Monday, June 12, 2017

UCHAGUZI MKUU WA TFF AUGUST 12,2017 DODOMA, SIFA ZA MGOMBEA ZAWEKWA WAZI

Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Tanzania (TFF), imetangaza Uchaguzi Mkuu wa shirikisho hilo utakafanyika Agosti 12, mwaka huu mjini Dodoma.

“Napenda kuwatangazia wadau wote wa mpira wa miguu kuwa mnakaribishwa kugombea nafasi zilizo orodheshwa hapo chini kwa kuchukua fomu Ofisi za TFF Karume Ilala na pia unaweza kuzipata katika tovuti ya TFF: www.tff.or.tz,” amesema Kuuli.

Akitangaza tarehe hiyo mbele ya wanahabari, Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi wa TFF, Wakili Revocatus Kuuli, amesema kwamba kamati yake haitakuwa na huruma kwa ishara yoyote ya rushwa katika kipindi chote cha uchaguzi.

 Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi wa TFF, Wakili Revocatus Kuuli (Katikati) akiwa pamoja na wajumbe wengine wa kamati hiyo.

Wakili Kuuli amesema kamati yake itandesha uchaguzi huo kwa Uhuru na Haki na kuzingatia taratibu, kanuni na sheria zote zilizopo.

Kuuli, amesema Kamati yake itafanya kazi na Taasisi nyingine za Serikali ikiwemo Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na jeshi la Polisi kuhakikisha uchaguzi huo hautakuwa na vitendo vya rushwa.

“Tunawatahadharisha wagombea woye kukaa mbali na vitendo vya rushwa…, kamati yetu haitakubali vitendo hivyo na tutafanya kazi na mamlaka za Serikali kuhakikisha yeyote atakayehusika na vitendo hivi anachukuliwa hatua, Takukuru wataufuatilia kwa karibu uchaguzi huu,” alisema Kuuli.

Akizungumzia mchakato mzima, Kuuli anasema, mchakato wa kuchukua fomu na kuzirejesha ni Juni 16 mpaka 20, mwaka huu na kikao cha mchujo wa awali kwa wagombea kitafanyika Juni 21 mkapa Juni 23.

Juni 24 na 25, mwaka huu, kamati itafanya kazi ya kuchapisha na kubandika kwenye mbao za matangazo majina ya wagombea wakati Juni 26-28 zitakuwa siku za kupokea na kuweka mapingamizi kwa wagombea na Juni 29 mpaka Julai Mosi itakuwa kipindi cha kupitia mapingamizi yote na kufanya usaili.

Kwa mujibu wa Kuuli, Julai 2-3 kitakuwa kipindi cha kuchapisha na kubandika matokeo ya usaili, Julai 4-7 na kipindi cha Sektretarieti kuwasilisha masuala ya Kimaadili kwenye Kamati ya maadili, Julai 7-11 ni kipindi cha kusikiliza na kutolea maamuzi masuala ya kimaadili.

Julai 15-17 kitakuwa kipindi cha kukataa Rufaa kwa maamuzi ya masuala ya kimaadili kwenye kamati ya rufaa ya Maadili ya TFF, Julai 18-22 itakuwa siku ya kusikiliza rufaa za maadili na Julai 23 mpaka Julai 25 itakuwa siku ya kutoa maamuzi ya Rufaa, Julai 26-28 kitakuwa kipindi cha kukata rufaa dhidi ya kamati ya Uchaguzi kwenye Kamati ya Rufaa ya Uchaguzi ya TFF, rufaa hizo zitasikilizwa Julai 29 mpaka Agosti 2.

Wagombea watajulishwa matokeo ya Kamati ya Uchaguzi ya TFF na Agosti 5-6 itakuwa siku ya kuchapisha majina ya wagombea watakaoingia kwenye Uchaguzi huo na kampeni kwa wagombea zitaanza Agosti 7 mpaka 11 na siku inayofuata yaani Agosti 12 itakuwa siku ya uchaguzi wa viongozi wa TFF.

Nafasi zinazogombewa ni Rais wa TFF, Makamu wa Rais pamoja na nafasi 13 za wajumbe TFF wanaowakilisha kanda 13 za Kagera na Geita;

Mara na Mwanza, Shinyanga na Simiyu, Arusha na Manyara, Kigoma na Tabora, Katavi na Rukwa, Mbeya na Iringa, Njombe na Ruvuma,Lindi na Mtwara, Dodoma na Singida,Pwani na Morogoro, Kilimanjaro na Tanga na Dar es Salaam ambayo ni kanda pekee.


SIFA ZA WAGOMBEA.

1. Awe raia wa Tanzania.
2. Awe na kiwango cha elimu kisichopungua kidato cha nne (Cheti cha Elimu ya Sekondari).
3. Awe na uzoefu wa uendeshaji Mpira wa Miguu uliothibitishwa wa angalau miaka mitano.
4. Asiwe na hatia yoyote ya kosa la jinai na asiwe amewahi kuhukumiwa kifungo kisicho na mbadala wa faini.
5. Awe na umri angalau miaka 25.
6. Awe amewahi kuwa ama Mchezaji Mpira wa Miguu, Kocha, Mwamuzi. Au kushiriki katika uendeshaji wa Mpira wa Miguu angalau katika ngazi ya Mkoa au ngazi ya daraja la kwanza.
7. Awe muadilifu na muaminifu mwenye uwezo wa utendaji katika utekelezaji na utimizaji wa majukumu na malengo ya TFF.
8. anayegombea nafasi ya Rais au makamu wa Rais awe na kiwango cha elimu kisichopungua shahada moja, mwenye utu na uwezo wa kuiwakilisha TFF ndani na nje ya nchi.


Mwisho wa kuchukua na kurudisha fomu ni tarehe 16-20/06/2017 saa kumi (10:00) jioni.

No comments: