Monday, October 16, 2017

Vigogo wa chuo cha Uhasibu (TIA) wapata dhamana.

Na Karama Kenyunko, blogu ya jamii.

Baada ya kukaa gerezani kwa siku tano, leo vigogo wawili wa zamani wa Chuo cha Uhasibu Tanzania (TIA) wameachiwa huru baada ya kukamilisha masharti ya dhamana waliyopewa ma Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu

Washtakiwa hao ambao wametimiza masharti ya na kuachiwa kwa Hakimu Mkazi Mkuu Thomas Simba ni, Kaimu Mtendaji wa (TIA), Shaha Hanzuruni na Mkuu wa Kitengo cha Fedha, Onesphor Luhungu wa Hakimu Mkazi Mkuu, 

Katika masharti yao ya dhamana kila mshtakiwa alitakiwa kuwa na wadhamini wawili ambao kila mmoja atasaini bondi ya milioni 250 na pia mdhamini mmoja kati ya wadhamini hao kuwasilisha fedha taslimu mahakamani Sh 250 milioni ama hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya kiasi hicho cha fedha na kwamba mali hiyo ni lazima iwepo Dar es Salaam.

Mbali na hayo kila mshtakiwa alitakiwa kusalimisha pasi yake ya kusafiria mahakamani na wasitoke nje ya jiji la Dar es Salaam bila ya kuwa na kibali cha Mahakama.

Kesi imeahirishwa hadi Oktoba 24,2017 ambapo washtakiwa hao watasomewa maelezo ya awali (PH).Washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka mawili likiwamo la matumizi mabaya ya madaraka na kusababisha hasara ya Sh 1, 097,681,107.

Mwendesha Mashtaka Mwandamizi wa Takukuru, Leonard Swai akiwasomea hati ya mashtaka washtakiwa hao alidai kuwa, kati ya Januari Mosi, 2012 na Desemba 30,2014 katika Chuo cha Uhasibu Tanzania kwa nafasi zao, walitumia madaraka vibaya kwa kutofuata taratibu za ununuzi katika kununua ardhi ya kampasi ya Chuo cha TIA Mwanza.

Alidai kuwa kitendo hicho kilisababisha Vedastus Ngasa Lukago kupata manufaa ya Sh 1, 097, 681,107.

Swai alidai kuwa, katika kipindi hicho cha Januari Mosi,2012 na Desemba 30,2014 washtakiwa hao wakiwa waajiliwa wa Chuo hicho, kwa ridhaa na kwamatendo yao walisababisha hasara ya Sh 1, 097,681,107.

Fedha ambayo ni Mali ya Chuo cha Uhasibu Tanzania kutokana na kutokufuata taratibu za manunuzi wakati wa kusaini mkataba wa ununuzi wa ardhi ya Chuo Cha Uhasibu Tanzania kampasi ya Mwanza.

Baada ya kusomewa mashtaka hayo washtakiwa walikana na upande wa mashtaka ulidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika.Washtakiwa hao, wanatetewa na Wakili , Jamuhuri Johnson.

No comments: