Wednesday, November 15, 2017

MASHINDANO YA KUMUENZI MTAKATIFU GASPARI ITIGI

Ni baadhi ya washiriki wa mchezo wa kuvuta kamba kwenye mashindano ya maadhimisho ya kumuenzi Mtakatifu Gaspari,Itigi,wilayani Manyoni.(Picha Na Jumbe Ismailly)

MASHINDANO ya michezo ya maadhimisho ya siku kuu ya kumbukumbu ya kumuenzi Mtakatifu Gaspari Del Buffalo yaliyokuwa yakifanyika katika viwanja vya michezo vya kanisa, hatimaye yamefikia tamati,ambapo timu ya Wafanyakazi wa Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Gaspari na chuo cha uuguzi iliyopo katika Mji mdogo wa Itigi,wilayani Manyoni imatawazwa kuwa mabingwa wa mpira wa miguu wa mashindano hayo mwaka huu.

Katika mashindano hayo yalizishirikisha jumla ya timu nane za wanaume za mpira wa miguu na mpira wa pete huku kukiwa na malalamiko yaliyotolewa na baadhi ya viongozi na wachezaji wa timu zilizoshiriki katika mashindano hayo.

Mmoja wa viongozi wa timu ya mpira wa pete kwa wanawake,Hayfat Hassani aliwashauri waandaaji wa mashindano hayo kwamba kwa kuwa timu nyingi zilizoshiriki hazikuwa na jezi,hivyo aliwataka kuangalia uwezekano wa kuzipatia jezi timu zitakazoshiriki katka mashindano ya mwaka ujao.

Aidha akizungumzia kuondokana na malalamiko ya upendeleo unaofanywa na waamuzi,Hayfat alishauri pia kwamba katika mashindano kama hayo kwa mwaka ujao ni vyema waamuzzi wa michezo hiyo wakatafutwa kutoka nje ya maeneo ya Halmashauri ya Itigi.

“Kwa sababu kulikuwa na malalamiko kutoka kwa baadhi ya wachezaji kuhusu kocha wa timu yetu ambaye naye alikuwa akichezesha kwenye mashindano hayo kuwa alikuwa hazitendei haki timu zingine pinzani na timu yake wakati zilipokuwa zikichuana huku yeye akiwa mwamuzzi wa mchezo huo”alifafanua Hayfat. 

Kwa upande wake kocha msaidizi wa timu ya wafanyakazi wa Hospitali na chuo ha uuguzi cha Mtakatifu Gaspari,Gabrieli Mathayo alipendekeza kuwepo sheria kali zitakazowabana viongozi pamoja na timu zao wenye tabia ya kupanga matokeo ya michezo wanayoshiriki.

Katika risala ya Watumishi wa Hospitali ya rufaa ya Mtakatifu Gaspari na Chuo cha Uuguzi iliyosomwa na Mwalimu Epafradito Frank ilieleza kwamba maadhimisho hayo hutanguliwa na michezo mbali mbali ambapo kipekee mwaka huu yamefanyika michezo ya mpira wa miguu,mpira wa pete,mchezo wa bao,mbio za baiskeli,mbio za maagunia,kuvuta kamba,kukimbia na yai kwenye kijiko na kufukuza kuku.

Naye Mratibu wa maadhimisho hayo mwaka huu,Dk.Peter Nyira aliitaja baadhi ya michezo iliyofanyika kuwa ni pamoja na mpira wa miguu na mpira wa pete ambapo jumla ya timu nane za wanaume zilishiriki mpira wa miguu huku Mkuu wa shirika la wamisionari wa damu Azizi ya Yesu kanda ya Tanzania,Fr,Chesco Msaga akiupongeza uongozi wa Hospitali hiyo kwa kujali sekta ya michezo.

No comments: