Tuesday, June 6, 2017

VIJANA WATOA SIRI KUFICHUA MITANDAO YA UHALIFU NCHINI

TAA 2
Na Jonas Kamaleki-MAELEZO.

Zaidi ya vijana wapatao  1230  wametoa siri nzito kwa  Maaskofu na Mashekhe  kutoka katika Kamati ya Kitaifa ya Maadili , Amani na Haki za Binadamu kwa Jamii ya Madhehebu ya Dini  Nchini  kufichua mtandao  haramu  wa watu  wanaoendesha mauaji na uhalifu mwingine kwenye   mikoa  13, nchini kama njia muhimu ya kumpongeza IGP mpya, Saimoni Sirro.

 Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Askofu William Mwamalanga, siri hiyo imetolewa  jana  na vijana hao katika   siku ya  tatu  mkutano wa kujenga maadili kwa vijana unao fanyika Mbagala, jijini Dar es Salaam na kuwashirikisha   vijana  wa madhehebu mbalimbali ya dini  kutoka katika  mikoa ya Pwani, Tanga, Lindi,  Morogoro,Dar es Salaam  ambapo wameyataja maeneo ya Mkuranga, Rufiji  Kigamboni, Kibiti, Msata, Tanga mjini, Pemba na Unguja kuwa maeneo hatari yanayowajengea vijana imani za  kigaidi.

 Aidha, Askofu Mwamalanga alisema kuwa vijana 147  wa kiislamu wanaohudhuria mkutano huo  wamewataja  baadhi ya watu  ambao ni   hatari  na wamekuwa wakieneza elimu ya mauaji  kwenye  misikiti mbali mbali nchini kwa kuiita Serikali ya Awamu ya Tano jina la katili na kwamba elimu hiyo imesambazwa kwa kasi  katika mikoa ya  Kagera, Tanga, Mwanza, Arusha, Pemba, Unguja, Dar es Salaam, Lindi, Mtwara, Morogoro, Iringa, Singida, Dodoma, Pwani na Kigoma huku vikosi vya vijana vikiandaliwa kufanya mauaji  mara baada ya mufungo mtukufu wa Ramadhani kama yale ambayo yamekuwa yakifanywa  Mukuranga, Kibiti  na Rufiji. 

Vijana hao wanamuomba  IGP  Sirro kuwachukulia hatua kali maafisa wa jeshi hilo ambao wanatumia jeshi kupandikiza Umngiki, na  kwamba wana imani na IGP Sirro amabaye kwa mujibu wa hao vijana hatamwangusha Rais  Magufuli na watanzania kwa ujumla.

Akifunga  Mkutano huo  Askofu Mwamalanga  amemtaja IGP  Sirro kama polisi mahiri wa maadili na jemadali  mweledi wa mapambano hivyo amewataka  vijana kote nchini kumuunga mkono kwa kuwafichua polisi wote wanaoenzi uhalifu. “Tusipofanya hivyo tutakuwa  kama  pipa zuri  tunalo jaza maji wakati tukijua chini limetoboka”,alisema Askofu Mwamalanga na kuongeza kuwa raia wema ni asilimia 99.9  wahalifu ni 0.1   hii ina maana kuwa ukiondoa polisi wahalifu  ndani ya jeshi hilo wahalifu ni wachache mno  mitaani  watayeyuka wenyewe. 

Aidha,  Askofu huyo amewahimiza vijana na viongozi wa dini kushiriki kwenye mafunzo hayo kote nchini ili  wapewe ufahamu wa elimu ya maadili ya kweli  ili wawe walinzi wa taifa na kupenda amani  na kuweka uchu wa kuchukia rushwa  na kujiwekea  mitazamo ya kupenda kazi za baraka.

Kiongozi huyo wa dini amekemea vikali nyumba za ibada   kugeuzwa  eneo la mafunzo ya uhalifu kwani ni aibu kwa msikiti au kanisa kufanya  mafunzo ya kigaidi  ndani  ya  nyumba  za ibada  kufanya hivyo ni ibada ya sanamu, watu wa jinsi hiyo hawana uhusiano wowote na Mwenyenzi MUNGU ambaye kusudi lake ni kuondoa uovu kwa mwanadamu.

Hivi karibuni yametokea mauaji ya viongozi wa Chama Tawala maeneo ya Kibiti, Mukuranga na Rufiji na kufanya wakazi wa maeneo hayo kuishi kwa wasiwasi na mashaka juu ya maisha yao. Wakati akiipishwa kuwa IGP, Kamanda Simon Sirro alisema kupambana na kuondoa uhalifu kwa kushirikiana na raia wema ni moja ya vipaumbele vyake.

No comments: