Monday, August 7, 2017

MBUNGE KIBAHA VIJIJINI AWASAIDIA WANANCHI JIMBONI KWAKE

Na Mwamvua Mwinyi, Kibaha Vijijini 
MBUNGE wa jimbo la Kibaha Vijijini, mkoani Pwani, Hamoud Jumaa, ametoa msaada wa sh.milioni 2.3 kwa mkazi wa kata ya Janga, Selemani Mgoto (43) ambaye alipata upofu kutokana na kudhurika na vidonge vya malaria 'fansidar' mwaka 2012.
Aidha mbunge huyo, amesema ataendelea kumshika mkono Mgoto kwa kumalizia ujenzi wa nyumba anayojenga. Jumaa pia ,anamjengea nyumba kada wa chama cha mapinduzi (CCM) ambaye aliwahi kukitumikia chama zaidi ya miaka 30, mzee Shabani Kifaru (80), mkazi wa kata ya Magindu.

Akizungumza wakati akikabidhi fedha hizo, Jumaa  alisema ataendelea kutatua changamoto za jimbo pamoja na kusaidia makundi maalum. Alieleza, ametoa fedha hizo kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa mtu huyo kuliko chakula ambacho angekula na kuisha .
Alisema licha ya Mgoto kuathirika macho yake lakini anaishi kwenye maisha ya kupanga hivyo nyumba anayojenga itamwezesha kuishi vizuri. Nae Mgoto ,alimshukuru Jumaa kwa msaada aliompatia na kumuomba asichoke kumshika mkono. Hata hivyo, aliwashukuru wadau wengine ambao wameweza kumsaidia tangu apate matatizo yake.
"Mbunge una watu wengi wa kuwasaidia lakini umeniona na mie, naahidi kuzitumia fedha hizi kwa matumizi lengwa ,nilianza ujenzi huu lakini ninekwama kumalizia "alisema Mgoto.
Akizungumzia juu ya tatizo lake la macho alisema bado amekwama kwenda nchini India kupata matibabu. Alisema Muhimbili walimwambia atafute msaada mtaani lakini amekwama. Mgoto alimuomba waziri wa afya,jinsia, wazee na watoto Ummy Mwalimu na mbunge huyo waendelee kumpigania apate rufaa ya serikali ili aweze kupona. 
Alisema wataalamu wa afya na hospital zote alizopita zimemhakikishia kuwa kwa asilimia 98 akipata matibabu atapona. Baada ya hapo alielekea kwa mzee Kifaru ambae aliwahi kuwa mwenyekiti wa CCM kata ya Magindu ambae anamjengea nyumba kutokana na kuishi kwenye mazingira yasiyoridhisha .
"Juzi nimepita hapa kwenye chaguzi za chama nikapita kumsalimia nikakuta akiwa amefiwa na mkewe na kumkuta anaishi kwenye mazingira magumu, Imenisikitisha nikaona ni vyema nimsaidie kumjengea nyumba ya kuishi na ukizingatia umri wake huu hawezi kujishughulisha wala kujenga nyumba, mimi kama mbunge nimemsaidia" alisema Jumaa.
Kwa upande wake, mzee Kifaru, alisema 1977 alichaguliwa kuwa kiongozi katika kata hiyo hivyo ni kada wa CCM na muasisi. Alisema ,wabunge wengi wamepita lakini kumpata Hamoud Jumaa anamshukuru kwa msaada aliompa.
"Mungu amjalie katika kazi zake, mnajua alinikuta hata mtu akipita nje alikuwa anaona kitanda ndani, madongo yamedondoka ndipo alipoguswa kunisaidia " alisema mzee Kifaru.
Mzee Kifaru ,alimsihi mbunge huyo aendelee na juhudi na kuchapa kazi kwake bila kuchoka ili kuweza kulisogeza kimaendeleo na kiuchumi jimbo hilo.


No comments: