Wednesday, January 31, 2018

NAMNA MAHABUSU,WAFUNGWA WANAVYOTUMIA SEHEMU ZA SIRI KUINGIA NA SIMU, SIGARA GEREZANI

Na Karama Kenyunko, blogu ya jamii 

WAMETAFUTA mbinu mbadala! Ndivyo unavyoweza kuelezea kinachoendelea kwenye baadhi ya magereza yaliyopo nchini kwa baadhi ya wafungwa na mahabusu kutumia sehemu zao za siri kwa ajili ya kuingia na simu za mkononi pamoja na sigara.

Sheria za magereza kuna baadhi ya vitu vimepigwa marufuku ikiwamo simu ya mkononi, dawa za kulevya, visu ,nondo na sigara lakini baadhi ya mahabusu na wafungwa wamekuwa wakiingia nazo kwa kutumia mbinu mbalimbali.

Kwa mujibu wa Mrakibu Msaidizi wa Magereza, makao makuu kitengo cha sheria Absalom Mokily ameiamba Michuzi Blog kwenye mahojiano maalumu yaliyofanyika leo alipokuwa kwenye maonesho ya Wiki ya Sheria inayoendelea jijini Dar es Salaam kuwa kuna mbinu nyingi wanazozitumia mahabusu na wafungwa kuingia na vitu hivyo.

SEHEMU ZA SIRI ZINATUMIKAJE? IKO HIVI .

Akielezea zaidi kuhusu baadhi ya wafungwa na mahabusu kutumia sehemu zao za siri kuingia na vitu ambavyo vimepigwa marufuku , Mokiry amesema wenye tabia hiyo wamekuwa wakijaza mizigo kupitia njia  za haja kubwa na njia ya mkojo.

Amesema kuwa wanaoingia na vitu hivyo hata askari Magereza wanashindwa kubaini kutokana na utaalamu wanautumia kificha vitu hivyo vilivyopigwa marufuku kuingizwa magerezani.

"Unaweza kuwapekua na usione chochote, hivyo unapomruhusu aondoke, anachokifanya anakwenda chooni na kisha kutoa vitu alivyoficha kwenye  sehemu zake za siri,"ameeleza.

Mokily amesema kwa mujibu wa kanuni za kudumu za Magereza namba 149 ya mwaka 2003 imezuia baadhi ya vitu kuingizwa magerezani.Ametaja baadhi ya vitu hivyo ni ni silaha, simu, visu, nondo, bangi, tumbaku na simu za mkononi."Ni marufuku kuingia na vitu,"amesema.

Amesema kuwa tabia hiyo si tu kwa baadhi ya wafungwa na mahabusu wa kiume tu bali hata wanawake nao wanatabia hiyo kwa kuchukua vitu hivyo na kuficha sehemu zao za siri.

"Wanawake wenye tabia ya kuficha vitu wanachokifanya ni kukimbilia chooni na kisha huvitoa na baada ya hapo utashangaa kuona wanawasiliana na watu walioko nje kwa kutumia simu ambazo wameingia nazo kwa mtindo huo,"amesema.

Amefafanua kuna watu magerezani wamekuwa wakiingia na kutoka , wengine wazoefu magerezani hasa mahabusu.Wanapokwenda mahakamani inakuwa ndio njia ya wao kupata vitu hivyo na kisha kuingia navyo magarezani.

WASHINDWA KUTHAMINI UTU WAO

Wakati huohuo, Mokiry anasema mfungwa anachukuliwa kama binadamu na kubwa zaidi askari magereza wanathamini sana utu wa watu wote lakini baadhi ya wafungwa na mahabusu wameshindwa kuthamini utu wao hasa wakiwa magerezani.

"Unapawakagua huoni chochote lakini ukienda chooni utagundua wameingia na pakiti za sigara na simu na vitu vingine ambavyo haviruhusiwi.Tunashindwa kuwapekua sana kwani unaweza kuambiwa unadhalilisha utu wa mtu lakini wenyewe wamekuwa wakwanza kutothamini utu wao,"amesema.

HATUA ZINAZOCHUKULIWA

Mokiry ameongeza mahabusu au mfungwa atakayekamatwa akiwa na vitu hivyo huchukuliwa hatua za kisheria ikiwamo ya kupelekewa mahakamani na ikitokea kuna mtumishi asiye mwaminifu na anayekiuka kanuni huchukuliwa hatua na ikiwezekana anafukuzwa kazi ikibainika ni kweli amehusika kusaidia kuinga kwa vitu hivyo.

MIMBA GEREZANI

Kwa upande wa Mrakibu wa Magereza, Amina Kavirondo  alipoulizwa kuhusu baadhi ya wafungwa na mahabusu kupata mimba wakiwa magerezani, amejibu haijawahi kutokea mwanamke akapata ujauzito akiwa gerezani.

"Kinachotokea wapo baadhi ya mahabusu na wafungwa wanaoingia wakiwa na mimba gerezani na hivyo hujifungulia huko huko na kupata watoto,"amesema.

Amefafanua wafungwa na mahabusu wanawake wanaipongia gerezani wanapimwa afya ili kubaini hali zao na kama mjamzito ripoti hupelekwa Makao Makuu ya Magereza na usimamizi wake kuanzia mwanzo hadi mwisho.

"Mfungwa wa kike akibainia ni mjamzito humpokea na kumtunza  ili kuhakikisha anakuwa salama yeye na kiumbe kilicho tumboni mpaka pale atakapojifungua salama,"amesema Kavirondo.
Mrakibu wa Magereza Kitengo cha Sheria, Absalom Mokiry akifafanua mambo mbali mbali juu ya wafungwa na mahabusu waliopo mahakamani ikiwemo kuingiza simu na vitu vilivyokatazwa gerezani kwa kutumia njia zisizostahili.

No comments: