Thursday, February 8, 2018

WIZARA YA MALIASILI, ARDHI NA TAMISEMI KUAMUA HATMA YA MGOGORO WA PORI LA AKIBA MKUNGUNERO – DK. KIGWANGALLA



Na Hamza Temba - Kondoa, Dodoma
.....................................................
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla jana tarehe 7 februari, 2018 ametembelea Pori la Akiba Mkungunero katika Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma na kuwataka wananchi wanaozunguka pori hilo kusubiri uamuzi wa Serikali  utakaoshirikisha Wizara yake,  Wizara ya Ardhi na Tamisemi katika kujibu maombi yao ya kutaka kupewa sehemu ya ardhi katika pori hilo kwa ajili ya kuendesha shughuli za kibinadamu.

Dk. Kigwangalla ambaye aliongozana na Mbunge wa Jimbo la Kondoa Vijijini ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Ashatu Kijaji na Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya hiyo, alitembelea vijiji vinne vya Ikengwa, Keikei Tangini, Keikei na Kisondoko na kufanya mikutano ya hadhara kwa ajili ya kujiridhisha na  kujifunza juu ya mgogoro uliopo baina ya vijiji hivyo na Pori la Akiba Mkungunero.

"Nimefika hapa leo kujifunza juu ya mgogoro huu, nimejionea hali halisi lakini pia nina maelezo ya wataalamu ambayo yapo kwenye maandishi naomba niende nikayasome, niyatafakari ili niweze kushauriana na wenzangu na mwisho wa siku tuweze kuja na suluhu ya namna ya kuondokana na changamoto ambazo zimekuwepo.

"Niwaombe sana wakati Serikali inaendelea kutafuta suluhu ya mgogoro huu ni vema tukafuata sheria zilizopo, tuzingatie mipaka iliyowekwa ili tusiingie kwenye migogoro, lakini kwa sasa siwezi kwa namna yeyote ile kutamka neno la kujibu maombi ya mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji na wananchi yaliyotolewa hapa leo.

"Kama Serikali tutakaa, Wizara yangu, Wizara ya Ardhi na Tamisemi ili tujue kiini cha mgogoro huu tufanye uamuzi kuwa ni maeneo gani yaongezwe katika hifadhi kwa ajili ya wananchi au ni vitongoji vipi vifutwe, tutaleta majibu, na jambo hili tutalifanya kwa uadilifu mkubwa bila kumuonea mtu ili kumaliza mgogoro huu," alisisitiza Dk. Kigwangalla.

Awali akimkaribisha Waziri huyo kuzungumza na wananchi wa kijiji cha Ikengwa, Mbunge wa jimbo hilo, Dk. Ashatu Kijaji alisema kutokana na ukweli kuwa Serikali ya awamu ya tano inasikiliza kero za wananchi na kuzipatia ufumbuzi, ni vema Waziri huyo akatumia hekima na kuangalia uwezekano wa kuwapa wananchi hao Kilomita 12 za mraba kutoka kwenye hifadhi hiyo kwa ajili ya kuendesha shughuli zao za kibinadamu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kijiji cha Ikengwa, Mohammed Tabahi alisema mgogoro baina ya vijiji hivyo na Pori la Akiba Mkungunero ulinza mwaka 2006 kufuatia zoezi la kuanzishwa kwake  pamoja na lile na uwekagi wa vigingi vya mpaka  na vijiji jirani kutoshirikisha wananchi na viongozi wa halmashauri za vijiji hoja ambayo ilipigwa na Meneja wa Pori hilo, Emannuel Bilaso

Aidha alisema wananchi wa vijiji hivyo wanakabiliwa na uhaba wa maeneo ya kilimo na ufugaji, hivyo akamuomba Waziri huyo pamoja na Serikali kwa ujumla kutumia busara  kuwamegea wananchi wa vijiji hivyo eneo la Kilomita 12 za mraba kwa ajili ya shughuli za kilimo na ufugaji.

Naye Meneja wa Pori hilo, Emannuel Bilaso alisema Pori la Akiba Mkungunero lilianzishwa kwa tangazo la Serikali Na. 307 la mwaka 1996 baada ya kupandishwa hadhi kutoka Pori Tengefu. Alisema mchakato wa kupandisha hadhi pori hilo ulishirikisha wananchi na viongozi wa vijiji na wilaya ambapo mihutasari mbalimbali ilisainiwa.

Alisema pori hilo linakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazochochea mgororo huo ikiwemo kijiji kimoja cha Kisondoko  kusajiliwa kimakosa ndani ya hifadhi hiyo pamoja na malalamiko mbalimbali ya wananchi kuwa hawakushirikishwa kwenye uanzishwaji wa pori pamoja na madai mengine kuwa pori hilo limeingilia mipaka ya vijiji hivyo.

Pori la Akiba Mkungunero ambalo lina ukubwa wa Kilimita za Mraba 557.9 lina umuhimu mkubwa kiuchumi na kiikolojia kwa kuwa ni chanzo muhimu cha mto Tarangire ambao ni uhai wa hifadhi ya Taifa ya Tarangire na ikolojia nzima ya ziwa Manyara. Pori hilo pia ni sehemu ya mapito na mazalia ya wanyamapori pamoja na makazi ya wanyamapori adimu duniani.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (kushoto) akimsikiliza Mwenyekiti wa Kijiji cha Ikengwa, Mohammed Tabahi aliyekuwa akimunesha mpaka wa kijiji hicho na Pori la Akiba Mkungunero wakati wa ziara yake ya kikazi katika pori hilo jana Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma kwa ajili ya kubaini changamoto za mgogoro wa mipaka kati ya pori hilo na vijiji jirani ili kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu ambapo alisema Wizara yake kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi na TAMISEMI zitakaa pamoja kutafuta suluhu ya mgogoro huo. Kulia ni Mbunge wa Jimbo la Kondoa Vijijini ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Ashatu Kijaji.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akisalimiana na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Kondoa muda mfupi baada ya kuwasili wilayana humo jana.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akioneshwa ramani ya Pori la Akiba Mkungunero na Mrasimu Ramani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa, Peter Nyange (kulia) wakati wa ziara yake ya kikazi katika pori hilo jana Wilayani Kondoa Mkoa wa Dodoma kwa ajili ya kubaini changamoto za mgogoro wa mipaka kati ya pori hilo na vijiji jirani ili kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu ambapo alisema Wizara yake kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi na TAMISEMI zitakaa pamoja kutafuta suluhu ya mgogoro huo. Kulia ni Mbunge wa Jimbo la Kondoa Vijijini ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Ashatu Kijaji.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akioneshwa mipaka ya Pori la Akiba Mkungunero na Mrasimu Ramani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa, Peter Nyange (kulia) wakati wa ziara yake ya kikazi katika pori hilo jana Wilayani Kondoa Mkoa wa Dodoma kwa ajili ya kubaini changamoto za mgogoro wa mipaka kati ya pori hilo na vijiji jirani ili kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu ambapo alisema Wizara yake kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi na TAMISEMI zitakaa pamoja kutafuta suluhu ya mgogoro huo. Kulia ni Mbunge wa Jimbo la Kondoa Vijijini ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Ashatu Kijaji. 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (wa tatu kulia) akiteja jambo na Meneja wa Pori la Akiba Mkungunero, Emannuel Bilaso wakati wa ziara yake ya kikazi katika pori hilo jana Wilayani Kondoa Mkoa wa Dodoma. 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla (wa pili kulia) akiteta jambo na Mwenyekiti wa Kijiji cha Ikengwa, Mohammed Tabahi wakati wa ziara yake ya kikazi jana katika Pori la Akiba Mkungunero Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma kwa ajili ya kubaini changamoto za mgogoro wa mipaka kati ya pori hilo na vijiji jirani ili kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu ambapo alisema Wizara yake kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi na TAMISEMI zitakaa pamoja kutafuta suluhu ya mgogoro huo. 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akipokea mabango ya malalamiko kutoka kwa wananchi wa kijiji cha Kisondoko kuhusu Pori la Akiba Mkungunero na vijiji jirani wakati wa ziara yake ya kikazi katika pori hilo jana Wilayani Kondoa Mkoa wa Dodoma. 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akizungumza na wananchi wa kijiji cha Kisondoko wilayani Kondoa jana.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akioneshwa mipaka ya Pori la Akiba Mkungunero na mmoja wa wahifadhi wa Pori hilo wakati wa ziara yake ya kikazi katika pori hilo jana Wilayani Kondoa Mkoa wa Dodoma kwa ajili ya kubaini changamoto za mgogoro wa mipaka kati ya pori hilo na vijiji jirani ili kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu ambapo alisema Wizara yake kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi na TAMISEMI zitakaa pamoja kutafuta suluhu ya mgogoro huo. Kulia ni Mbunge wa Jimbo la Kondoa Vijijini ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Ashatu Kijaji.

No comments: