Wednesday, September 26, 2018

MKANDARASI WA MRADI WA MAJI TUNDUMA APEWA MWEZI MMOJA KUKAMILISHA KAZI, NA MKANDARASI ALIYETELEKEZA MARADI WA MAJI GALIJEMBE APATIKANA

Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhe. Jumaa Aweso (Mb) ametoa muda wa mwezi mmoja kwa mkandarasi wa mradi wa maji Tunduma kukamilisha kazi hiyo. 

Mhe. Aweso (Mb) ametoa muda huo mjini Tunduma baada ya kukagua mradi huo ambao umekamilika kwa asilimia 93 na kusisitiza atarudi kuufungua baada ya muda aliotoa kukamilika. Amesema wananchi wanasubiri majisafi na salama kutoka katika mradi huo ambao Serikali imetoa kiasi cha Shilingi milioni 895 kuhakikisha huduma inawafikia wananchi. 

Wakati huohuo, Mhe. Aweso (Mb) amewaelekeza Wahandisi wa Maji mkoani Mbeya kufanya kazi kwa weledi na kuepuka vishawishi ambavyo vinaharibu taaluma yao na kazi. Mhe. Aweso amesema hayo katika kikao kazi kilichowakutanisha Wahandisi wa maji wa mkoa wa Mbeya, jijini Mbeya. Amewaelekeza moja ya kazi wanayotakiwa kufanya ni kutembelea miradi na kujiridhisha na ubora wake, pia kujua kinachofanyika katika ujenzi na sio kukaa maofisini. 

Mhe. Aweso (Mb) amesema mradi ukijengwa katika kiwango bora na wananchi wakapata huduma nzuri jambo hilo ni moja kati ya kumbukumbu muhimu kwa wote waliofanya kazi, na kusisitiza wahandisi wote wanaofanya vizuri watatambuliwa kwa ubora wa kazi walizosimamia. 

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini 
Wizara ya Maji na Umwagiliaji 
25.09.2018

Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhe.Jumaa Aweso (Mb), akiongea na vyombo vya habari katika eneo la mradi wa maji Tunduma. Mkandarasi wa mradi huo kapewa mwezi mmoja kukamilisha kazi. 
Watumishi wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira jijini Mbeya wakiwa katika kikao na Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhe.Jumaa Aweso (Mb), hayupo pichani, jijini Mbeya.
Katibu Mkuu Wizara ya Maji na Umwagiliaji Profesa Kitila Mkumbo (kushoto) akimkaribisha Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhe. Jumaa Aweso (Mb) kuongea na watumishi wa Mamlaka ya Maji jijini Mbeya.
Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhe.Jumaa Aweso (Mb), akiongea na Wahandisi wa Maji wa mkoa wa Mbeya kuhusu uwajibikaji katika miradi ya maji.
Wahusika walioshiriki katika kusimamia mradi wa Maji Galijembe mkoani Mbeya, Wahandisi wa majina na mkandarasi-kampuni ya Black Dot, wakiwa katika gari la Polisi ili kusaidia kuhusu mkandarasi kulipwa na mradi kutokamilika. 
Mhusika kutoka kampuni ya Black Dot iliyopewa kandarasi ya mradi wa maji Galijembe mkoani Mbeya, na kuutelekeza, pamoja na Mhandisi aliyehusika katika mradi huo, wakitoa maelezo yao kwa Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Jumaa Aweso (Mb), hayupo pichani.
Mmoja kati ya wahusika wa kampuni ya Black Dot iliyopewa kandarasi ya ujenzi wa mradi wa maji Galijembe mkoani Mbeya akitoa maelezo ya kutokamilika mradi kwa Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhe. Jumaa Aweso, MB, (hayupo pichani) . 
Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhe.Jumaa Aweso (Mb), akipanda kukagua moja ya tanki la kuhifadhi maji la mradi wa Mlowo mkoani Mbeya.
Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhe.Jumaa Aweso (Mb), akiangalia maendeleo ya ujenzi wa chujio la maji katika mradi wa maji wa Vwawa mkoani Mbeya. 

No comments: