Wednesday, August 23, 2017

TTCL YAPEWA CHANGAMOTO KUFIKA VIJIJINI


NAIBU Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhe Mhandisi Edwin Ngonyani, ameitaka Kampuni ya Simu Tanzania TTCL kuongeza juhudi za kutoa huduma kwa Wananchi hasa waliopo katika maeneo ya Vijijini ili kuwawezesha Wananchi kupata Mawasiliano ya uhakika kutoka katika Kampuni yao Umma.

Mhe Ngonyani ametoa maelekezo hayo alipofanya ziara fupi ya kutembelea Makao Makuu ya TTCL ambapo amepata fursa ya kuzungumza na Bodi na Menejimenti ya TTCL ambapo alitumia hadhatra hiyo kutoa mrejesho wa ziara yake ya kutembelea maeneo mbali mbali ya Tanzania Bara na Visiwani kukagua huduma za Taasisi zilizo chini ya Wizara yake.

Mhe Ngonyani amesema, pamoja na mafanikio makubwa ambayo TTCL imeyapata katika Viwango vya ubora wa huduma, kuongeza idadi ya Wateja, usimamizi na uendeshaji wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano (NICTBB) na Kituo cha Kutunzia Kumbukumbu za Kimtandao( NIDC) bado TTCL inakabiliwa na changamoto kubwa ya kufikisha huduma ya Mawasiliano Vijini hasa katika maeneo ambayo kwa sasa hayana Mawasiliano kabisa baada ya kuzimwa mwa mitambo ya Mawasiliano iliyokuwa ikitumia teknolojia ya CDMA.

Aidha, Mhe Ngonyani ameiagiza Bodi na Menejimenti ya TTCL kuongeza kasi ya kusambaza huduma za TTCL 4G pamoja na kufanyia kazi kilio cha muda mrefu cha Watumishi wa TTCL kuomba kuboreshewa Maslahi yao.

“Pote nilipopita Bara na Visiwani, Watumishi wa TTCL wameniomba nifikishe kilio chao kwenu, wamekaa kipindi kirefu sana bila kuboreshewa maslahi yao huku gharama za maisha zikiwa juu. Ninashauri msikie kilio hiki ili pamoja na kuboresha huduma zenu, mazingira ya kazi na maslahi ya Watumishi pia yapewe kipaumbele,”

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya TTCL Mhe Mhandisi Omari Rashid Nundu amesema, Bodi na Menejimenti ya TTCL zimepokea maelekezo ya Mhe Naibu Waziri na kwamba mpango mkakati wa muda mfupi uliowekwa na Kampuni hiyo, changamoto hizo zitafanyiwa kazi.

“Mhe Naibu Waziri, tunayo nia ya dhati ya kuibadilisha TTCL na kuifanya iwe kweli Kampuni ya Umma inayowaunganisha Watanzania. Tumedhamiria kuwafikia Wananchi wote kwa huduma za kiwango cha juu na unafuu sana wa gharama sambamba na kuimarisha vitendea kazi na maslahi ya Watumishi. Tunaomba Serikali iendelee kutuunga mkono na kutuwezesha kutimiza mipango hii,” amesema Mhandisi Nundu.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa TTCL Bw Waziri Waziri Kindamba amesema, TTCL mpya imejipanga kikamilifu kujiendesha kibishara na kufikia lengo la kutoa gawio Serikalini. Bw Kindamba ameongeza kuwa, TTCL kupitia kauli mbiu yake ya Rudi Nyumbani imekusudia kuhakikisha kuwa Watanzania wote wanapata huduma za Mawasiliano kwa Teknolojia za 2G/3G na 4G LTE sambamba na huduma za kifedha za TTCL PESA ambayo imezinduliwa hivi karibuni.

Mapema mwezi ulipita, TTCL ilizindua huduma za kifedha kwa njia ya Mtandao ijulikanayo kama TTCL PESA. TTCL PESA itawawezesha Wananchi kupata huduma mbali mbali kama Kutuma Fedha, Kulipia Ankara za huduma kama vile Maji, Umeme (LUKU), Ving’amuzi na Kununua vifurushi vya TTCL huku huduma nyingine zikiendelea kuongezwa.

Aidha,TTCL PESA itasaidia katika kufanya makusanyo ya tozo za Serikali pamoja na kuongeza usalama na kupunguza hatari ya kupotea kwa fedha kupitia vitendo vya uhalifu kama ujambazi wanavyofanyiwa Wananchi (Wakulima na Wafugaji) wanaotembea na fedha nyingi katika maeneo mbali mbali wanapofanya biashara zao za mazao na mifugo.


Afisa Mtendaji Mkuu wa TTCL Bw Waziri Waziri Kindamba (kushoto) akizungumza jambo na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mh. Mhandisi Edwin Ngonyani (kulia) mara baada ya kuwasili katika ofisi yake kusaini kitabu cha wageni.
Sehemu ya menejimenti ya kampuni ya TTCL ikiwa katika kikao hicho na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mh. Mhandisi Edwin Ngonyani alipowatembelea.
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Mhandisi Edwin Ngonyani (kulia) akizungumza na wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) leo Makao Makuu ya kampuni hiyo alipotembelea na kuzungumza na Bodi hiyo katika ziara yake ya kutembelea taasisi zilizo chini ya wizara yake. Kulia ni Mwenyekiti wa Bodi ya TTCL, Mhandisi Omar Nundu.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) Mhandisi Omar Nundu (kushoto) akitoa maelezo mafupi kuhusiana na utendaji kazi wa kampuni hiyo kwa Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mh. Mhandisi Edwin Ngonyani (kulia) alipotembelea na kuzungumza na Bodi ya TTCL leo Makao Makuu ya TTCL jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Afisa Mtendaji Mkuu wa TTCL, Bw Waziri Waziri Kindamba akiwa katika kikao hicho.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) Mhandisi Omar Nundu (kushoto) akitoa maelezo mafupi kuhusiana na utendaji kazi wa kampuni hiyo kwa Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mh. Mhandisi Edwin Ngonyani (kulia) alipotembelea na kuzungumza na Bodi ya TTCL leo Makao Makuu ya TTCL jijini Dar es Salaam.

No comments: