Monday, March 12, 2018

FIRE KLABU ZITUMIKE KUZUIA MAJANGA YA MOTO SHULENI - ZIMAMOTO

Mkaguzi Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Emmanuel Kibona akitoa elimu ya Kinga na Tahadhari Dhidi ya Majanga ya moto kwa Walimu na Wanafunzi wa Shule ya Secondari Azania (Picha na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji)

Na Nasibu Mgosso. 

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ndicho chombo chenye jukumu la kuzuia na kukabiliana na majanga mbalimbali kama mafuriko , Tetemeko la Ardhi, ajali za vyombo vya usafiri na usafirishaji, kuporomoka kwa majengo, migodi, pamoja na matukio ya moto.

Mara kwa mara, majanga ya moto yamekuwa yakitokea katika jamii yetu kwa sababu moto ni sehemu ya maisha yetu ya kila siku. Utafiti umethibitisha kwamba, vyanzo vingi vya moto ni sisi wenyewe (binadamu) kutokana na uzembe, hujuma au kutokukuwa na elimu ya Tahadhali na Kinga Dhidi ya Moto.

Aidha, matukio ya moto yamekuwa yakitokea mara kwa mara katika shule za bweni hapa nchini hususani shule za sekondari, na kusababisha uharibifu wa miundo mbinu kama vile Mali, majengo na wakati mwingine majeraha au vifo kwa wanafunzi wetu na kuleta simanzi na sintofahamu kwa Wananchi na Taifa kwa ujumla .
Picha ni sehemu ya bweni iliyoathirika na moto na kuteketeza mali za Wanafunzi.

Uchunguzi wa moto (Fire Investigation) umebaini sababu za matukio hayo ni matumizi mabaya ya umeme yanayofanywa na wanafunzi kwa kujiunganishia nyaya za umeme wenyewe bila kuwa na weledi iliwapate sehemu za kuchaji simu na heater za kuchemshia maji kwa kificho kwa sababu Wanafunzi hawaruhusiwi kuwa na simu wala heater pindi wanapokuwa shuleni.

Lakini pia sababu nyingine ni matumizi ya mishumaa, unapokatika umeme wakati wa kujisomea. Shule nyingi zinajaribu kuzuia mabweni kutumika kama sehemu za kujisomea, lakini bado wapo baadhi ya Wanafunzi wanaamua kujisomea ndani ya mabweni bila kuchukua tahadhari yoyote na wanapopitiwa na usingizi, uacha mishumaa inaendelea kuwaka na hatimaye kusababisha ajali ya moto.

Utakumbuka miaka kadhaa iliyopita matukio kama haya ya kuungua kwa shule yalileta majonzi makubwa kwa kuangamiza maisha ya Wanafunzi wengi. Kuungua kwa shule ya Shauritanga Mkoani Kilimanjaro mwaka 1994 ambapo zaidi ya wanafunzi 40 walipoteza Maisha pamoja na Mali.

Mwaka 2009 shule ya sekondari Idodi Mkoani Iringa iliteketea kwa moto na zaidi ya wanafunzi 20 walipoteza Maisha pamoja na Mali. Hiyo ni mifano tu lakini matukio ya kuungua kwa shule ni mengi sana hapa nchini.

Ili kupunguza matukio hayo, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limeanzisha Fire klabu katika shule mbalimbali za Msingi na Sekondari ili kupata wajumbe watakaoliwakilisha katika shule na makazi yao. Kwa kutumia fire klabu, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limejenga ukaribu mkubwa na Wanafunzi wa shule hizo, hatua inayosaidia kuwapa elimu stahiki ya kukabiliana na majanga ya moto.

Changamoto iliyopo ni mapokeo ya baadhi ya Viongozi wa shule kutokuwa tayari kuruhusu shule zao kuanzisha klabu za Zimamoto zinazosimamiwa na kuratibiwa na Jeshi hilo ambapo mpaka sasa ni shule 100 ndizo zilizofungua klabu hizo kwa nchi nzima.

Kama nilivyo eleza hapo mwanzo, lengo la klabu hizo ni kuwapa fursa wanafunzi kuwa familia moja na wataalamu wa Zimamoto. Ukaribu huo hutumika kwa wazimamoto kuwapa mbinu mbalimbali za kuzuia na kukabiliana na vyanzo vya moto.

Lakini kwa upande wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, ni kupanua wigo wa kuwa na idadi kubwa ya watu, wanaoifahamu vyema elimu hiyo na kuwa mabalozi wazuri watakao liunganisha Jeshi na jamii kwa kufikisha elimu hiyo, Mijini na Vijijini na hatimaye kuweza kupunguza na kutokomeza kabisa majanga.

Wito wangu kwa wamiliki wa shule, walipokee jambo hili kama ukombozi kwao kupunguza majanga ya moto katika shule zao. Tukishirikiana tutapunguza majanga ya moto, na Taifa litakuwa salama. Mungu ibariki Afrika Mungu ibariki Tanzania.

No comments: