Sunday, July 2, 2017

WANAWAKE WAPONGEZA MWENGE WA UHURU KUWAEPUSHA KUCHANGIA MAJI NA MIFUGO


Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa uhuru Amour Hamad Amour akimtwisha ndoo ya maji moja ya akina mama waliojitokeza kushuhudia uzinduzi wa mradi wa maji katika kijiji cha Merya Wilayani Singida.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa uhuru Amour Hamad Amour akifungua maji katika bomba wakati wa uzinduzi wa mradi huo katika kijiji cha Merya Wilayani Singida, pembeni yake Mkimbiza Mwenge Kitaifa Fredrick Ndahani.


Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa uhuru Amour Hamad Amour akitazama vitunguu katika shamba la mboga mboga la umwagiliaji kwa njia ya matone wakati wa uzinduzi wa mradi huo katika kijiji cha Msange Wilayani Singida.
Sehemu ya shamba la mbogamboga lenye kilimo cha umwagiliaji kwa njia ya matone ambapo vitunguu vinaonekana vimestawi vizuri, shamba hilo lina ukubwa wa ekari 25.

…………………….

Wanawake wa Vijiji vya Merya na Ikugha katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida wameushukuru Mwenge wa Uhuru kwa kuwafungulia mradi ambao umewaepusha kutembea umbali mrefu kutafuta maji ya kutumia ambayo si safi wala salama huku wakiyachangia na mifugo yao.

Wanawake hao wametoa pongezi hizo mara baada ya kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru Amour Hamad Amour kufungua mradi wa maji wenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 49 utakaohudumia vijiji hivyo ambao umegharimiwa na shirika la saving International, halmashauri ya Singida pamoja na michango ya wananchi.

Wamesema kabla ya kupatikana mradi huo wanawake wa vijiji hivyo wamekuwa wakifuata maji umbali mrefu sana kiasi cha kushindwa kutekeleza shughuli nyingine za kuzalisha mali.

“Tulikua tunatembea mpaka tunachoka, tunaamua kupumzika njiani kwanza ndio tuendelee na safari ya kuleta maji nyumbani, yani tunashukuru sana kwakweli”, ameongea Bi Greta Senge Mkazi wa kijiji cha Ikugha.

Aidha wameongeza kuwa mradi huo utawapatia maji safi na salama kwakuwa maji waliyokuwa wakiyafuata umbali mrefu hapo awali yalikuwa machafu na si salama.

“Yani tulikuwa tunachota maji ambayo unakuta ng’ombe anakunywa hapohapo, wakati mwingine anajisaidia na inabidi uchote hivyo hivyo, kwakweli tunaushukuru sana mwenge kutufungulia mradi huu, tulikua tunaumwa matumbo kila mara”, ameongeza Rehema Lazaro.

Wameongeza kuwa mradi huo utapunguza magonjwa ya tumbo na macho ambayo yamekuwa yakiwasumbua mara kwa mara hukua wakiridhia kulipia kiasi cha shilingi 50 kwa lita 20 za maji ili kupata fedha za kutunza mradi huo.

Kwa upande wake kiongozi wa Mbio za Mwenge wa uhuru Amour Hamad Amour ameitaka jumuiya ya watumia maji ya mradi huo kuutunza mradi huo ili utoe maji kwa wingi na muda huo kutokanana kuonekana ni hitaji la muhimu.

“Nimefika hapa na kushuhudia akina mama wengi mnamiminika na ndoo ili mpate maji, hii ni ishara kuwa mradi huu ni muhimu hivyo basi jumuiya ya watumia maji hakikisheni mda wote maji yanatoka na sio kupanga masaa ya kutoa maji au mvua ikinyesha tu mnayafunga, hapana” amesisitiza Amour.

Amesema mradi huo usimamiwe vizuri kusiwe na upendeleo au ubaguzi wowote kwakuwa maendeleo hayo hayana ubaguzi wa rangi, dini, itikadi za kichama au makabila.

Amour amesema jumuiya hiyo ihakikishe miundombinu ya mradi huo inatunzwa ili kuepusha kuwarudisha akina mama hao katika shida waliyokuwa wakiipata awali huku akiwashauri kuangalia namna ya kuipatia mifugo maji pamoja na kuweka taratibu nzuri za mapato na matumizi ya mradi huo.

Wakati huo huo Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru amezindua mradi wa umwagiliaji mbogamboga kwa njia matone wa ekari 25 wenye thamani ya shilingi milioni 326 katika kijiji cha Msange.

Akisoma taarifa ya mradi huo Afisa Kilimo wa Halmashauri ya wilaya ya Singida Adam Mngale amesema mradi huo ulianzishwa mwaka 2012 na hadi sasa una wanachama 32 ambao wananufaika kwa kujiongezea kipato kutokana na kulima misimu miwili yani kiangazi na masika.

Mngale amesema malengo ya mradi huo ni kuongeza eneo la uzalishaji hadi kufikia ekari 1400, kupanua miundombinu ili waweze kutumia kutumia bwawa la suke na lililoko eneo jirani katika umwagiliaji na kutumia kiwanda cha kusindika mbogamboga kilichoko Msange kusindika mazao yao.

1 comment:

Tom olali said...

Mwenge wa Uhuru umesaidia katika utoaji wa maji safi ili kuwalisha mifugo pamoja na miradi ya kilimo.