Wednesday, June 7, 2017

UCHAMBUZI KIVUKO CHA MV KAZI: JPM aliahidi, anatekeleza

Na Benjamin Sawe.

Upo usemi wa wahenga usemao “mnyonge mnyongeni ila haki yake mpeni.” Hivi ndivyo ninavyoweza kusema kuhusiana na harakati za Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli katika kuhakikisha kuwa Sekta ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi inaimarika.

Dkt. John Pombe Magufuli kabla ya kuteuliwa kuwa Rais, amekuwa Waziri katika Awamu mbili zilizopita. Anao uzoefu mkubwa wa utendaji kazi lakini pia katika kuongoza Wizara ambapo amewahi kuwa  Waziri wa Ujenzi na Miundombinu na Kilimo na Ufugaji. 
Kutokana na umuhimu wa Sekta ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi katika maendeleo ya Taifa, mara tu baada ya kuchaguliwa kuwa Rais, aliagiza ujenzi wa barabara ya kutoka Mwenge hadi Moroco ambayo ilikuwa ina msongamano mkubwa wa magari kuelekea katikati ya jiji.

Msongamano huo umekuwa ukiathiri malengo ya Wafanyakazi ambao walikuwa wakitumia muda mwingi wakiwa kwenye foleni na hivyo kupunguza muda wa kufanya kazi lakini pia uzalishaji na utoaji huduma za msingi kwa Taifa.

Aidha, Mheshimiwa Rais ameshiriki uwekaji wa jiwe la msingi kwenye mradi wa ujenzi wa barabara za juu (fly over) katika makutano ya barabara ya Nyerere na Mandela eneo la Tazara unaogharimu kiasi cha shilingi bilioni 100 za Kitanzania na pia ujenzi wa barabara za juu kwenye makutano ya barabara za Morogoro, Mandela na Sam Nujoma eneo la Ubungo Jijini Dar es Salaam
Hivi karibuni Serikali kupitia Waziri Mwenye dhamana ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa amepokea Kivuko cha MV Kazi ambacho kimejengwa na Kampuni ya Kizalendo ya M/S Songoro Marine Transport Boatyard ya Mwanza.

Kivuko hicho kilichogharimu jumla ya Shilingi bilioni 7.3 za Kitanzania, ni moja ya ahadi ya Mheshimiwa Rais John Magufuli alizozitoa wakati wa Kampeni zake za Urais za kuwapunguzia kero za usafiri Wananchi wakiwemo wakazi wa Kigamboni.

Akipokea Kivuko hicho chenye uwezo wa kubeba abiria 800 na  magari 22 Prof. Mbarawa amesema lengo la Serikali ni kuboresha huduma za kusafirisha abiria na magari kati ya Magogoni na Kigamboni ambapo kwa muda mrefu kimekuwa kilio cha Wananchi waishio kigamboni. 

Kabla ya ujio wa kivuko hicho kipya kumekuwa na jitihada zizolikuwa zinafanywa na Serikali katika kutatua tatizo la usafiri kwa Wananchi wa Kigamboni kwa njia ya Pantoni.
 Moja ya jihihada katika kukabiliana na tatizo hilo ni ujenzi wa Kivuko cha MV Magogoni chenye uwezo wa kubeba abiria 2000 na magari 60 kwa pamoja sawa na Tani 500.

Profesa Mbarawa amesema Kivuko cha MV Kazi kinakwenda kuimarisha usafiri kwa Wakazi wa Kigamboni ambapo kwa sasa kutakuwa na jumla ya Vivuko vitatu kikiwemo pia kivuko cha…..
Aidha, uzinduzi wa daraja la Kigamboni ni moja ya mafanikio makubwa ambayo yanafanywa na Serikali ya Awamu ya Tano inayotekeleza Ilani yake ya Chama Tawala cha CCM.

Daraja hilo licha ya kuunganisha wananchi wa Kigamboni lakini pia linaunganisha watu wote ikiwa ni pamoja na kuleta maendeleo nchini hasa kwa wakazi wa Kigamboni.

Daraja la Kigamboni lenye urefu wa mita 680 linaunganisha upande wa Kurasini na Kigamboni wenye urefu wa Kilometa 2.5. Ujenzi wa daraja hilo umefanywa na Kampuni ya China Railway 15 Group ikishirikiana na Kampuni ya China Bridge Engineering Group na umegharimu zaidi ya shilingi bilioni 250 za Kitanzania.

Kwa maoini yangu, utendaji wa jinsi hii unatoa taswira ya uwajibikaji mahsusi unaopaswa kufanywa na viongozi wa Kisiasa ukihusisha usimamizi na ufuatiliaji yakinifu wa Sera/michakato/mikakati na mipango ya serikali.

Usimamizi na ufuatiliaji unaofanywa na Prof. Mbarawa uwe chachu kwa Viongozi wengine wa Serikali na Wanasiasa waliopewa dhamana katika awamu ya Tano. Si jambo geni kumsikia  Prof. Mbalawa kwa siku moja akiwa katika mikoa miwili tofauti akifuatilia utekelezaji wa ahadi za Serikali ya Awamu ya Tano. 

Wapo watu wanaoweza kubeza uwajibikaji wa Waziri huyu lakini kimsingi anachofanya ni kuhakikisha kuwa Wananchi wanapata huduma ya msingi katika kuwaletea maendeleo yao na Taifa kwa jumla. Ndio maana nimesema kuwa “mnyonge mnyongeni ila haki yake mpeni.”

No comments: