka kwa wawekezaji au wamiliki walioshidwa kukidhi masharti na yale yasiyoendelezwa kwa muda mrefu

No comments: