Thursday, June 21, 2018

PASS YATAMBULISHA FURSA MPYA YA MIKOPO KWA WADAU WA SEKTA YA KILIMO NCHINI.

Na Dixon Busagaga wa Globu ya Jamii .

Taasisi ya kusaidia sekta binafsi ya kilimo nchini (PASS) imeingia makubaliano na Mfuko wa uwekezaji wa biashara na kilimo Afrika (AATIF) kusaidia wadau wa sekta ya Kilimo nchini kwa kutoa mikopo mikubwa itakayowezesha utekelezwaji wa miradi mikubwa ya kilimo.

Makubaliano haya baina ya PASS na AATIF yanatajwa kuwa mkombozi wa changamoto za muda mrefu za wadau wa sekta ya Kilimo ambao wamekuwa wakipitia kwa kushindwa kupata mikopo ya muda mrefu kutoka kwa taasisi za kifedha hapa nchini kutokana na ufinyu wa muda wa urejeshwaji wa mikopo hiyo. 

Kwa kiasi kikubwa hali hii imekuwa ikitajwa kama sababu ya sekta hii kushindwa kuwa na maendeleo makubwa kutokana na mipango mingi kujikita katika uwekezaji wa muda mfupi. 

Akizungumza wakati wa hafla fupi ya kutambulisha fursa hiyo kwa wadau wa kilimo na baadhi ya taasisi za fedha iliyofanyika mapema leo asubuhi katika Hotel ya Serena jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa PASS Bwana Nicomed Bohay amesema.hatua ya upatikanaji wa mikopo mikubwa na ya muda mrefu kwa wadau wakubwa wa kilimo utachochea ukuaji wa sekta ya kilimo. 

“Malengo yetu sisi ni kutengeneza mashirikiano baina ya taasisi hizi ili ziweze kupata mikopo hii, imani yetu kama PASS nikuwa itachochea uwekezaji mkubwa katika maeneo mbalimbali ya kilimo na hivyo kuifanya sekta ya kilimo nchini kuwa mdau mkubwa wa falsafa ya serikali ya awamu ya tano ya kuziwezesha sekta binafsi na hasa kilimo katika kushiriki katika uchumi wa viwanda” Amesema Bwana Nicomed Bohay. 

Naye Mwakilishi wa AATIF, Bwana Samuel Ndonga akizungumza katika hafla hiyo amesema, makubaliano hayo ni sehemu ya jitihada za taasisi yake kuunga mkono kiu ya siku nyingi ya Taasisi ya PASS, ambayo imekuwa ikitamani kumpunguzia changamoto mdau wa kilimo kwa kumhakikishia upatikanaji wa mikopo ya uhakika na nafuu kupitia taasisi za kifedha. 

“AATIF kwa kushirikiana na PASS tumedhamiria kuwawezesha wakulima wakubwa kwa wadogo kufikia ndoto ya kuendesha miradi mikubwa ya Kilimo hapa Tanzania,imani yetu ni kuwa Wadau mbalimbali kama vile Taasisi za fedha zinazo toa mikopo kwa wakulima, Wazalishaji,Wasindikaji,Wafanyabiashara na Wajasiliamali wengine katika sekta ya Kilimo watachangamkia fursa hii” Amesema Bwana Samuel Ndonga 

Kwa miaka mingi upatikanaji wa mitaji na mikopo kwa sekta ya Kilimo imekuwa ni changamoto kubwa, na kwa ujio huu wa Taasisi ya AATIF sasa tumaini la sekta ya kilimo nchini kupata mikopo kati ya dola za kimarekani milioni tano mpaka thelathini ni la uhakika jambo ambalo linaelezwa kuwa litaleta mapinduzi makubwa ya uchumi nchini kupitia sekta hii ya kilimo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Binafsi ya kusaidia sekta ya kilimo nchini (PASS) Bw,Nicomed Bohay akizungumza wakati wa kutambulisha fursa mpya kwa Wadau wa sekta ya Kilimo. 

Baadhi ya Wadau wa Sekta ya Kilimo wakifuatilia kwa makini maelezo yaliyokuwa yakitolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi ya PASS wakati wa utambulishaji wa fursa mpya kwa wadau wa sekta ya Kilimo.
Mwakilishi wa AATIF, Bwana Samuel Ndonga akizungumza wakati wa hafla hiyo iliyofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam .
Meneja uwekezaji Mashariki na Kusini mwa Afrika wa Mfuko wa UGEAP,Sonja Riedke akizungumza wakati wa hafla hiyo iliyoandaliwa na Taasisi ya PASS. 
Balozi wa Denmark nchini Tanzania ,Einar Jensen akizungumza wakati wa hafla hiyo.
Wadau wa sekt ya Kilimo wakiwa katika picha ya pamoja na watendaji wa taasisi ya PASS ,AATIF pamoja na Balozi wa Denmark nchi Tanzania ,Einar Jensen.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Binafsi ya kusaidia sekta ya kilimo nchini (PASS) Bwana Nicomed Bohayakizungumza na Wanahabari muda mfupi baada ya kumalizika kwa hafla hiyo.

No comments: