Friday, November 10, 2017

WAZAZI WAASWA KUWASOMESHA WATOTO WA KIKE

NA DENIS MLOWE, IRINGA

WAZAZI na Walezi wameaswa kuwasomesha watoto wa kike na kuachana na fikra potofu kuwa kumsomesha mtoto wa kike ni kupoteza rasilimali fedha kwani maisha ya sasa bila elimu ni changamoto kubwa kwa mtoto wa kike.

Kauli hiyo imetolewa hivi karibuni na Kenneth Komba kutoka Idara ya Elimu mkoa wa Iringa kwa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Iringa Amina Masenza wakati alipokuwa mgeni rasmi wakati wa mahafali ya kumi kidato cha nne katika shule ya Sekondari ya Wasichana ya Spring Valley iliyopo Mkoani Iringa.

Alisema kuwa mtoto wa kike akipatiwa elimu kuna uwezekano mkubwa kwa taifa kuwa na maendeleo kutokana na kuwajibika kwao katika maisha ya kila siku hivyo wazazi na walezi ni muhimu kuwasomesha watoto wa kike kwa lengo la kuendeleza ndoto walizonazo.

Alisema kuwa jukumu la kusomesha elimu ya msingi hadi sekondari ni la serikali lakini wazazi na walezi wanaosomesha shuleni hapo ni kuisaidia serikali hivyo ipo tayari kupokea changomoto zote katika shule hiyo na kushirikiana kuzitatua.

Komba aliipongeza shule ya sekondari Spring Valley kwa kuwa moja ya shule zinazofanya vizuri mkoani hapa kielimu na tabia kwani ni moja ya shule ambazo idara ya elimu haipati malalamiko ya mara kwa mara kutoka shuleni hapo.

Aidha Komba aliwataka wahitimu hao kusoma mazingira ya maisha popote watakapokuwa na kuamua namna ya kujiajiri ili mradi isiwe shughuli zinazopingana na sheria na maadili ya kijamii, kama vile kuuza madawa ya kulevya, ukahaba, unyang'anyi na mambo mengine yanayofanana na hayo ambayo watajiingiza matatani na kuonekana wabaya.

Awali mkuu wa shule ya Wasichana Spring Valley, Adia Mbwanji alisema kuwa uongozi wa shule hiyo umeweka mikakati mbalimbali itakayotekelezwa mwaka 2018 ikiwemo ujenzi wa ukuta upande wa Kusini mwa shule, upanuzi wa maktaba, ununuzi wa gari la shule na kukarabati mifumo ya maji taka na maji safi.

Alisema kuwa shule hiyo inayomilikiwa na kanisa la Baptist Convention of Tanzania imejipanga kujenga chumba cha kompyuta na kununua komputa zenyewe ili kutoa elimu hiyo kwa wanafunzi kuendana na ulimwengu wa sayansi na teknolojia.

Kwa upande wao wahitimu kwa kupitia msoma risala, Happy Njavike walisema kuwa shule hiyo inatakiwa kuboresha ujenzi wa jengo la maabara vifaa vyake vinunuliwe ili kutoa fursa kwa wanafunzi wengi kujifunza kwa vitendo hasa masomo ya sayansi kwa lengo la kukuza ufaulu na kuongeza ujuzi katika masomo ya sayansi.

 Wanafunzi wa shule ya wasichana ya Spring valley wakicheza muziki katika sherehe za kumaliza kidato cha nne
 wanafunzi wa shule ya sekondari ya wasichana ya Springa Valley wakiwa katika picha ya pamoja
Baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari ya wasichana ya Spring Valley iliyoko katika manispaa ya Iringa wakiwa katika mafunzo ya vitendo shuleni hapo

No comments: