Wednesday, August 23, 2017

MAKAMU WA RAIS AFUNGUA MKUTANO WA SIKU 2 WA TAIFA WA URUTUBISHAJI WA CHAKULA

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amewataka wataalamu wa masuala ya lishe na urutubishaji chakula kuwa mstari wa mbele katika kutoa elimu ya virutubisho kwa wananchi.

Makamu wa Rais ameyasema hayo leo wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa siku mbili wa Kitaifa kuhusu Urutubishaji Chakula uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere, Jijini Dar es Salaam.

Mhe. Samia Suluhu alisema ukosefu wa upatikanaji wa vyakula vyenye virutubisho   unaweza kuathiri Taifa hasa wakati huu nchi inapolekea kuwa Tanzania ya viwanda, Alielekeza ushirikishwaji na wadau malimbali katika kukabiliana na changamoto utasaidia kupunguza tatizo hili , takwimu zinaonyesha hali yetu ya lishe bado hairidhishi ila ni vyema kuweka nguvu pamoja ili watoto wetu ambao ni Taifa la Kesho waweze kujenga Taifa imara.

Makamu wa Rais alisema Tanzania ina asilimia 34 ya watoto wenye udumumavu pamoja na magonjwa mengine kama mgongo wazi na vichwa vikubwa kutokana na lishe duni.Makamu wa Rais alisema atakuwa na mkataba na Wakuu wote wa mkoa kuhakikisha kila mkoa unaweka takwimu zake vizuri na jitihada wanazofanya kuelimisha wananchi wao umuhimu wa lishe bora na virutubishi.

Alisema kuna umuhimu wa sekta husika kuwa na mfumo wa kutunza kumbukumbu zinazoonyesha taarifa kuhusu aina ya virutubisho kuweza kufanikisha kuondoa tatizo hili lazima uwekezaji ufanyike haswa kwenye kutunza kumbukumbu , taarifa na aina ya virutubisho  na matokeo yake baada ya matumizi.

Makamu wa Rais alisema yeye kama Mama, mlezi wa masuala ya lishe  na kama Kiongozi Mwanamke anaguswa sana na suala la lishe duni na ameahidi kuendelea kulisimamia kwa ukaribu na alimuelekeza Waziri wa TAMISEMI kuhakikisha kuwa  fedha zilizotengwa kwa ajili ya uitoaji wa tembe za folic acid kwa akina mama zinapatikana na kuweza kupunguza vifo vya watoto wanaozaliwa na matatizo kutokana na ukosefu wa chakula chenye virutubisho.

Nae Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu alisema kuwa Serikali itaendelea kusimamia  sera , mpango mkakati, wa lishe na taratibu zilizowekwa kama mpango mkakati wa masuala ya lishe na kuhakikisha kuwa suala la upatiknaji wa lishe bora unaendelea kuwa kipaumbele .

 Naibu Waziri Nishati na Madini Dkt. Medard Kalemani  alisema kwa miaka 30 sasa serikali inaendelea na suala la kuweka madini joto kwenye chumvi ni la kisheria na sera na mzalishaji yeyote atakaekiuka adhabu yake ni kifungo kisichozidi miezi sita au kama faini isiyopungua milioni mbili kwani mahitaji ya madini joto kwenye chumvi ni muhimu katika ukuaji wa mtoto na kujenga akili.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akihutubia wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Taifa wa Urutubishaji wa Chakula uliofanyika kwenye kituo cha Mikutano Cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)
 Baadhi ya wadau mbalimbali wakimsikiliza Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan alipokuwa akihutubia katika Mkutano wa Taifa wa Urutubishaji wa Chakula uliofanyika kwenye kituo cha Mikutano Cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)
 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akikata keki iliyopikwa kwa unga wa mahindi wenye vitamini A na ngano mara baada ya ufunguzi wa Mkutano wa Taifa wa Urutubishaji wa Chakula uliofanyika kwenye kituo cha Mikutano Cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na watoto waliozaliwa na tatizo la vichwa vikubwa na mgongo wazi (Hydrocephalus and Spina Bifida) na wazazi wao wakati ufunguzi wa Mkutano wa Taifa wa Urutubishaji wa Chakula uliofanyika kwenye kituo cha Mikutano Cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipata maelezo ya virutubishi vya watoto kutoka kwa makamu Mkurugenzi wa Shirika la SOLEO Bi. Grace Mghamba ​mara baada ya ufunguzi wa Mkutano wa Taifa wa Urutubishaji wa Chakula uliofanyika kwenye kituo cha Mikutano Cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)
 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Mkurugenzi wa WFP nchini Bw. Michael Danford wakati akiwasili kwenye ufunguzi wa Mkutano wa Taifa wa Urutubishaji wa Chakula uliofanyika kwenye kituo cha Mikutano Cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)

No comments: