Wednesday, November 29, 2017

DAWA ZA SARATANI ZAPATIKANA KWA ASILIMIA 80 % KUTOKA ASILIMIA 4%

Na Dotto Mwaibale
TAASISI ya Saratani ya Ocean Road wameipongeza Bohari ya Dawa (MSD), kwa usambazaji wa dawa katika taasisi hiyo na maeneo mengine nchini.
Pongezi hizo zimetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani ya Ocean Road Dk. Julius Mwaiselage wakati akizungumza na watendaji wa MSD ambao walifanya ziara ya kikazi ya kujua changamoto mbalimbali za usambazaji dawa katika taasisi hiyo wakiongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Laurean Bwanakunu.
Katika hatua nyingine  upatikanaji wa dawa za saratani,vifaa tiba na vitendanishi  vya maabara katika taasisi hiyo ni asilimia 80  kutoka asilimia nne mwaka 2015.
Kutokana na hatua hiyo taasisi hiyo imesema ipo haja jamii kutambua mchango mkubwa unaotolewa na Bohari ya Dawa MSD katika kupunguza changamoto za huduma za saratani ambapo ilikuwa kero miaka miwili iliyopita.
 Mwaiselage alisema hapo awali  upatikanaji wa dawa vifaa tiba na vitendanishi ilikuwa ni changamoto kubwa katika utendaji.
"2015 taasisi hiyo ilikuwa ikipata dawa,vifaa tiba na vitendanishi asilimia nne sasa ni asilimia 80 haya ni matokeo mazuri ya utendaji wa kazi wa MSD," alisema.
Alisema bajeti ya taasisi hiyo mwaka 2015 ilikuwa ni sh.milioni 790 na sasa ni sh.bilioni saba jambo ambalo linatia faraja.
Mkurugenzi Mkuu wa MSD,  Laurean Bwanakunu alisema taasisi hiyo inatambua kuwa dawa za kansa ni gharama lakini atahakikisha zinaendelea kupatikana kwa wakati ili kuokoa maisha ya watanzania.Alisema suala la vifaa vya maabara ni tatizo linalohitaji mpango wa kitaifa wa manunuzi.
"Nawahakikishia Ocean Road ni mteja muhimu hivyo nipo tayari muda wote kuwahudumia leteni orodha ya mahitaji ya dharura hata leo," alisema.
Mfamasia wa Hospitali ya Rufaa ya Amana, Anna Kajiru alisema katika Hospitali hiyo upatikanaji wa dawa kutoka MSD ni asilimia 80 na kuwa hali hiyo imetokana na ushirikiano mzuri baina yao.
"Hivi sasa hali ya upatikanaji wa dawa ambazo zinahitajika sana na wananchi ni mkubwa mkubwa tofauti na zamani na hii inatokana na kazi nzuri inayofanywa na ninyi MSD" alisema Kajiru.
Mkurugenzi wa MSD, Laurean Bwanakunu na maofisa wake yupo katika ziara ya kikazi ya kutembelea Hospitali za Mkoa wa Dar es Salaam ambapo leo alitembelea Hospitali ya Rufaa ya Amana na Saratani ya Ocean Road na kesho atazitembelea Hospitali ya Taifa ya  Muhimbili, Vijibweni na Temeke.
  Mkurugenzi Mkuu wa MSD,  Laurean Bwanakunu (kulia), akizungumza na maofisa wa Hospitali ya Rufaa ya Amana wakati wa ziara yake ya kikazi ya siku moja Dar es Salaam leo ya kujua changamoto za upatikanaji wa dawa katika hospitali hiyo na kuzitafutia ufumbuzi. Kushoto ni Mganga Mkuu wa Hospitali ya Rufaa ya Amana, Meshack Shimwela.
 Mganga Mkuu wa Hospitali ya Rufaa ya Amana, Meshack Shimwela, akisisitiza jambo katika mkutano huo.
 Maofisa wa Hospitali ya Rufaa ya Amana wakimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa MSD,Laurean Bwanakunu.
 Meneja wa MSD Kanda ya Dar es Salaam , Celestine Haule akichangia jambo wakaz8i akizungumza na maofisa wa Hospitali ya Rufaa ya Amana.
 Mfamasia wa Hospitali ya Rufaa ya Amana, Anna Kajiru (kulia), akisisitiza jambo kwenye mkutano huo.
 Mkurugenzi Mkuu wa MSD,  Laurean Bwanakunu (wa sita kushoto), akiwa katika picha ya pamoja na maofisa wa Hospitali ya Rufaa ya Amana. 
 Mkutano ukiendelea.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani ya Ocean Road Dk. Julius Mwaiselage akizungumza katika mkutano huo.
 Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Laurean Bwanakunu akisisitiza jambo wakati akizungumza na maofisa wa Taasisi ya Saratani ya Ocean Road katika ziara hiyo ya siku moja.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani ya Ocean Road Dk. Julius Mwaiselage ( kulia), akiteta jambo na Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Laurean Bwanakunu wakati wa ziara hiyo.
Mkurugenzi Mkuu wa MSD,  Laurean Bwanakunu (wa tano kulia), akiwa katika picha ya pamoja na maofisa wa Taasisi ya Saratani Ocean Road. 

No comments: