Wednesday, June 21, 2017

TPSC YAANZISHA MAFUNZO YA SHAHADA YA UHAZILI NA UTUNZAJI KUMBUKUMBU,TAARIFA NA NYARAKA

Chuo Cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kwa mara ya kwanza kimeanzisha Masomo ya Shahada ya kwanza (Degree) katika fani za Uhazili na Utunzaji wa Kumbukumbu, Taarifa na Nyaraka.

Kufuatia kuanzishwa kwa masomo ya Shahada ya kwanza katika Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, Mkuu wa Chuo Dkt. Henry Mambo ametoa wito kwa watumishi wa umma na Watanzania wenye sifa kuchangamkia nafasi hizo za masomo kwa manufaa yao binafsi na Taifa kwa ujumla.

Dkt. Mambo alisema masomo hayo ya Shahada ya kwanza yataanza Mwezi Septemba,2017 katika Matawi ya Dar es Salaam na Tabora, nayo ni hatua kubwa kwa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania katika kuwaendeleza Watumishi na Watanzania Kitaaluma.

Kwa upande wa sifa za kujiunga na masomo hayo ya shahada ya kwanza, Dkt. Mambo alisema muombaji anatakiwa kuwa na elimu ya kidato cha sita pamoja na ufaulu katika masomo mawili au Diploma katika fani husika yenye ufaulu au GPA alama 3.

Mkuu wa Chuo pia aliendelea kufafanua kwamba Masomo hayo ya ngazi ya Shahada yameanzishwa ili kuhakikisha kwamba watumishi wa umma na Watanzania wenye sifa za kujiunga wanakabiliana na changamoto zinazojitokeza katika soko la ajira kufuatia mabadiliko ya teknolojia na mifumo mbalimbali ya utendaji kazi.“Kutokana na mabadiliko hayo ni vema Watumishi wa Umma na Watanzania wenye sifa kwa ujumla nao wakapata mafunzo ambayo yatawawezesha kukabiliana na changamoto mbalimbali katika soko la ajira,”.

Kuhusu shahada ya Uhazili na Utawala, Mkuu wa Chuo alisisitiza kwamba Wahitimu wataweza kukabiliana na changamoto mbalimbali za mawasiliano  katika utendaji wao wa kazi wa kila siku na hivyo kuwawezesha kufanya kazi kwa ufasaha katika sekta ya umma na hata sekta binafsi. “Mafunzo hayo pia yatawawezesha wahitimu kumudu nafasi ya Maofisa Wasaidizi Waandamizi ambao watafanya kazi katika taasisi mbalimbali hapa nchini na hata nje ya nchi kulingana na soko la ajira litakavyowahitaji” alisema.

Kuhusu Shahada ya Utunzaji Kukumbukumbu, Taarifa na Nyaraka, Mkuu wa Chuo cha Utumishi alibainisha kwamba mafunzo hayo yatawawezesha wahitimu kutekeleza majukumu yao kwa ufasaha mkubwa zaidi katika eneo hilo na hivyo kuchangia katika uendelezaji na ukuaji wa Taaluma ya Utunzaji Kukumbukumbu, Taarifa na Nyaraka. 

Mafunzo ya ngazi ya shahada (Degree) yatatolewa kwa muda wa miaka mitatu, wakati yale ya Diploma na Cheti yataendelea kutolewa kwa kipindi cha miaka miwili na mwaka mmoja kama kawaida na akatoa wito kwa watumishi wa umma na watu wote wenye sifa za kujiunga na masomo hayo kuchangamkia fursa hizo kwa kujaza fomu za kujiunga na Chuo zinazopatikana katika matawi yote ya Chuo cha Utumishi wa Umma ya Dar es Salaam, Tabora, Singida,Mtwara, Tanga na Mbeya, na katika tovuti ya Chuo www.tpsc.go.tz

Katika kongamano la Mkutano Mkuu wa mwaka wa Chama Cha Makatibu Mahsusi Tanzania (TAPSEA) lililofanyika hivi karibuni Mkoani Dododma, Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan wakati wa kufungua Mkutano huo, aliwataka makatibu Mahsusi hao kuichangamkia kozi hiyo, kwa kuwa ni fursa nzuri kwa Makatibu Mahsusi na itawasaidia sana katika kuongeza weledi na ufanisi kazini.

Nae Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejiment ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mh. Angellah Jasmine Kairuki, ambae pia alihudhuria Kongamano hilo na ambaye Chuo cha utumishi wa Umma kiko chini ya Wizara yake, aliwatoa hofu waombaji wa kozi hizo mpya zilizoanzishwa na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa kusema Ofisi yake inalitambua hilo na inalifanyia kazi suala hilo ili Wahitimu watakapomaliza mafunzo yao ya miaka mitatu(3), waweze kutambulika nafasi zao katika Muundo wa Utumishi wa Umma. Hivyo akawahimiza Makatibu Mahsusi na Watunza Kumbukumbu Taarifa na Nyaraka kuchangamkia nafasi hizo.

Mwandishi wa gazeti hili pia aliweza kuongea na Katibu Mkuu wa TAPSEA, Festo Melikiory ambaye alisema kuwa kuanzishwa kwa kozi hizo ni fursa kwa Watanzania hususan Makatibu Mahsusi na Watunza Kumbukumbu na kwamba ni matumaini yake kuwa kozi hizo zitaongeza weledi na ujuzi miongoni mwa watumishi wa umma na watanzania kwa jumla. “Hiki kilikuwa ni kilio chetu cha siku nyingi, sasa kimesikilizwa, ni matumaini yangu kuwa Makatibu Mahsusi wengi wataichangamkia fursa hii,”alisema.

Katibu Mkuu huyo wa TAPSEA alitoa wito kwa Makatibu Mahsusi kuichangamkia kozi hiyo kwani itaongeza uwezo wao wa utendaji wa kazi.Alisema kozi hiyo ni fursa nzuri kwa Makatibu hao kwani itawasaidia sana katika kuongeza weledi na ufanisi kazini.

Baadhi ya Watumishi wa Umma na wananchi wamekipongeza Chuo cha Utumishi wa Umma kwa kuanzisha masomo ya Shahada katika fani hizo na kusema kwamba mafunzo hayo ni hatua kubwa katika mchakato wa kuendeleza taaluma ya elimu hapa nchini. 

Pamoja na kutoa Mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi majukumu mengine ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania ni kutoa Huduma ya Shauri za Kitaaluma, Tafiti na Machapisho mbalimbali yanayohusiana na uendeshaji wa Utumishi wa Umma.

Mafunzo ya muda mfupi yanatolewa kwa Watumishi wa Umma pamoja na watumishi wa sekta binafsi ili kuwajengea uwezo katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku kwa ufanisi mkubwa zaidi.

Mafunzo yatolewayo na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania yamejikita katika maeneo ya Menejimenti, Utawala na Uongozi, Usimamizi wa Rasilimali Watu, Utunzaji wa kumbukumbu Taarifa na Nyaraka, Usimamizi wa Fedha, Uendeshaji wa Ofisi, Ununuzi na Ugavi, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano .
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe Angellah Kairuki akijadiliana jambo na Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) Dkt.Henry Mambo, katika moja ya hafla jijini Dar es Salaam hivi karibuni(Picha na Maktaba) 

No comments: