Friday, June 9, 2017

HATUA ZA KISHERIA ZITACHUKULIWA DHIDI YA UHARIBIFU WA VYANZO VYA MAJI.


NA TIGANYA VINCENT,TABORA.

SERIKALI ya mkoa wa Tabora imesema haitasita kuchukua hatua za kisheria kwa mtu yoyote atakayebainika kuendesha vitendo vya uharibifu wa ardhioevu kwa kuendesha shughuli za kibinadamu kama kilimo, ufugaji mifugo, uchomaji mkaa na uchomaji moto hovyo kwenye vyanzo vya maji na hifadhi za misitu.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri mara baada ya kushiriki kampeni ya upandaji na umwagiliaji wa miti ambalo ziliendeshwa na vijana 600 wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Msange ambao wametekeleza agizo la Makamu wa Rais kwa vitendo .

Alisema kuwa viongozi wote wanatakiwa kushirikiana na wananchi katika kuwabaini wote wanaoendesha shughuli hizo ovu katika mistu mkoani hapo kwa kuwa wanahatarisha wakazi wa Tabora na mikoa jirani.

Mkuu huyo wa Mkoa aliwashukuru vijana hao wa JKT waliomba kushiriki katika zoezi la kupanda miti kabla ya kumaliza mafunzo yao Jumamosi ili iwe alama ya uwepo wao katika eneo hilo.

Alisema kuwa kitendo walichoufanyia vijana hao kimeonyesha jinsi walifundishwa vizuri juu ya kuwa wazalendo kwa Taifa lao na kitabaki katika kumbukumbu za Mkoa huo na majina yao yataandikwa.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo Mmoja Mdau wa Mazingira na Mkurugenzi Mtendaji wa Kuja na Kushoka Bw. Leonard Kushoka alisema kuwa chanjo kikubwa cha uharibifu wa mazingira ni ukaushaji wa tumbaku kwa kutumia Mabani ya kizamani na matumizi ya mkaa wa miti kama nishati ya kupikia.

Alisema kuwa ili tumbaku iweze kukauka katika heka moja unahitaji kilo 10,000 za kuni kwa msimu mmoja kwa mabani ya kizamani wakati ya kisasa mkulima anahitaji kilo 5,000.

Bw. Kushoka alisema kuwa hali hiyo inasababisha miti mingi kukatwa kila mwaka na kuongeza iwapo mistu ya Tabora kwingineko iweze kunusurika inabidi wakulima waanze kutumia mashine maalum ambayo inatumia mkaa uliozalishwa na taka katika kuendesha zoezi la kukaushia tumbaku.

Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw. Aggrey Mwanri akizungumza na waandishi wa habari jana kabla ya kuanza zoezi la kuondoa magugu katika miti iliyopandwa katika Manispaa ya Tabora juzi.
Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw. Aggrey Mwanri akishirikiana na askari wa Kujenga Taifa(JKT) Msange wanaohitimu mafunzo yao Jumamosi wakati wa zoezi la kuondoa magugu katika miti iliyopandwa katika Manispaa ya Tabora juzi.Picha na Tiganya Vincent-RS -Tabora

No comments: