Saturday, July 15, 2017

TRA YAVIFUNGULIA VITUO VITATU VYA MAFUTA BAADA KUTIMIZA MASHARTI YA KUFUNGA MASHINE ZA KIELEKTRONIKI


Na Kajunason Blog/Cathbert Kajuna. 
 Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imevifungulia vituo vya mafuta vipatavyo vitatu jijini Dar es Salaam baada ya kutimiza masharti ya kufunga mashine za kielekitroniki zinazotoa risiti moja kwa moja kutoka kwenye pampu ya mafuta (Automatic EFD).
 Akizungumza mara baada ya kufungua vituo hivyo, Kamishina wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Charles Kichere amewashukuru wamiliki wa vituo hivyo kwa kuonyesha ushirikiano kwa serikali kwa kutimiza masharti waliyopewa ya kufunga mashine hizo na kusisitiza kuwa hakuna kituo kitakachofunguliwa kama hakitatimiza masharti. 
 "Niwaombe wamiliki wa vituo vilivyofungiwa kuwa kwa sasa hakuna kitakachofunguliwa bila kutimiza mashart, timiza masharti tuje tukague na tukufungulie uanze biashara yako," amesema Kamishna Kichere. Amesema vituo vilivyofunguliwa leo ni GBP kilichopo eneo la Majumba Sita, Simba Oil kilichopo eneo la Sitakishari, Ukonga na PETRO kilichopo eneo la Kigamboni. 
 "Kitendo cha kuunganisha mashine hizi na pampu za mafuta ni cha muda mfupi sana na wala hakichukui muda mrefu, angalia huyu tulimfungia siku ya jumanne tarehe 11 Julai na leo Ijumaa Julai 14 ameshafunga mashine na anaanza kufanya biashara bila kugombana na serikali;" amesema Kamishna Kichere. Mpaka sasa vituo zaidi ya 40 vimefungiwa nchi nzima ikiwemo jijini Dar es Salaam kwa kosa la kushindwa kufunga mashine za kielekitroniki zinazotoa risiti moja kwa moja kutoka kwenye pampu ya mafuta (Automatic EFD). 
Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Charles Edward Kichere akikata utepe katika kituo cha mafuta cha Kigamboni jijini Dar es Salaam baada ya kutimiza masharti ya kufunga mashine za kielekitroniki zinazotoa risiti moja kwa moja kutoka kwenye pampu ya mafuta. Wafanyakazi wakifurahia baada ya kufunguliwa kituo chao.
Mfanyakazi wa kituo cha mafuta cha Kigamboni akitoa risiti mara baada ya kuuza mafuta.
Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Charles Edward Kichere akikagua risiti mara baada ya kuuza mafuta.
Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Charles Edward Kichere akiuza mafuta katika kituo cha GBP kilichopo uwanja wa ndege mara  baada ya kukifungulia.
Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Charles Edward Kichere akiongea na vyombo vya habari mara baada ya kumaliza zoezi ya kufungulia vituo vipatavyo vitatu vilivyokuwa vimefungwa tokea juzi baada ya kushindwa kufunga mashine za kielekitroniki zinazotoa risiti moja kwa moja kutoka kwenye pampu ya mafuta.

No comments: