Sunday, February 25, 2018

SERIKALI YA AWAMU YA TANO HAIKO TAYARI KUONA MWANANCHI ANAONEWA, ANANYANYASWA'

Naibu waziri wa madini Stanlaus Nyongo Akizungumza na Wakazi Wa Kijiji Cha Nyakabale wakati wa ziara yake Mkoani Geita. 
Naibu waziri wa madini Stanlaus Nyongo akishiriki zoezi la kupanda mawe ya dhahabu. 
Naibu waziri wa madini Stanlaus Nyongo akizungumza na diwani wa kata ya Mgusu Patory Ruhusa. 
Naibu Waziri Akimsikiliza Pili Mwaluko Anaefanya Kazi Ya Uchenjuaji Madini kwenye mtaa wa Nyakabale. 
Wananchi wakiwa kwenye Mkutano wa pamoja na Naibu Waziri wa madini Stanlaus Nyongo.


Na,Joel Maduka,Geita. 


NAIBU Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo amesema Serikali ya Awamu ya Tano haiko tayari kuona mtu akilalamika ,kunyanyaswa au kunyimwa haki yake.

Ametoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Nyakabale, Kata ya Mgusu wilayani Geita wakati wa ziara yake ya siku mbili mkoani humo ya kuzungukia maeneo ya uchimbaji na kusikiliza kero za wananchi walizunguka kwenye baadhi ya maeneo ya mgodi wa Geita(GGM).

Hatua hiyo ya Naibu Waziri Nyongo imekuja baada ya kusikia malalamiko mengi kutoka kwa wananchi kuhusu mgodi wa GGM kushindwa kuwalipa fidia kwa muda mrefu licha ya kuwepo kwa maagizo mengi  yaliyotolewa na  baadhi ya viongozi ambao wamekuwa wakifika mkoani humo.

 Amesema mtu mwingine yuko tayari kuona Mtanzania mwenzake akikandamizwa ilimradi yeye aendelee kulinda maslahi yake binafsi, na kwamba miaka hiyo imeshapita na muda uliopo kwa sasa ni kufanya kazi za kuwatumikia wananchi ambao ni wanyonge.

“Tukikaa kwenye viyoyozi hatuambiwi ukweli na wamiliki wa migodi lakini tunapo fika katika eneo husika tunapata ukweli , unakuta mtu kazaliwa hapo, kakulia hapo amejenga ana watoto.Halafu mtu anakuondoa kwa madai kuwa upo kwenye leseni yake ,hiyo haingii akilini na kama unahitaji eneo langu njoo tukae tumalizane unipe changu mimi nisepe inakuwa nilipe nisepe,”amesema Nyongo.

Amewataka watu wa mgodi huo kuwalipa wananchi hao ama waondoke wawaachie wananchi hao eneo lao waendelee kuchimba na si kuwazuia ikiwa hawafanyi shughuli za uchimbaji kwa sasa.

Ameongeza  au wawaache waendelee kufanya shughuli za bila kubuguziwa, mgodi ulikuja kama neema za Mungu, hivyo isiwe mgodi huu kazi yake kuwanyanyasa wananchi.

Awali akitoa malalamiko kwa Naibu Waziri, Mwananchi wa Nyakabale kwa niaba ya wenzake Joseph Kihengu amemwambua Naibu Waziri kuwa wanailaumu serikali iliyopita.

Amefafanua inawezekana wakati wanabinafsisha mgodi huu na wao walbinafisishwa humo bila kujua.

“Mheshimiwa kipindi cha nyuma usingeweza kupata umati kama huu, umati huu umetokana na imani ya Serikali ya awamu ya tano waliyo nayo,hivyo iwaangalie kwa jicho la tatu ili watu Wanyakabele wajue hatima ya maeneo ambayo yapo ndani ya bikoni mgodi wa GGM”Amesema Joseph.

Katika hatua nyingine akina mama wa Nyakabale wakiwakilishwa na Godliva Mgini waliutupia lawama mgodi huo wa GGM kwa kuwafilisi kwa kukilaghai kikundi chao cha Baraka baada ya kuwaahidi kuwawezesha kuanzisha mradi ufungaji wa nguruwe 100.

Ambapo amedai waliambiwa wasombe mawe ili wajenge na kujikuta wakighalamia kiasi cha Sh.800,000, baadae wakatokomea kusiko julikana na kuwaacha maskini zaidi.

Nae Makamu wa Rais GGM, Saimon Shayo amesema “Tunatambua majirani hivyo niseme tu baadhi ya maneno yaliyoelezwa hapa mengine yanafahamika na  mengine ni mageni ndo tunayasikia na mangine tunahitaji kama mgodi kukaa na kuyapatia ufumbuzi”.

Aidha amesema kuna baadhi ya watu wa Nyakabale vigingi vyao vipo ndani ya mgodi na kimsingi jambo hilo lipo wazi pia kuna watu wana haki ya ardhi kisheria suala na kwamba suala hilo ni namna ya kukaa pamoja na kujadili kwasasa.

No comments: