Monday, November 20, 2017

KABURI LAFUKULIWA MOSHI KUONDOA UTATA WA MWILI WA MTU ALIYEZIKWA BAADA YA KUOKOTWA MTONI

Na Dixon Busagaga wa Globu 
ya Jamii Kanda ya Kaskazini.
 UTATA umeighubika familia ya Jackson Makundi ambayo kijana wake aliyetambulika kwa jina la Humphrey Makundi,Mwanafunzi wa shule ya Sekondari ya Scolastica iliyopo mji mdogo wa Himo kupotea katika mazingira tatanishi.
 Utata wa kupotea kwa mwanafunzi huyo unatiliwa shaka zaidi na familia hiyo baada ya kufukuliwa kwa kaburi ulimozikwa mwili uliookotwa mto Ghona mita 300 ,jirani na shule hiyo ukidaiwa kushabihiana na wa mwanafunzi huyo.
  Humphrey Makundi, mwanafunzi wa kidato cha pili katika shule ya sekondari ya Scolastica anatajwa kupotea tangu Novemba 7 mwaka huu akiwa shuleni hapo huku wanafunzi wenzake wakiendelea na mitihani ya kidato cha Pili ya upimaji ya kitaifa .

 Familia ya kijana huyo yenye makazi yake mkoani Dodoma ikalazimika kutumia mitandao ya kijamii kutoa taarifa za kupotea kwake ikidai mazingira ya kutoweka kwake ni ya kutatanisha na baadae kuwasilisha taarifa katika kituo cha Polisi cha Himo .

Kutokana na kuwepo kwa taarifa za kuokotwa kwa mwili huo ,familia iliwasilisha maombi katika mahakama ya Hakimu Mkazi, Moshi na mahakama ikaamuru kufukuliwa kwa Kaburi hilo zoezi lililoanza majira ya saa 8:30 mchana na kudumu kwa zaidi ya saa moja.
Jeshi la Polisi liliongoza zoezi hilo katika makaburi ya Karanga huku likishuhudiwa na ndugu wa mtoto aliyepotea ambapo baada ya mwili kutolewa kaburini hali ya simanzi ilionekana katika nyuso za baadhi ya ndugu wa Mwanafunzi huyo akiwemo baba mzazi wa kijana huyo.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro,Kamishna Msaidizi wa Polisi ,Hamis Issa akathibitisha uwepo wa tukio hilo huku akieleza kuwa tayari jeshi la Polisi linawashikilia wati 11 akiwemo mmiliki wa shule hiyo Edward Shayo huku likifanya uchunguzi wa kina kuhusu matukio hayo mawili.
Mwili uliofukuliwa katika makaburi ya Karanga upande wa marehemu wasiokuwa na ndugu ulipelekewa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya KCMC kwa uchunguzi zaidi chini ya uangalizi wa jeshi la Polisi wakishirikiana na madaktari kutoka  KCMC.
Jeshi la Polisi likiwa limezungushia utepe eneo ambalo kuna kaburi ulimozikwa mwili ambao familia ya Mwanafunzi wa shule ya sekondari ya Scolastica iliyopo mji mdogo wa Himo aliyepotea ,Humphrey Makundi ulitilia shaka.
Kaburi ulimozikwa mwili wa mtu aliyezikwa na Manispaa ya Moshi baada ya kuokotwa Mto Ghona jirani na ilipo shule ya Sekondari .
Askari Polisi wakishirikiana na ndugu wa Mwanafunzi aliyepotea Humphrey Makundi wakifukua Kaburi ulimozikwa mwili wa mtu aliyeokotwa Mto Ghona katika wilaya ya Moshi.
Kaburi likifukuliwa.
Baba mzazi wa Mwanafunzi wa shule ya Sekondari ya Scolastica aliyepotea,Jackson Makundi (Katkati) akijadili jambo na wanandugu wakati zoezi la kufukua kaburi likiendelea.
Baba mzazi wa Mwanafunzi Humphrey ,Jackson Makundi (Mwenye suti nyeupe) akitizama mwili (haupo pichani) baada ya kaburi kufukuliwa.
Baba mzazi wa Mwanafunzi Humphrey ,Jackson Makundi (Mwenye suti nyeupe) akionekana akiwa amekaa chini baada ya kutizama mwili uliofukuliwa katika kaburi .
Askari Polisi na Wanandugu wa kijana aliyepotea wakijaribu kusaidia kumnyanyua mzazi wa Mwanafunzi huyo kutoka katika eneo lilipo kaburi lililofukuliwa .
Baba mzazi wa Mwanafunzi Humphrey ,Jackson Makundi (Mwenye suti nyeupe) akisindikizwa kutoka katika eneo la Makaburi ya Karanga katika manispaa ya Moshi.
Mwili uliofukuliwa katika makaburi hayo ukiwekwa katika gari la Polisi kwa ajili ya kwenda kuhifadhiwa katika Hosptali ya Rufaa ya KCMC.
Gari la Polisi likiwa na mwili uliofukuliwa katika Makaburi ya Karanga.

No comments: