Sunday, April 29, 2018

PROFESA KABUDI AFUNGUA BARAZA LA WAFANYAKAZI TUME YA KUREKEBISHA SHERIA


Na Munir Shemweta, Morogoro

Waziri wa Katiba na Sheria Profesa Palamagamba Kabudi amesisitiza umuhimu wa kuwashirikisha watumishi katika mipango ya uendeshaji Taasisi kwa kuwa suala hilo lipo kisheria.

Aidha, alisema kwa miaka yote Serikali imekuwa ikisisitiza Taasisi kujenga na kutekeleza utaratibu wa kushirikisha watumishi na hali hiyo inatokana na ukweli kuwa palipo na watumishi wengi pana mawazo mengi.Profesa Kabudi alisema hayo mwishoni mwa wiki wakati akifungua mkutano wa kumi na tatu wa Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania uliofanyika katika ukumbi wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) mkoani Morogoro.

‘’Ushirikishwaji watumishi kwenye mipango ya uendeshaji ofisi unasaidia kupata mawazo mengi na mapya yanayoweza kurahisisha uendeshaji wa ofisi na kutoa fursa ya kusikiliza kero na changamoto kwenye uendeshaji wa Taasisi na kushirikiana katika kutafuta ufumbuzi’’ alisema profesa Kabudi.

Aliongeza kuwa, kwa kushirikiana na watumishi ni dhahiri wanapata morari wa kushiriki kikamilifu kwenye utekelezaji wa mipango ya taasisi ambayo wao wenyewe walishiriki kuiandaa.Waziri huyo wa Katiba na Sheria alisema, ushirikishwaji unafanywa kupitia baraza la wafanyakazi kwa kuwa baraza ni chombo kinachowashirikisha wafanyakazi katika kupanga , kusimamia na kutekeleza mipango mbalimbali inayohusu shughuli za kazi za Taasisi kama zilivyoainishwa katika sheria za nchi.

Kwa mujibu wa Profesa Kabudi, Mabaraza hutoa fursa kwa wafanyakazi kushiriki katika maamuzi mbalimbali na kuboresha uhusiano baina ya wafanyakazi na uongozi pamoja na mazingira ya utendaji hasa mahala pa kazi hivyo baraza ni chombo cha kuimarisha na kuboresha demokrasia mahala pa kazi.

Amewataka wajumbe wa baraza wa Tume ya Kurekebisha Sheria kuzingatia suala la nidhamu kazini, misingi ya kazi na kutekeleza majukumu kwa kuzingatia sheria, kanuni, taratibu. Aidha, alitaka uzembe kazini upigwe vita na suala la kufanya kazi kwa mazoea kukomeshwe na kubainisha kuwa,vipaumbele viwekwe katika kulinda rasilimali za Tume na kuwa na nidhamu katika matumizi ya fedha na mali zake.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Kurekebisha Sheria ambaye ni Katibu Mtendaji Tume Casmir Kyuki alisema katika kipindi cha Julai 2017 hadi Machi 2018 Tume yake imeweza kutekeleza majukumu yake kama yalivyoainishwa katika bajeti.

Ameyataja majukumu hayo kuwa ni kufanya mapitio ya Mfumo wa Sheria Unaosimamia Haki Jinai, Sheria ya Ushahidi, Uchambuzi wa Kesi za Mahakama ya Rufaa, Mfumo wa Sheria Unaosimamia Huduma ya Ustawi wa Jamii, Mfumo wa Sheria za Ufilisi pamoja na kutoa elimu ya sheria kwa umma.

Ameishukuru serikali kwa mabadiliko makubwa iliyoyafanya katika sekta ya sheria kupitia tangazo la serikali namba 48,49 na 50 ambapo yameleta muundo mpya kwa kuanzishwa Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka ya Jinai na ile ya Wakili Mkuu wa Serikali ili kuongeza tija na ufanisi katika utendaji kazi.
Waziri wa Katiba na Sheria Profesa Palamagamba Kabudi akifungua mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Kurekebisha Sheria uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine, kushoto ni Katibu Mtendaji wa Tume Casmir Kyuki na kulia ni Katibu wa Baraza Ambokile Mwakasungula (Picha na Munir Shemweta-TUMESHERIA)
Katibu Mtendaji wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania Casmir Kyuki (Kushoto) akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi Waziri wa Katiba na Sheria Profesa Palamagamba Kabudi kufungua mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine mkoani Morogoro, kulia ni Katibu wa Baraza Ambokile Mwakasungula (Picha na Munir Shemweta-TUMESHERIA)
Waziri wa Katiba na Sheria Profesa Palamagamba Kabudi akimsikiliza Katibu Msaidizi wa Tume ya Kurekebisha Sheria Khalist Luanda mara baada ya kufunguka mkutano wa Baraza la Wafanyakazi Tume ya Kurekebisha Sheria uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine mkoani Morogoro, katikati ni Katibu Msaidizi wa Tume (Idara ya Mapitio) Angelah Bahati (Picha na Munir Shemweta-TUMESHERIA)
Sehemu ya Wajumbe Baraza la Wafanyakazi la Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania wakimsikiliza Waziri wa Katiba na Sheria Profesa Palamagamba Kabudi (hayupo pichani) wakati akifungua mkutano huo uliofanyika Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine mkoani Morogoro.
Waziri wa Katiba na Sheria Profesa Palamagamba Kabudi akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Tume ya Kurekebisha Sheria katika Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine mkoani Morogoro.

No comments: