Wednesday, May 9, 2018

CHUO KIKUU MZUMBE CHAJADILI SEKTA ISIYO RASMI

 Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe (Utawala na Fedha), Prof. Ernest Kihanga, akisoma hotuba yake kwa niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe, Prof. Lughano Kusiluka jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa Mradi wa Miaka Minne utakaotafiti na kuonyesha njia sahihi ya sekta isiyo rasmi kupata Huduma za Hifadhi za Jamii.
Baadhi ya washiriki wa kongamano hilo.
Washiri kutoka ndani na nje ya nchi.
Abbas Cothema Ofisa Matekelezo kutoka Kitengo cha Hiari-NSSF akiwa katika kongamano hilo.
 Meza Kuu.



Lone Riisgaard kutoka Chuo Kikuu cha Roskilde, akitoa mada.
Lone Riisgaard kutoka Chuo Kikuu cha Roskilde, akitoa mada.

Anne Kamau kutoka Institute Development Studies (IDS) Chuo Kikuu cha Nairobi akitoa mada kuhusu sekta isiyo rasmi katika Huduma za Hifadhi za Jamii.
Washiriki.
Washiriki.


Abbas Cothema Ofisa Matekelezo kutoka Kitengo cha Hiari-NSSF akitoa mada katika kongamano hilo.
Abbas Cothema Ofisa Matekelezo kutoka Kitengo cha Hiari-NSSF akitoa mada katika kongamano hilo.
Mhadhiri Chuo Kikuu Mzumbe, Dk. Godbertha Kinyongo, akizungumza na wandishi wa habari.

NA MWANDISHI WETU
LICHA ya kuchangia asilimia 35 katika pato la taifa, bado sekta isiyo rasmi haijapewa uzito unaostahili kwa kutoshiriki ipasavyo kwenye hifadhi za jamii.
Hayo yalisemwa Dar es Salaam na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe Kampasi ya Dar es Salaam, Dk. Godbertha Kinyondo wakati wa uzinduzi wa Mradi wa miaka minne utakaotafiti na kuonesha njia sahihi ya Sekta isiyo rasmi kupata huduma za hifadhi za jamii.
“Tumeona tufanye utafiti ili kuona namna sahihi ya kusaidia waliojiajiri kwenye sekta isiyorasmi kwa kuwa ni kundi kubwa linalofanya biashara ndogondogo zinazochangia karibu asilimia 35 kwenye pato la taifa.
“Katika mradi huu tunaziangalia sekta za aina tatu zisizo rasmi kwanza ujenzi, usafirishaji na wajasiriamali ambao ndio kundi kubwa… kama bodaboda vijana wetu wengi wamejiajiri humu lakini hawana taarifa za kutosha kuhusu haki yao ya kuingia kwenye hifadhi za jamii.
“Hawa mama lishe wengi lakini jiulize wangapi wamejisajili na NSSF? Wangapi wanazo kadi za bima ya afya? Hawa madereva wa bodaboda kila leo wanapata ajali wangapi wanazo bima za matibabu?.
“Hao ndio tunaowazungumzia na tumewaalika kwenye warsha hii waje waseme changamoto zao na tutawaambia namna ya kutoka huko ili wafanye kazi zao kwa furaha na amani wajue kwamba mchango wao kwa taifa ni mkubwa,” alisema Dk. Kinyondo.
Kuhusu mradi huo, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Utawala na Fedha, Profesa Ernest Kihanga aliyemwakilisha Makamu Mkuu wa Chuo cha Mzumbe, alisema mradi huo ulioanza mwaka 2017 hadi mwaka 2020 umeshirikisha wasomi kutoka nchi tatu tofauti kwa ufadhili wa Shirika la Msaada la watu wa Denmark (DANIDA).
Alivitaja vyuo vilivyoshiriki kwenye mradi huo wa utafiti kuwa ni Chuo Kikuu cha Roskile kutoka Denmark, Chuo Kikuu cha Nairobi cha Kenya na Mzumbe kutoka Tanzania.
Alisema utafiti uliofanywa na Shirika la Kazi Duniani (ILO) mwaka 2014 ulionesha kwamba watu wanane kati ya 10 waliopata kazi kwa mara ya kwanza walikuwa kwenye sekta isiyo rasmi.
“Ni ukweli usiopingika kwamba sekta isiyo rasmi inakuwa kwa kasi… sio tu hapa Tanzania ama Kenya, bali katika nchi nyingi zinazoendela ulimwenguni kote.
“Ninafahamu kwamba watafiti mbalimbali wamekwishafanya tafiti katika sekta hii kwa ujumla wake na hasa katika kuangalia jinsi gani shughuli za wafanyakazi katika sekta hii zinaweza kurasimishwa.
“…Umasikini wa mahitaji muhimu ambao inamaanisha uwezo wa mwananchi kushindwa kujipatia mahitaji muhimu ya maisha umepungua kutoka asilimia 34.4 mwaka 2006 mpaka asilimia 28.2 mwaka 2012.
“Katika kipindi hicho hicho, umasikini uliokithiri ulipungua kutoka asilimia 11.7 mpaka asilimia 9.7 ingawa kuna ukuaji unaowasaidia wananchi masikini, bado maandiko yanasema asilimia 70 ya watanzania wanaishi chini ya Dola mbili za Marekani kwa siku.
“Hakika, wengi walioko katika biashara hii ya bodaboda, ama wafanyabiashara ndogondogo ama mafundi ujenzi hawana aina yoyote ya ulinzi wa kijamii inayowalenga.
“Nilikua nasoma ripoti ya polisi ya usalama barabarani ya mwaka 2016 kwa bodaboda pekee na imeonyesha mfano mwaka 2014 kulikua na ajali 4,169 zilizosababisha vifo 928 na majeraha 3,884; mwaka 2015 kulikua na ajali 2,626, vifo 934 na majeraha 2,370.
“…Kwa robo mwaka pekee ya mwaka 2016 kulikua na ajali 663; vifo 200 na majeraha 559,” alisema Profesa Kihanga.

No comments: