Tuesday, July 11, 2017

DC- TABORA AONGOZA ZOEZI LA KUWAONDOA WAKULIMA WA MBOGA MBOGA WAVAMIZI WA BWAWA LA IGOMBE.


Na Tiganya Vincent-RS-Tabora

Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya ya Tabora imeendesha oporesheni ya kung’oa mazao mbalimbali ya bustani yaliyokuwa yamepandwa na wavamizi katika maeneo ya vyanzo vya maji na kando kando ya Bwawa la Igome na hivyo kusababisha uzalishaji wa maji kupungua.

Kamati hiyo iliyoongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Tabora Mwalimu Queen Mlozi iliendesha zoezi hilo jana mjini hapa baada ya kugunduliwa kuwepo kundi kubwa la watu wanaondeshea kilimo cha mazao mbalimabli ikiwemo matunda na kuhatarisha afya ya watumiaji.

Katika oporesheni hiyo mazao mbalimbali kama vile majani ya maboga, hoho, nyanya na matembele yaliweza kung’olewa.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya zoezi alisema kuwa wavamizi hao wakiendesha shughuli mbalimbali katika vyanzo vya Bwawa hilo ikiwemo kilimo cha mboga mboga na wakati mwingine wamekuwa wakiweka dawa ambazo wakati mwingine dawa hizo zimekuwa zikiingia katika maji hayo ambayo ndio wakazi wengi wa Wilaya ya Tabora wanatumia.

Mwalimu Mlozi aliongeza kuwa endapo maji hayo yasipowekewa dawa vizuri ya kusafisha upo uwezekano wa watumiaji kunywa dawa na kilimo zilizotoririkia majini.Aliongeza kuwa hali ya maji katika Bwawa hilo sio nzuri na endapo wavamizi hao wasipodhibitiwa upo uwezekano mkubwa wa wakazi wa Manispaa ya Tabora kukabiliwa na upungufu wa maji katika miezi ijayo.

Mkuu wa Wilaya huyo aliwaonya wavamizi hao kutorudi tena katika eneo hilo kwani atakayekamatwa hatua kali zitachukuliwa dhidi yake.Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya alisikitishwa na kitendo cha baadhi ya watu kuvijisha siri ambayo ilipelekea wavamizi hao wakimbie kabla ya kutiwa nguvuni.

Alisema wakati watakapotaka kuendesha zoezi la pili itabidi aende kwa kushitukiza bila kupanga kwa zoezi hilo kwa muda mrefu.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Manispaa ya Tabora(TUWASA) Christopher Shinyanza alisema kuwa mavamizi hao wamesababishia kina cha maji kimepungua na kusababisha gharama uzalishaji wa ili yamfikie mtumiaji yakiwa safi bila kuwa na tope lilitokana na kilimo kando kando ya bwawa hilo.

Aliongeza kuwa shughuli za kilimo katika vyanzo vya maji vya bwawa hilo zimesababisha kupungua uzalishaji wa maji kwa ajili ya matumizi kwa wakazi wa Manispaa ya Tabora hasa kipindi hiki cha kiangazi ukilinganisha na kipindi cha masika.

Bwana Shinyanzi Alisema kuwa wakati wa masika kwa sababu ya kupata mvua kuwepo waliweza kuzalisha wastani mita za ujazo 16,500 ambazo kwa kiasi kikubwa yalikuwa yakitosha , lakini kwa hivi sasa kutokana na kuongezeka kwa shughuli za kilimo katika Bwawa hilo , hivi sasa wanazalisha mita za ujazo 11,000.

Alisema kuwa wamekuwa wakipita mara kwa mara lakini bado kumekuwepo na tatizo hilo la wavamizi kuendelea kuendesha kilimo hicho na kuathiri upatikanaji wa maji ya kutosha.

Kaimu Mkurugenzi huyo Mtendaji wa TUWASA alitoa wito kwa wananchi wenye mapenzi mema kuwafichua watu wanaoendesha kilimo katika eneo hilo kwa sababu kitendo cha kuendelea kuwaficha kinasababisha athari kwa wakazi wengi wa Manispaa ya Tabora kwa faida ya wachache.

Mwisho wa wiki Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw. Aggrey Mwanri alikiwahotubia wananchi katika eneo la Soko Kuu aliwatahadharisha wananchi uwezekano wa Bwawa la Igombe kukauka kutokana shughuli za uharibifu wa mazingira ambazo ni ukataji miti ovyo ,uchomaji moto, kilimo cha kuhama hama na idadi kubwa ya mifugo katika vyanzo vya maji.
 Mkuu wa Wilaya ya Tabora Mwalimu Queen Mlozi (aliyeshika miche ya nyanya) akiongoza Kamati ya Ulinzi na Usalama wilayani humo kung’oa na kuwaondoa wakulima wa bustani walivamia kando kando ya Bwawa la Igombe na kusababisha uharibifu wa vyanzo vya maji vya Bwawa hilo. Zoezi hilo lilifanyika jana katika eneo la Bwawa hilo. 
Mkuu wa Wilaya ya Tabora Mwalimu Queen Mlozi (wa kwanza kushoto) akiongoza Kamati ya Ulinzi na Usalama wilayani humo kung’oa na kuwaondoa wakulima wa bustani walivamia kando kando ya Bwawa la Igombe na kusababisha uharibifu wa vyanzo vya maji vya Bwawa hilo. Zoezi hilo lilifanyika jana katika eneo la Bwawa hilo.
Picha na Tiganya Vincent-RS  - Tabora

No comments: