Saturday, December 16, 2017

UKARABATI WA SHULE KONGWE WAWAKUNA WANAFUNZI

Zoezi la ukarabati wa shule kongwe 89 hapa nchini limeonyesha kupandisha hamasa ya wanafunzi kimasomo kutokana na kubadilika kwa mazingira ya kujifunzia kuwa bora zaidi ikilinganisha hali ya awali kabla ya ukarabati huo ulipokuwa haujaanza.

Hali hiyo imebainika wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tamisemi Selemani Jafo alipotembelea shule ya wavulana Bwiru pamoja na shule ya Ngaza zilizopo mkoani mwanza. 

Katika ziara hiyo ,Jafo amepata nafasi ya kuongea na wanafunzi wa Ngaza ambao walimhakikishia Waziri Jafo kwamba watafanya vizuri zaidi katika mitihani yao kwani kwasasa wamepata amani kubwa na hamasa tele.

Ukarabati wa shule hizo umehusisha ukarabati wa madarasa, mabweni, vyoo, bwalo za chakula, maktaba, maabara, pamoja na mifumo ya maji na umeme.Katika hatua nyingine,Waziri Jafo amepongeza jiji la Mwanza kwa kuanza ujenzi wa jengo la ghorofa kwa ajili ya wodi ya wanaume katika hospitali ya wilaya ya Ngamagana.

Ujenzi wa jengo hilo umeanza kwa kutumia mapato ya ndani ya jiji hilo na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Julai 2018.Jengo hilo linajengwa na mkandarasi Mzinga Company ambapo mpaka sasa ujenzi huo unaenda vizuri.

Katika mradi huo, Jafo amezitaka Halmashauri zingine kuiga mfano huo ili kupunguza changamoto za miundombinu katika hospitali za wilaya.
Jengo la shule ya wavulana Bwiru baada ya kufanyiwa ukarabati.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tamisemi Selemani Jafo akikagua ukarabati wa shule ya sekondari Ngaza mkoani Mwanza.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tamisemi Selemani Jafo akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa mkoa wa Mwanza na walimu wa shule ya Ngaza.
Wanafunzi wa shule ya Ngaza wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tamisemi Selemani Jafo.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tamisemi Selemani Jafo akipata maelezo ya ujenzi wa jengo jipya katika hospitali ya wilaya ya Nyamagana.
Mafundi wakijenga jengo la Hospitali ya wilaya ya Nyamagana.

No comments: