Sunday, June 18, 2017

WARIOBA :Msaidieni Rais tushinde Vita ya Rasilimali za nchi, Suala la Makinikia sio la Chama wala Siasa ni la Watanzania wote

Na Judith Mhina .


Wananchi hawahitaji mgawanyiko wa uongozi na malumbano wanataka maendeleo.Msaidieni Rais tushinde Vita ya Rasilimali za nchi
Suala la Makinikia sio la Chama wala Siasa ni la Watanzania wote

Hivi karibuni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli alipokea ripoti ya Kamati ya kwanza na ya pili ya uchunguzi wa makontena 277 ya mchanga wa madini (makinikia) yaliyokuwa njiani kusafirishwa nje ya nchi na uchunguzi ulifanyika na kulibaini ndani ya mchanga huo kuna dhahabu na madini mengine kwa asilimia kubwa.

Aidha, Mhe Rais amechukua hatua mbalimbali kulingana na ushauri wa kamati husika, pamoja na maamuzi yake kama Rais. Kutokana na sakata la hilo, Idara ya Habari-MAELEZO imepata fursa ya kufanya mahojiano na Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mstaafu Mheshimiwa, Jaji Joseph Sinde Warioba katika ofisi zake zilizopo Osterbay Jijini Dar-es-salaam.

SWALI: Ninanukuu maneno ya Baba wa Tafa, Hayati Mwl Julius Kambarage Nyerere kuhusu raslimali za nchi na hususan madini alisema: “Madini yetu tuliyonayo ni vema kuyaacha mpaka Watanzania watakapokuwa na ufahamu wa kutosha wataamua kuyachimba” mwisho wa kunukuu nini maana yake?

JIBU: Mara baada ya Uhuru wa Tanganyika mwaka 1961 Hayati, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alipokea nchi kama Waziri Mkuu wa kwanza wa Tanganyika huru akiwa hana wataalamu zaidi ya madaktari 2 na yeye mwenyewe ambaye alikuwa msomi kutoka chuo Kikuu cha Edinburg Uingereza. Kwa hali hiyo, Mwalimu alikuwa sahihi usingeweza kuruhusu rasilimali za nchi mfano madini kuchibwa na wageni kutoka nje maana yake Watanganyika wangekuwa watazamaji tu bila kufaidika na lolote.

Mwalimu alihakikisha anawekeza katika elimu ambayo ilikuwa bure kuanzia msingi hadi chuo kikuu elimu ndio msingi wa kuondoa Ujinga Umasikini na Maradhi. Alitambua Watanganyika wakielimika na kupata utaalamu wa madini ikiwani pamoja na uchimbaji watakuja kuyachimba na kufaidika.

SWALI:Tanzania ni kati ya nchi zilizobarikiwa kuwa na raslimali nyingi za kila aina kuanzia madini, gesi, wanyamapori na hifadhi, misitu, milima, maporomoko ya maji, mabonde maziwa makubwa kwa madogo, bahari ya hindi na raslimali za mazao ya uvuvi, nchi yenye ardhi ya kutosha watanzania wenye uwezo wa kufanyakazi kwa ufanisi . Unadhani nini tatizo letu, nini cha kufanya?

JIBU Sioni kama kuna tatizo la msingi lakini, ni suala la uelewa mara nyingi kuna watu ambao huamini viongozi wao kwa kila kitu wanachosema. Lazima  wananchi wawe makini kwa sababu tatizo la watanzania ni maendeleo kila mwananchi ana kiu ya kutaka tufikie mahala pazuri kama Taifa na mimi nakubaliana nao kabisa.

Tuna rasilimali nyingi, ambazo kimsingi tukiweza kuzishughulikia kwa makini kama lilivyoshughulikiwa suala la mchanga wa madini tutakuwa mbali sana kiuchumi.

Mosi, tuangalie rasilimali ya madini kwa mapana yake na kushughulikia wawekezaji wa ndani na wale wa nje, Barick na Acaccia ni sehemu ndogo sana ya madini, tuangalie wachimaji wa ndani mfano Tanzanite ni aibu madini yanachibwa Manyara biashara hii inatokaje Mererani na kufanyika Nairobi na New Delhi tujiulize kwa nini sio Arusha na Dar-Es-Salam.

Pili, upande wa rasilimali za maziwa makubwa tuliyonayo Victoria, Tanganyika na Nyasa, Bahari ya Hindi kuanzia Moa mpaka Tanga kwa kiasi gani tumeweza kutumia rasilimali za bahari maharamia wanakuja na meli zao wanavuna tu na kuwatajirisha watu wengine. Mfano ziwa Victoria linategemewa na wananchi wengi na sasa samaki hamna wamekwisha kwa sababu hatusimamii rasilimali zetu ipasavyo. Maana suala sio kuvuna tu tunalindaje hizi rasilimali zetu ili ziwepo leo kesho na vizazi vijavyo.

Tatu, Maliasili zetu za wanayamapori, mbuga za wanyama, vitalu vya utalii unampaje mfanyabiashara kibali cha kuwinda miaka 99 yaani atumie yeye, wanawe na wajukuu zake, watanzania watatumia lini, haya ni masuala ya msingi kabisa ya kuangalia upya.

Nne, Ardhi Mwalimu alisema ili tuendelee tunahitaji vitu vine Watu, Ardhi Siasa Safi na Uongozi Bora. Mwalimu Nyerere aliona ardhi ndio kilakitu hivyo vyote tulivyovitaja vipo ardhini pamoja na sisi wanadamu tunaitegemea kwa kila kitu. Maeneo mengi yaliyotumiwa na watu kwa shughuli za ufugaji aidha , yana matumizi mengine kama nyumba, kilimo cha mashamba makubwa, na idadi ya watu inaongezeka ardhi ni ileile hii imesababisha migogoro ya watumiaji wa asili wa maeneo hayo na wenye matumizi mengine tunatatuaje changamoto hii.

SWALI: Kwa kuwa umebobea katika masuala ya mikataba na sheria, ushauri gani unautoa katika masuala yote ya raslimali za Tanzania? Nani anatakiwa kusimamia raslimali hizi kwa ufanisi?

JIBU: Hii sio suala la mjua sheria au asiyejua, Mwanasheria lazima anazijua sheria ndio maana amepewa dhamana. Linalojitokeza ni ukosefu wa maadili ya uongozi, imani, utiii, uwazi na kutopenda nchi yako na Watanzania ambao wamekupa dhamana ya kusimamia jambo.

Ndio maana Mwalimu Nyerere aliweka miiko ya uongozi, maadili ya uongozi kwenye Azimio la Arusha. Kila mwananchi alikuwa anaweza kujua kiongozi huyu muadilifu au sio muadilifu na anachukuliwa hatua kabla mambo hayajaharibika.

Lakini sio vema kumhukumu mtu kwa jambo lolote lile, ni vema busara itumike kujua kilichotokea mfano hili suala la mchanga wa madini ya makinikia.

Jambo la msingi ni kutafuta suluhu itakayotupeleka mbele, tuone sera zetu zikoje na zinatusaidiaje kulinda rasilimali za Taifa, tunarekebisha vipi kuondoa tatizo, sheria na utendaji kwa ujumla. Naomba watanzania tutoe maoni na mawazo yatakayoboresha sera, sheria na utendaji au usimamizi wa rasilimali husika. Tunaweza kurudisha miiko na maadili ya uongozi katika kusimamia rasilimali za nchi, kila Mtanzania ajue sio mali yake ni ya Watanzania wote lazima aitunze vinginevyo atahukumiwa kwa hilo.

SWALI: Ni ukweli usiopingika kuwa kosa limeshafanyika kwa hili tuliloliona la mchanga wenye madini ya dhahabu, ambapo mhusika ambaye ni mmiliki wa Kampuni inayobeba mchanga huo tangu 1998 hadi 2017 amewasili nchini kuonana na viongozi wakuu wa serikali, nini maoni yako kuhusu hili?

JIBU Sisi hatukushughulika na uchimbaji wa madini, lakini utafiti tulifanya na kujua madini yapo na kuna maeneo mengi ambayo tumeweza kufanya vizuri tunapata mapato, lakini hatukupata mapato yote.

Lakini hili la mchanga sitaki kulizungumzia sana nadhani watu wanalichukulia kwa mihemko sioni faida kuzungumzia matukio badala ya kuona tafsiri nzima nini cha kufanya.

Ninachokiona na cha muhimu sana, Watanzania wamepata faida kwa mara ya kwanza tumeweza kujua mikataba ya madini ikipitiwa na Kamati zote mbili zimetueleza maeneo yote ya mikataba waliyopitia na kuja na mapendekezo. Tumetambua serikali ilikuwa na hisa au la mrahaba asilimia ngapi, kodi kiasi gani, na mambo kama hayo.

Naomba jambo hili lisibague, tunasema hatupati mapato ya kutosha ni lazima tujue kwa wachimbaji wa nje na wa ndani mfano nani anajua wachimbaji wadogo wadogo wamechimba madini kiasi gani tangu 1998 hadi 2017 na kodi kiasi gani imeimngia. Tumepata nafasi sasa ya kuangalia sera za kulinda rasilimali ya madini na nyingine zote katika nchi, kama maliasili ya bahari tunaitumiaje, gesi, makaa ya mawe, chuma, wanyama pori na mambo kama hayo.

Hii imetufungua macho sera ya aina gani sheria za aina gani, jinsi gani ya kutunza na kutumia rasilimali hizi tulizopewa na mungu.

SWALI: Kwa kuwa wananchi tulio wengi tunaenda kwa mihemko bila kupambanua hoja husika na kutoa mapendekezo au maoni yatakayo isaidia serikali kuboresha sera sheria na utendaji wa rasilimali zetu unadhani tatizo ni nini?

JIBU: Hatujaona uongozi wa Kitaifa katika hili suala la mchanga wa makinikia ninachokiona mimi ni uongozi wa chama na siasa nyingi, sio sahihi kabisa wanafanya makosa hili ni suala la rasilimali za nchi ni la kila Mtanzania.

Viongozi hawawatendei haki wananchi wanaowakilisha, wanakuwa na mihemko wanasema kamata, shitaki, wafunge. masuala ya kitaifa hayaendi hivyo sisi sio Polisi wala Mahakama waachieni wenye kazi yao.

Uongozi wa kulalamika hautusaidii, wananchi wanataka kuona rasilimali zetu zinanufaisha na kuboresha huduma za jamii ambazo wanalalamika kila leo hakuna dawa, elimu isiyowajenga vijana na mambo kama hayo.

SWALI: Mhe. Kutokana na sakata la mchanga wa dhahabu uliokuwa unasafirishwa nje ya nchi na matokeo yake watanzania tunajifunza nini kwa maoni yako?

JIBU: Kabla ya tuona funzo tulilopata nadhani ni vema nikazungumzia jambo hili, nimeona mjadala katika mitandao ya kijamii ambayo inafanywa kwa mihemko. Ukiangalia vyombo vya habari au viongozi tumejikita katika majina ya watu, nilikuwa nnaangalia Bunge wote wanakwenda kwa wale waliotajwa unakuta kuna wanaochangia na wanaolaumu ama unsahangilia au unalalamika kuhusu watu.

Kubwa ni utaratibu tulionao haitasaidia kulalamika juu ya watu waliofanya kazi huko nyuma, tunaweza kuwauliza wahusika nini kilitokea mpaka kufanya hivyo, lakini hilo sio kubwa, muhimu ni kutafuta ufumbuzi.

Mjadala huu umenikumbusha Awamu ya kwanza ya Mwalimu Nyerere viongozi wote na wananchi walikuwa wanalalamika kila kitu wanachokikosa ni kwa sababu ya wakoloni. Mwalimu akasema namnukuu: “Ni kweli wakoloni wametuleta matatizo mengi sana lakini haitoshi kulaumu wakoloni bila kuondoa mateso ya wananchi”. Mwalimu akaja na Waraka ambao ulikuwa unaitwa “Act dont Argue” nadhani bado upo.

Waziri wa Katiba na Sheria Profesa Palamagamba Kabudi nanukuu amesema. “Napenda kupata maoni tufanye nini kuhusu suala hili la mchanga wa dhahabu (makinikia).” Namuunga mkono, sasa tumepata nafasi ya kutoa maoni, mawazo ambayo ni muhimu sana maoni ya wadau katika uundaji wa sera na sheria

Sasa hivi siamini kama hatuna utaalamu, nina hakika tunao wa kutosha tatizo ni maadili na hilo lazima kutafuta ufumbuzi wake, pia tuunge mkono serikali inachofanya kupambana na rushwa na ufisadi.

“Lakini tusijidanganye bishara ya madini, mafuta ina changamoto kubwa sana duniani hususan Afrika, maana unapambana na watu wenye fedha biashara hii popote utakapo kwenda, ambapo uchumi unategemea mafuta na madini utaona jinsi wakubwa wanavyooneemeka na rasilimali hizo na kuwaaacha wananchi wakiwa masikini mfano mzuri Nigeria”.

Pamoja na kuangalia maadili na nidhamu lazima kuwe na uwazi katika mikataba ni muhimu sana.

SWALI: Una maoni na mapendekezo yako kwa viongozi wote na Mhe Rais katika kumuunga mkono?

Kwanza naliona hili la malumbano yatatugawa, waache tofauti zao hii lawama ya madini ingekuwa ni mwanzo kwa kuleta mawazo na maoni ya kutengeneza nchi yetu katika kulinda na kuzitumia rasilimali zote kwa maendeleo ya taifa letu.

Viongozi msaidieni Rais kulishughulikia kwa pamoja hili si jambo la chama wala Taasisi. Hakuna haja ya kupeana lawama ukishasema tumekosea unatakiwa ueleze tufanye nini, sio kusema serikali ichukue hatua kwani serikali ni nani si mimi na wewe sasa kwa nini hutaki wewe kulitolea maoni?

Tujiamini nimeona katika malumbano hayo, wengine wanaonekana kama hatujiami kama tukifanya hivi tunaweza kushitakiwa, mabadiliko yoyote yana machungu yake. Tusije tukapoteza imani tuliyonayo maana tunaweza tukapoteza mapato yetu lakini ni lazima tufanye kwa kujenga afya ya rasilimali zetu.

Rais amekutana na mmiliki wa Barick na kila upande una msimamo wake, tuiachie serikali na nina imani kabisa serikali itafanikiwa. Kinachonishangaza ni mazungumzo ya baadhi ya viongozi kuwa serikali ihakikishe tunapata hizo fedha walizo taja kwenye taarifa.

Nadhani hii sio sahihi, tuna imani na Viongozi wet wakuu haswa Rais, lolote litakaloafikiwa tulipokee na kulikubali tusije kuanza kulumbana ripoti imesema trilioni 108 ziko wapi? Pia nilisemee hili la dalili za kupoteza imani, eti tukifanya hivyo tutashitakiwa, sababu ya mikataba na wawekezaji hawatakuja mimi naamini watakuja tu rasilimali zipo kwetu hawana jinsi.

SWALI: Msaada wako binafsi kwa Rais au maoni yako kwa Rais

JIBU: Sisi tupo, Uongozi ni suala la kupeana vijiti mimi natoka Mara nimepitia utamaduni wa kabila langu kwa utamaduni wetu unafika mahali unangatuka watu wanadhani kungatuka ni kustaafu hapana sio sahihi. Ukitoka jandoni mzee wako lazima angatuke maana umekuwa sehemu ya jeshi la kabila na yeyote ambaye kijana wake yuko kwenye jeshi yeye anatoka.

Wazee hawaingii katika mambo ya vijana na sisi tupo lakini hatutaki kuingilia utendaji wao kama sisi tulivyoachiwa kuendesha nchi, ila Rais akituhitaji tupo tayari kwa ajili ya ushauri anaweza kuukubali au kuukataa. Nataka nimhakikishie kwa hili tupo pamoja na tutatoa maoni ya kurutubisha Sera, Sheria na Utendaji katika rasilimali za nchi hii.

No comments: