Sunday, April 29, 2018

IDADI YA WAATHIRIKA WA MAFURIKO YA MVUA KATIKA KATA YA MWARU YAFIKIA ZAIDI YA WAKAZI 700

Na Jumbe Ismailly, IKUNGI 

IDADI ya wakazi wa vijiji vya Kaugeri na Mduguyu,kata ya Mwaru,wilaya ya Ikungi waliokosa makazi kutokana na nyumba zao kuanguka kufuatia mvua kubwa zinazoendelea kunyesha Mkoani hapa zimeongezeka kutoka kaya 22 zanye zaidi ya wakazi 154 hadi kufikia kaya 177 zenye zaidi ya wakazi 700 baada ya nyumba189 kuanguka.

Ongezeko la idadi hiyo ya wakazi linatokana na mvua kubwa iliyonyesha apr,16 hadi 18,mwaka huu na kusababisha mto kuacha njia yake na kulenga katika Kitongoji cha Mwasusu,na ndipo kaya 22 zenye zaidi ya wakazi 154 katika vijiji vya Kaugeri na Mduguyu,Kata ya Mwaru kukosa makazi baada ya nyumba 34 kuanguka.u

Ofisa Mtendaji wa Kata ya Mwaru,Hamisi Malongo alisema hayo alipokuwa akitoa taarifa za athari zilizotokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha hivi sasa Mkoani Singida na kuongeza kwamba pamoja na nyumba hizo vile vile makanisa matatu ya FPCT na AIC yalianguka kufuatia mvua hizo.

“Na tuliloligundua sisi kama viongozi kama serikali upande wa kata kwamba vijiji vya Kaugeri na Mduguyu ni vijiji vya mpakani na Mkoa wa Tabora ambavyo ndiyo bonde la Mto Wembere unapita kwa hiyo mvua inaponyesha pande zote za dunia kwa hiyo wao ni rahisi sana kuathirika na mvua hizo.”alisisitiza Malongo.

Naye Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Kaugeri,Laurence Bomba Torokoko akizungumzia hasara zilizotokana na mvua hizo alizitaja kuwa ni pamoja na nyumba 105 zenye wakazi 412 walikosa makazi kabisa ya kuishi na hekari 92 za mazao mbali mbali.

Madhara mengine kwa mujibu wa Torokoko magunia 334 ya mpunga na mtama,kuku 20 na ng’ombe moja amba hatha hivyo alitumia fursa hiyo kuiomba serikali kuwasaidia familia zilizoathirika kutokana na mvua hizo ambazo bado zinaendelea kunyesha.

Kwa upande wao baadhi ya waathirika wa mvua hizo,Mchungaji,Hosea Eliudi licha ya kuishukuru serikali kwa msaada wa awali lakini hakusita kueleza changamoto zinazowakabili kwenye kambi hiyo kuwa ni hatari ya kuugua ugonjwa wa malaria kutokana na kuwepo kwa mbu wengi huku wakiwa hawana vyandarua baada ya walivyokuwa wakitumia kuangukiwa na nyumba zao.

Misaada pamoja na changamoto zingine kwa mujibu wa mchungaji huyo ni mahema makubwa yatakayoimarisha kambi hiyo kufanana na zile za wakimbizi na kuzitaja changamoto zingine kuwa ni kushindwa kuvuna kwa kuwa hawana sehemu ya kuhifadhi mazao yao.

Mashiri Masunga mkazi wa ni mmoja waathirika wa mafuriko ya mvua hizo kwa upande wake anaelekeza shutuma zake kwa Mbunge wa jimbo la Singida Magharibi,Elibariki Kingu kwamba licha ya kuwaahidi kuwapelekea kadi za CCM pamoja na maturubai tangu apr,23,mwaka huu lakini wamejikuta wakiende na matatizo ya kutokuwa na kifaa hicho muhimu kwa kujikinga na mvua.
Mmoja wa wananchi walioathirika kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha akiwa kwenye makazi yake mapya yaliyopo kitongoji cha Mwasusu,Kijiji cha Kaugeri akihofia wingu lililotanda kama alivyokutwa na kamera ya kituo hiki(Picha zote Na Jumbe Ismailly)
Baadhi ya wakazi wa vijiji vya Kaugeri na Mduguyu,kata ya Mwaru,wilayani Ikungi wakihamisha baadhdi ya vitu vilivyosalia kwenye makazi yao ya zamani na kuhamia kwenye eneo lililotengwa na serikali kwa ajili ya wahanga hao wa mafuriko yaliyotokana na mvua zilizonyesha kwa sisku tatu mfululizo na hivyo kusababisha zaidi ya wakazi 700 kukosa mahali pa kuishi
Ni Miundombinu ya barabara ya kutoka Mlandala kwenda kwenye Kitongoji cha Mwasusu,Kijiji cha Kaugeri sehemu iliyotengwa kwa ajili ya wahanga wa mafurriko ya mvua zilivyoharibika kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha Mkoani Singida.

No comments: