Wednesday, October 10, 2018

MAWAZIRI WA SEKTA YA KILIMO WATUAMA JIJINI DODOMA KUJADILI UTEKELEZAJI WA ASDP AWAMU YA PILI

Waziri wa Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na walemavu Mhe Jenista Mhagama (Mb) akizungumza jambo wakati akifungua kikao cha Mawaziri wa sekta za kilimo juu ya utekelzaji wa Mpango wa kuendeleza sekta ya kilimo awamu ya pili (ASDP II) leo tarehe 10 Octoba 2018. (Picha Zote Na Mathias Canal-WK)
Kutoka kushoto ni waziri wa ardhi, nyumba na maendeleo ya makazi Mhe Willium Lukuvu (Mb), Waziri wa kilimo Mhandisi Dkt Charles Tizeba (Mb) na Naibu waziri wa Fedha na Mipango Dkt Ashatu Kijaji wakifatilia kwa umakini kikao cha Mawaziri wa sekta za kilimo juu ya utekelzaji wa Mpango wa kuendeleza sekta ya kilimo awamu ya pili (ASDP II) leo tarehe 10 Octoba 2018.
Waziri wa kilimo Mhandisi Dkt Charles Tizeba (Mb) akieleza umuhimu wa kuanza haraka utekelezaji wa ASDP II wakati wa kikao cha Mawaziri wa sekta za kilimo juu ya utekelzaji wa Mpango wa kuendeleza sekta ya kilimo awamu ya pili (ASDP II) leo tarehe 10 Octoba 2018.
Waziri wa ardhi, nyumba na maendeleo ya makazi Mhe Willium Lukuvu (Mb), akisisitiza jambo wakati wa kikao cha Mawaziri wa sekta za kilimo juu ya utekelezaji wa Mpango wa kuendeleza sekta ya kilimo awamu ya pili (ASDP II) leo tarehe 10 Octoba 2018. Mwingine ni Waziri wa kilimo Mhandisi Dkt Charles Tizeba.
Naibu waziri wa Fedha na Mipango Dkt Ashatu Kijaji akieleza utayari wa ushiriki wa wizara yake wakati wa kikao cha Mawaziri wa sekta za kilimo juu ya utekelzaji wa Mpango wa kuendeleza sekta ya kilimo awamu ya pili (ASDP II) leo tarehe 10 Octoba 2018.
Waziri wa Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na walemavu Mhe Jenista Mhagama (Mb) akizungumza jambo wakati akifungua kikao cha Mawaziri wa sekta za kilimo juu ya utekelzaji wa Mpango wa kuendeleza sekta ya kilimo awamu ya pili (ASDP II) leo tarehe 10 Octoba 2018.



Na Mathias Canal, WK-Dodoma

Mawaziri wa wizara za sekta ya kilimo leo tarehe 10 Octoba 2018 wametuama kwa masaa kadhaa Mjini Dodoma katika Ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu kujadili kwa kina kuhusu maandalizi ya utekelezaji wa Mpango wa kuendeleza sekta ya kilimo awamu ya pili (ASDP II).

Wizara washirika katika kutekeleza ASDP II ni pamoja na Wizara ya kilimo, Wizara ya mifugo na Uvuvi, Wizara ya Viwanda, Biashara, na Uwekezaji Wizara ya Maji, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya makazi, na Ofisi ya Rais-TAMISEMI.

Utekelezaji wake utachagizwa pia na Wabia wa maendeleo, Sekta binafsi, Taasisi zisizo za kiserikali, Wakulima, Wafugaji na Wavuvi.Mawaziri hao wakiongozwa na Mwenyekiti ambaye ni Waziri wa Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na walemavu Mhe Jenista Mhagama (Mb) wameridhia kwa pamoja kuanza haraka utekelezaji wa mradi huo wa ASDP II ambao utakuwa chachu ya ukuzaji wa uchumi kupitia kilimo.

Majadiliano hayo yalijikita zaidi kujadili mapendekezo ya kikao cha makatibu wakuu wa wizara za sekta ya kilimo kilichofanyika tarehe 30 Agosti 2018 pia kujadili namna bora ya Uratibu wa ASDP II, na Mikakati ya kutafuta fedha za kugharamia utekelezaji wa ASDP II.

Katika Mkutano huo Mwenyekiti ambaye ni Waziri wa Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na walemavu Mhe Jenista Mhagama (Mb) aliitaka timu ya ASDP II Taifa kueleza kwa kina mikakati ya kuboresha masoko ya mazao ya kipaumbele yaliyoainishwa katika utekelezaji wa ASDP awamu ya pili.

Alisema kuwa kumekuwa na uhamasishaji mkubwa kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kulima pindi unapofika msimu wa kilimo lakini bado hamasa ya kutafuta masoko ni ndogo jambo ambalo linageuka karaha kwa wakulima nchi hivyo muarobaini wa kutafuta masoko ndio njia pekee ya kumkomboa mkulima.

Kwa upande wake Waziri wa Kilimo Mhandisi Dkt Charles Tizeba akizungumza katika kikao hicho alisema kuwa “ Majira ya Nchi yetu tunaendeshwa na msimu wa kilimo hivyo tunapaswa kutekeleza mpango wa kuendeleza sekta ya kilimo kwa haraka ili kuendana na msimu” Alisema

Aidha, alisema kuwa punde utekelezaji utakapoanza wafadhili wa mradi huo wanapaswa kupewa uhuru wa kuchagua eneo watakalosaidia ili kuongeza chachu na ufanisi wa haraka katika uwajibikaji. Naye Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Dkt Ashatu Kijaji amewahakikishia mawaziri hao wa sekta za kilimo kuwa, wizara yake imejipanga vyema katika utekelezaji wa Mpango wa kuendeleza sekta ya kilimo awamu ya pili (ASDP II).

“ Wengi wamezoea kuiita wizara yetu kama wizara ya madeni sasa tumejipanga vyema katika utekelezaji wa ASDP II kwani tunaamini kabisa kuwa ili kuwa na uchumi mzuri ulioimarika kwa wananchi na Taifa kwa ujumla tunahitaji kuwa na kilimo madhubuti “ Alikaririwa Dkt Kijaji

ASDP II inalenga katika mnyororo wa thamani wa mazao ya kipaumbele na ikolojia ya kanda ya kilimo tofauti na utekelezaji wa ASDP awamu ya kwanza ambao ulifanyika nchi nzima na kuwa na miradi karibu sekta ndogo zote za serikali na vipaumbele na maamuzi ya uwekezaji wa Mamlaka za serikali za mitaa.

Katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa ASDP II Mazao ya kipaumbele yaliyochaguliwa kwa kilimo ni Mchele, Mahindi, Mtama/Uwele, Muhogo, Mboga/Matunda, Mazao ya Mbegu za mafuta (Alizeti, Ufuta, Nazi, Michikichi n.k) Pamba, Kahawa, Sukari, Korosho, Chai, Viazi mviringo na vitamu, Mikunde, Ndizi, na kwa Mifugo na Uvuvi ni Maziwa, Nyama (Ng’ombe), Mbuzi na Kondoo, Kuku, samaki na Mwani.

Malengo ya ASDP II ni kuleta mageuzi ya sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ili kuongeza uzalishaji na tija, kufanya kilimo kiwe cha kibiashara zaidi na kuongeza pato la wakulima wadogo kwa ajili ya kuboresha maisha yao, usalama wa chakula na lishe.

No comments: