Sunday, March 4, 2018

CHUMVI, CHOKAA ZINAWEZA KUITAJIRISHA KIGOMA - NYONGO


Na Veronica Simba – Kigoma 

Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo, amesema kwamba ikiwa wananchi wa Kigoma watatumia vyema fursa za upatikanaji wa Madini ya Chumvi na Chokaa, zilizopo katika Mkoa huo, wanaweza kutajirika. 

Akihitimisha ziara yake katika Mkoa huo, jana Machi 3, baada ya kutembelea Migodi mbalimbali ya Madini ya Chokaa na Chumvi, Nyongo aliwaeleza waandishi wa habari kuwa upatikanaji wa Chumvi na Chokaa ni neema kwa wananchi hao kutokana na uhitaji wake mkubwa katika maisha ya kila siku. 

“Ni fursa kubwa sana kwa wananchi wa Kigoma. Wasidhani kwamba fursa iliyopo hapa ni ya uvuvi na mawese peke yake; wanaweza kuwa matajiri wakubwa kupitia Madini ya Chokaa na Chumvi.” 

Akifafanua zaidi, Nyongo alisema kuwa, katika siku mbili za ziara yake mkoani Kigoma, ameshuhudia maeneo mengi yenye Chokaa ya kutosha na kwamba uzalishaji wake ni rahisi sana kwani kinachohitajika ni kuyachoma mawe husika na kusaga; basi. 

Akizungumzia upande wa Chumvi, alisema kuwa, Mgodi wa kuzalisha Chumvi wa Nyanza, uliopo Uvinza unafanya kazi nzuri katika uzalishaji lakini kwa bahati mbaya asilimia 70 ya bidhaa wanayozalisha, huiuza nje ya nchi hususan katika nchi jirani za Kongo na Burundi. 

Alisema kuwa, pamoja na kwamba wawekezaji hao wanalazimika kuuza asilimia kubwa ya chumvi yao nje ya nchi kutokana na sababu za kijiografia na miundombinu ya usafirishaji; Serikali inaona suala hilo siyo sawa, hivyo inaweka mikakati kuhakikisha wazalishaji hao na wengine wote wanatosheleza Soko la Ndani ya nchi kwanza; ambalo ni kubwa, kabla ya kuuza nje. 

“Mahitaji ya Chumvi kwa Tanzania ni takribani tani 250,000 kwa Mwaka na takwimu zilizopo zinaonesha tunaagiza kiasi kikubwa cha Chumvi kutoka nje ya nchi, hususan Kenya, wakati hii ya kwetu tunayozalisha nchini, tunaiuza nje. Hii siyo sawa. Ni lazima sasa tuweke mikakati itakayowezesha wawekezaji wetu kutosheleza Soko la Ndani kwanza,” alisisitiza. 

Kuhusu mikakati ambayo Serikali inaifanya katika kuboresha sekta hiyo ndogo ya chumvi; Naibu Waziri alisema kuwa, ni pamoja na kuwawezesha wachimbaji wadogowadogo, waweze kuzalisha chumvi nyingi itakayotosheleza Soko la Ndani na la Nje. 

“Mathalani, tumedhamiria kufungua Vituo vya Mfano (Centre of Excellence) sehemu mbalimbali nchini. Tumekwishaanza na Lindi, tutafanya hivyo kwa Mikoa mingine ikiwemo huu wa Kigoma ili wachimbaji wajifunze namna ya uzalishaji bora wa chumvi ikiwemo kuiongezea madini joto, ambao ni mkakati wa kidunia pamoja na kuifungasha katika hali ya ubora iweze kukidhi viwango vya Soko la Ndani na hata vya ushindani katika Soko la Nje.” 

Aidha, Naibu Waziri alisema kuwa, ili kuwawezesha zaidi wawekezaji katika sekta husika; Serikali kupitia Wizara ya Madini pamoja na Idara nyingine zinazohusika, watakaa pamoja wajadili namna wanavyoweza kupunguza wingi wa kodi zinazotajwa kufikia 14 na kulalamikiwa na wawekezaji, ili waweze kufanya biashara hiyo kwa tija zaidi. 

Alisema kuwa, ni suala linaloleta ‘ukakasi’ kuona wingi wa kodi inayotozwa kwa wazalishaji wa chumvi wa ndani ya nchi na wakati huohuo nchi inaagiza chumvi kutoka nje pasipo kodi yoyote, hivyo akasisitiza kuwa Serikali imeona kuna umuhimu mkubwa kwa wadau kukutana, kujadili na kuweka mikakati itakayoleta suluhisho lenye tija. 

Awali, akiwasilisha Taarifa ya Mgodi wa Uvunaji Chumvi wa Nyanza kwa Naibu Waziri, Meneja wa Mgodi Bonny Mwaipopo, alisema kuwa jumla ya kodi iliyolipwa kwa Serikali kwa kipindi cha Mwaka 1999 hadi 2016 ni shilingi bilioni 8.8 za kitanzania. 

Wizara ya Madini imekuwa ikieleza dhamira yake ya kuhakikisha uchangiaji wa sekta hiyo katika Pato la Taifa unakua zaidi ya ilivyo sasa, kupitia usimamizi mzuri utakaowezesha ongezeko la wawekezaji wenye kulipa kodi na tozo zote stahiki za Serikali.
Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo na Ujumbe wake, akikagua maeneo mbalimbali ya Mgodi wa Chumvi wa Nyanza ulioko Uvinza (Nyanza Salt Mines), wakati wa ziara yake ya kazi mkoani Kigoma, Machi 3 Mwaka huu.
Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo na Ujumbe wake, akikagua maeneo mbalimbali ya Mgodi wa Chumvi wa Nyanza ulioko Uvinza (Nyanza Salt Mines), wakati wa ziara yake ya kazi mkoani Kigoma, Machi 3 Mwaka huu. 
Mmoja wa wafanyakazi katika Mgodi wa Chumvi wa Nyanza, ulioko Uvinza (Nyanza Salt Mines), akifunga Mifuko ya Chumvi tayari kupelekwa Sokoni kwa ajili ya kuuzwa. Picha hii ilipigwa wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo (hayupo pichani), Mgodini hapo, Machi 3 Mwaka huu.
Shughuli za uchakataji chumvi zikiendelea katika Mgodi wa Chumvi wa Nyanza ulioko Uvinza (Nyanza Salt Mine), siku Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo (hayupo pichani), alipotembelea Mgodi huo akiwa katika ziara ya kazi, Machi 3 Mwaka huu.

No comments: