Tuesday, October 31, 2017

MAKAMU WA RAIS MAMA SAMIA SULUHU HASSAN AZITAKA TAASISI ZA FEDHA KUPUNGUZA RIBA YA MIKOPO

Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, akizundua rasmi Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo ya Fedha ya mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wake katika kipindi cha miaka 10 kuanzia 2017/2018 hadi mwaka 2027/2028, mjini Dodoma.
Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, akimkabidhi Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo ya Fedha ya mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Posta Tanzania –TPB Bw. Sabasaba Moshingi baada ya Sera na Mkakati huo kuzinduliwa rasmi, mjini Dodoma.
Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, akimkabidhi Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo ya Fedha ya mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wake, Mwenyekiti wa Kikundi cha Akiba na Mikopo-(KIKOBA) cha Mwende Manispaa ya Dodoma, Bi. Bertha Chisawilo, baada ya Sera na Mkakati huo kuzinduliwa rasmi, mjini Dodoma.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), akimpongeza Mwenyekiti wa Kikundi cha Akiba na Mikopo-(KIKOBA) cha Mwende, Manispaa ya Dodoma, Bi. Bertha Chisawilo, baada ya Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, kumkabidhi Mwenyekiti huyo, Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo ya Fedha ya mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wake, baada ya Sera na Mkakati huo kuzinduliwa rasmi, mjini Dodoma.
Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, akimkabidhi Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo ya Fedha ya mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wake, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika lisilo la Kiserikali linalojihusisha na masuala ya fedha (Financial Sector Deepening Trust-FSDT), Bw. Sosthenes Kewe, baada ya Sera na Mkakati huo kuzinduliwa rasmi, mjini Dodoma.



Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Mhe. Hawa Ghasia (Mb), akichangia mada kuhusu umuhimu wa huduma za fedha hususan vijijini, kabla Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, hajazindua rasmi 




Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Khatibu Kazungu (Sera), akizungumza maneno ya utangulizi wakati wa uzinduzi wa Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo ya Fedha ya mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wake katika kipindi cha miaka 10 kuanzia 2017/2018 hadi mwaka 2027/2028,  iliyozinduliwa na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango mjini Dodoma.




Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), akizungumzia mapinduzi makubwa yaliyofanywa na Serikali kwa kuja na Sera ya kuhudumia Sekta Ndogo ya Fedha nchini ijulikanayo kama Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo ya Fedha ya mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wake katika kipindi cha miaka 10 kuanzia 2017/2018 hadi mwaka 2027/2028,  iliyozinduliwa na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango mjini Dodoma.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa-TAMISEMI, Mhe. Selemani Jafo (Mb), akielezea utayari wa Wizara yake katika kutekeleza Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo ya Fedha ya mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wake katika kipindi cha miaka 10 kuanzia 2017/2018 hadi mwaka 2027/2028, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango mjini Dodoma.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), akielezea umuhimu wa Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo ya Fedha ya mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wake katika kipindi cha miaka 10 kuanzia 2017/2018 hadi mwaka 2027/2028 katika kukuza uchumi na kuondoa umasikini katika jamii, wakati wa uzinduzi wa sera hiyo mjini Dodoma.

Picha na Kitengo cha Mawasiliano serikalini-Wizara ya Fedha nan Mipango



Na Benny Mwaipaja, Dodoma


MAKAMU wa Rais Mhe. SAMIA SULUHU HASSAN, amezinduzi Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo ya Fedha ya mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wake katika kipindi cha miaka 10 kuanzia 2017/2018 hadi mwaka 2027/2028, tukio  litakalofanyika Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango mjini Dodoma.

Makamu wa Rais ametoa wito kwa watoa huduma ndogo za fedha kupunguza riba za mikopo na tozo mbalimbali ili kufanikisha lengo la Sera hiyo ambalo ni kuimarisha huduma jumuishi za fedha kwa kujenga mazingira wezeshi yatakayoleta ufanisi wa utoaji wa huduma ndogo za fedha nchini kwa wananchi wenye kipato cha chini.

“Ninawaomba pia muongeze ubunifu katika kutoa huduma zinazohitajika na wananchi wa kipato cha chini pamoja na kupeleka huduma hizo katika maeneo yaliyo karibu na makazi yao au biashara zao” aliongeza Mhe. Samia Suluhu Hassan

Alizitaka taasisi za huduma za fedha kuwaelimisha wananchi kabla ya kutoa huduma hizo ili kupunguza athari wanazozipata wananchi.

“Ni matarajio yangu kuwa, Wizara ya Fedha na Mipango itashirikiana na wadau katika kutekeleza Sera hii na kuhakikisha malengo ya Sera ambayo ni   kukuza uchumi na kupunguza umaskini yanafikiwa” alisisitiza

Alisema Ripoti ya Finscope ya mwaka 2017 ambayo iilionesha kuwa Tanzania imepiga hatua kwenye suala zima la huduma jumuishi za fedha (financial inclusion) na kufikia asilimia 72 kwa 2017, huku changamoto kuu iliyoainisha ni elimu/uelewa mdogo wa huduma za fedha kwa wananchi.

Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango alisema kuwa Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wake itaweka mazingira yatakayowezesha kuchochea maendeleo stahiki na ubunifu wa Huduma Ndogo za Fedha ili kukidhi mahitaji halisi ya wananchi wa kipato cha chini na hivyo kuongeza ukuaji wa uchumi na kupunguza umaskini.

Alisema kuwa Sera hiyo itaongeza utoaji wa huduma bora na jumuishi ya Kifedha Vijijini na kutungwa kwa sheria ambazo zitawalinda wananchi dhidi ya baadhi ya taasisi za kifedha zinazoibuka na kuwa kero kwao kwa kuweka riba kubwa pamoja na kupatiwa huduma zisizoridhisha.

“Sera ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wake vitaendelea kutoa miongozo kwa wadau wote na kuchochea uanzishwaji wa washiriki wapya na ukuaji wa waliopo ili kutoa ushindani zaidi ili kuleta matokeo yatakayoongeza huduma rasmi, kukuza utamaduni wa kuweka akiba, kuimarisha sekta ndogo ya fedha, ambayo yatachangia ukuaji wa uchumi, ajira na kupunguza umaskini” Aliongeza Dkt. Mpango

Sekta ya huduma ndogo ya fedha nchini inajumuisha aina ya watoa huduma za fedha wafuatao: benki na taasisi za fedha zinazotoa huduma ndogo za fedha; vyama vya ushirika wa kuweka akiba na kukopa; kampuni za huduma  ndogo za fedha kama vile BRAC, Blue Finance, Tujijenge, Platinum n.k,

Nyingine ni asasi za fedha zisizo za Serikali, Mifuko na Programu za Serikali; na Vikundi vya Kifedha vya Kijamii kama vile asasi za kijamii, benki za kijamii za vijiji (VICOBA), Ushirik a wa akiba na mikopo vijijini (VSLAs), Ushirika wa akiba na mikopo kwa zamu (ROSCAs), wakopeshaji binafsi na wengine wanaotoa huduma zinazohusiana na fedha.

Serikali kwa kutambua umuhimu wa upatikanaji wa Huduma Ndogo za Fedha kwa wananchi wa kipato cha chini iliamua kufanya mapitio ya Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2000 kwa kutunga Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2017 na Mkakati wa Utekelezaji wa Sera hiyo kwa kipindi cha miaka kumi ili kutatua changamoto zilizojitokeza katika sekta ndogo ya fedha

Changamoto hizo ni pamoja na ongezeko la idadi ya watoa Huduma Ndogo za Fedha; Ukosefu wa mfumo wa Sheria na Kanuni za kusimamia Taasisi Zisizochukua Amana na Vikundi vya Fedha vya Kijamii; Ukosefu wa mfumo wa kumlinda Mtumiaji na mtoa Huduma Ndogo za Fedha na uelewa mdogo wa masuala ya fedha; Kutokuwepo na uwazi katika vigezo na masharti ya utoaji mikopo; Viwango vya juu vya riba; na Kuibuka kwa taasisi zisizo kuwa na uaminifu.

No comments: