Na Felix Mwagara (MOHA)
MWENYEKITI wa Baraza la
Taifa la Usalama Barabarani, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya
Nchi, Mhandisi Hamad Masauni amesema Baraza lake litakutana kujadili uwezekano
wa Jeshi la Polisi, Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) pamoja na Chuo cha
Usafirishaji (NIT) ziweze kuungana ili kufanya ukaguzi wa lazima wa magari kwa
lengo la kuondoa ajali nchini.
Akizungumza jijini Dar
es Salaam jana mara baada ya kumaliza ziara yake ya kutembelea ofisi za Temesa
na Chuo cha NIT, Masauni alisema ziara yake ilikua na mafanikio makubwa, hivyo anatarajia
kukutana na Wajumbe wa Baraza lake katika vikao vyao na kuwasilisha uzoefu
alioupata mara baada ya kuzitembelea Taasisi hizo za Serikali.
“Nimeshuhudia Temesa na
NIT mambo ambayo sikuyatarajia, inaonyesha kwamba katika vita ya kuzuia ajali
nchini hatutaanza sifuri, tunasehemu fulani ya kuanzia, tutaanza na utaratibu
wenye mfumo mzuri ambao utaweza kutekelezwa ili kufikia malengo ya kuwa na
utaratibu wa lazima wa ukaguzi wa magari yote ambayo yanatumika katika nchi
yetu,” alisema Masauni na kuongeza;
“Lengo la mipango hiyo
ni kuhakikisha tunakuwa na magari mazuri ambayo hayawezi kusababisha ajali,
hivyo nitawasilisha katika kikao hicho chha Baraza uzoefu huu nilioupata baada ya
ziara hii ili nijadiliane na wajumbe wenzangu tuone jinsi tutakavyokubaliana
kuhusiana na mafanikio niliyoyapata baada ya ziara hii.”
Pia alisema lengo la
kuunganisha nguvu kwa kuungana kwa taasisi hizo za Serikali ni kufanikisha
zaidi makabiliano ya ajali za barabarani, ambapo kwasasa Jeshi la Polisi pekee
ndilo linalofanya ukaguzi wa lazima nchini, hivyo nguvu inahitajika endapo
kutakua na muungano wa taasisi hizo ikiwa na lengo moja la kuijenga Tanzania.
Hata hivyo, Masauni aliongeza
kuwa, katika kufanikisha hilo, kuna umuhimu wa kumtafuta mshauri mwelekezi ili
afanye utafiti wa kina ili aweze kushauri jinsi ya kuvitumia vyombo na taasisi
zetu zilizopo nchini, nini kifanyike ili kuweza kufikia muafaka wa namna bora
ya kuweza kufanya ukaguzi wa magari wa lazima uanze kazi haraka iwezekanavyo ili kuweza kupunguza
ajali za barabarani ambazo nyingi zinasababishwa na ubovu wa magari.
Masauni akiwa Temesa
alitembelea karakana ya utengenezaji wa magari na kujionea kazi mbalimbali
ambazo zinafanywa na wataalamu katika karakana hiyo inayotengeneza magari ya
Serikali pamoja na watu binafsi, ambapo aliona watalaamu wa Taasisi hiyo
wanavyotumia vifaa mbalimbali vya matengenezo ya magari ikiwemo uwepo wa mashine
ya kisasa ya kukagulia magari kwa njia ya umeme.
Alipokuwa katika Chuo
cha NIT, Masauni alifanikiwa kupata taarifa fupi ya historia ya chuo hicho
pamoja na kozi mbalimbali zinazotolewa chuoni hapo zikiwemo za masuala ya
usalama barabarani. Pia alitembelea sehemu ya kisasa ya ukaguzi wa magari
chuoni hapo pamoja na madarasa ya Wahudumu wa Ndege pamoja na Marubani ambapo
ni kozi ipya ya masuala ya anga inayotarajiwa kuanzishwa chuoni hapo hivi
karibuni.
Aidha, Mkuu wa Chuo
hicho, ambaye pia ni Mjumbe wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, Profesa Zakaria
Mganilwa, alisema chuo chake kina kituo kilichofungwa mitambo ya kisasa ya
kukagua magari ambapo kituo hicho kina uwezo wa kukagua magari mia sita kwa
siku.
“Kama utaratibu utaweza
kuwekwa wa kukagua magari, chuo kipo tayari kwasababu mitambo ipo na tumeajiri
vijana ambao wanauwezo mkubwa wa kuhudumia idadi hiyo ya magari kwa siku,”
alisema Mganilwa.
Masauni alimaliza ziara
yake ya siku moja ambayo ilikua na lengo la kufanikisha utekelezaji wa
mapendekezo ya Kamati iliyoundwa na Baraza lake la Usalama Barabarani katika
hatua ya kukabiliana na ajali za barabarani ambazo zinasababishwa na mambo
makuu matatu, moja ni matatizo ya kibinadamu, pili matatizo ya miundombinu, na tatu
ubovu wa magari au vyombo vya moto ambako ndio lengo kuu la kuunganisha taasisi
hizo ili kupata nguvu zaidi katika ukaguzi wa magari nchini.
No comments:
Post a Comment