Thursday, October 12, 2017

TEMESA YATAKIWA KUKUSANYA MADENI YOTE KWA WADAIWA WAKE

Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi Elias Kwandikwa (wa pili kushoto) akipata maelekezo toka kwa Fundi Sanifu Mwandamizi toka kwa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Bw. Yakubu Kibingo wakati alipofanya ziara ya kikazi mapema hii leo jijini Dar es Salaam, kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Joseph Nyamuhanga, wa tatu toka kushoto ni Mtendaji Mkuu wa Wakala hiyo Mussa Ngwatu.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Mussa Ngwatu (wa pili kulia) akitoa maelekezo kwa Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi Elias Kwandikwa (wa pili kushoto) wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo mapema hii leo jijini Dar es Salaam, kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Joseph Nyamuhanga.
Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi Elias Kwandikwa (kulia) akipata maelekezo toka kwa Meneja Msaidizi wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Peter Bongele (katikati) wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo mapema hii leo jijini Dar es Salaam, kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Joseph Nyamuhanga.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi Joseph Nyamuhanga (kushoto) akimkaribisha Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi Elias Kwandikwa (katikati) kuzungumza na watumishi wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo mapema hii leo jijini Dar es Salaam, kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Mussa Ngwatu.
Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi Elias Kwandikwa (katikati) akizungumza na watumishi wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) (hawapo pichani) wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo mapema hii leo jijini Dar es Salaam, kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi Joseph Nyamuhanga na kulia ni Mtendaji.Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Mussa Ngwatu.
Baadhi ya watumishi wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) wakimsikiliza Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi Elias Kwandikwa (hayupo pichani) wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo mapema hii leo jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya watumishi wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) wakimsikiliza Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi Elias Kwandikwa wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo mapema hii leo jijini Dar es Salaam.
Picha na Eliphace Marwa – Maelezo


Na Thobias Robert


Naibu Waziri wa Ujenzi wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhe. Elias Kwandikwa ameitaka Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) kukusanya na kutumia madeni zaidi ya bilioni 10, inayozidai taasisi, idara na wakala mbalimbali wa sekta za umma na binafsi ili watumie pesa hizo katika shughuli za uzalishaji na maendeleo.

Waziri ameyasema hayo jijini Dar es Salaam alipofanya ziara ya kikazi kuongea na kuangalia utendaji kazi wa wafanyakazi pamoja na kukagua mitambo inayotumiwa na wakala hiyo iliyo chini ya wizara ya Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano.

“Madeni ni rasilimali ambayo tunahitaji kuisimamia vyema, chambueni vizuri madeni ambayo taasisi inadai kwenye taasisi, idara na wakala mbalimbali za serikali ili tuweze kuona namna gani tutafanya ili madeni hayo yalipwe, kwa sababu tukikaa na madeni mengi yatatukwamisha katika shughuli zetu,” alisisitiza Waziri Kwandikwa.

Aidha alisema kuwa wakala na idara zinazofanya kazi na TEMESA zinapaswa kulipa madeni wanayodaiwa ili kuiwezesha taasisi hiyo kufanya kazi kwa ufanisi zaidi kwa kutumia vifaa na miundombinu ya kisasa inayoandana na utoaji wa huduma unaofanya na TEMESA.

“Nitoe wito kwa taasisi mbalimbali zinazodaiwa na TEMESA ziweze kulipa haraka hayo madeni ili tuweze kufanya kazi vizuri zaidi, maana wangekuwa wanakwenda kwenye kampuni binafsi kama wanadaiwa basi magari yao yangekuwa yanakamatwa, sasa isije tukafika wakati na sisi kuanza kampeni ya kuzuia magari, kwa sababu lazima TEMESA isimame ili tuweze kutoa huduma vizuri,” aliongeza Waziri Kwandikwa.

Aliwataka wafanyakazi kufanya kazi kwa kujituma, uzalendo, umoja na kuzingatia sheria, taratibu pamoja na kanuni zilizowekwa kwa ajili ya kurahisisha utoaji wa huduma kwa wateja na wadau wanaotumia taasisi hiyo.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa TEMESA Dkt. Mussa Ngwatu alisema kuwa wamefanikiwa kufanya mambo mbalimbali tangu serikali ya awamu ya tano iingie madarakani ambapo, wameweza kununua boti ndogo 4 kwa ajili ya matumizi ya dharura katika maeneo mbalimbali katika mikoa ya Mtwara na Tanga.

“Katika mwaka wa fedha 2016/2017, ujenzi wa kivuko cha Mv. Magogoni umekamilika kwa gharama ya shilingi bilion 7, kivuko cha MV. Tanga kimekamilika kwa gharama ya shilingi bilioni 4, pia kivuko cha Mv Pangani kimekarabatiwa”.alifafanua Dkt. Ngwatu.

Aliongeza kuwa, mwaka huu wa fedha TEMESA wana mpango wa kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa maegesho ya kivuko cha Chato, mkoani Geita, ujenzi wa maegesho ya Lindi-Kitunda na0 ununuzi wa kivuko kipya cha Kigongo Busisi katika ziwa Viktoria kwa gharama ya bilioni 8.9 ambao utakamilika mwezi Januari mwakani.

Vilevile TEMESA inatarajia kufanya ununuzi wa kivuko kipya cha Kayenze-Bezi mkoani Mwanza, kukarabati vivuko vya Misungwi na Sengerema vilivyopo ziwa viktoria, pamoja na kivuko cha Kigamboni, ujenzi wa maegesho ya Malinyi pamoja na kuweka mashine za ukataji tiketi kwa njia ya kielektroniki katika kivuko cha Magogoni-Kigamboni.

Aidha Dkt. Ngwatu alisema kuwa TEMESA wanatarajia kuzalisha zaidi ya shilingi bilioni 71 katika kipindi cha mwaka wa fedha 2017/18, ambapo zaidi ya bilioni 40.3 ya fedha hizo ni kutoka katika vyanzo vya ndani na bilioni 22.7 ni fedha za ruzuku kutoka serikalini.

Aidha Dkt. Ngwatu alisema kuwa, kwa mwaka, wa fedha 2017/2018, wakala unatarajia kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 71 ambapo zaidi ya billion 40.3 ni kutoka katika vyanzo vya ndani na zaidi ya shilingi bilioni 22.7 ni fedha za ruzuku kutoka serikalini.

TEMESA ni wakala wa ufundi na umeme iliyopo chini ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ambayo ilianzishwa mwaka 1997 kwa lengo la kutoa huduma za uhandisi wa mitambo na umeme katika taasisi za serikali na binafsi.

No comments: