Monday, May 8, 2017

Wachimbaji wadogo waiomba Serikali kutoa elimu ya uchimbaji bora

Mchimbaji mdogo wa Madini ya Almas ambaye pia ni Mshauri Mwelekezi wa SANA Gems Gregory Kibusi, akiangalia ubora wa Madini ya Alams.

Na Asteria Muhozya, Arusha

Wachimbaji wadogo wa Madini walioshiriki Maonesho ya 6 ya Kimataifa ya Madini ya Vito, Arusha wameiomba Serikali kuendelea kutoa elimu ya uchimbaji bora na uhifadhi wa mazingira kwa wachimbaji nchini.

Ombi hilo lilitolewa na Mshauri Mwelekezi wa Kampuni ya SANA Gems, ambaye pia ni mchimbaji mdogo wa madini ya Almas, Gregory Kibusi. Kampuni ya SANA Gems inayofanya shughuli zake za uchimbaji mkoani Shinyanga ndiyo kampuni pekee ya wachimbaji wadogo iliyokuwa ikionesha madini ya Almas katika Maonesho hayo.

Kibusi aliongeza kuwa, ushiriki wa wachimbaji katika maonesho hayo ni fursa kwao ya kukutana na wanunuzi na kujenga mtandao wa kibiashara hivyo kuiomba serikali kuendelea kuwahamisha wachimbaji wadogo nchini kushiriki katika maonesho hayo kwa kuwa, yanawezesha uhakika wa masoko ya madini yao.

"Nikiwa pia kama Katibu Mkuu wa wachimbaji wadogo Shinyanga, natoa wito kwa wachimbaji nchini kutumia vyama vyao washiriki maonesho haya ya Arusha kwa kuleta madini yao. Soko la uhakika lipo," alisema Kibusi. Aidha, Kibusi alitumia fursa hiyo kuwataka wachimbaji nchini kuachana na matumizi ya zebaki na kuwataka kutumia njia bora zinazoelekezwa na Serikali.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampuni hiyo Ravi Hasmukh, alisema kuwa, kampuni hiyo imeshiriki Maonesho hayo ili kuweza kujenga mtandao wa kibiashara ikiwemo pia kutoa fursa kwa Watanzania kujifunza namna Madini ya Almas yanavyochimbwa na mahali yanapopatikana. Aidha, ameitaka Serikali ifikishe umeme katika eneo hilo na maeneo mengine mbapo shughuli za uchimbaji mdogo zipofanyika ili kuwezesha kuharakisha maendeleo ikiwemo kuwezesha shughuli za kiuchumi na kupanua wigo wa ajira.

Akizungumzia namna kampuni hiyo inavyosaidia eneo linalozunguka mgodi wake alisema kuwa, kampuni hiyo imetengeneza kisima cha maji kwa ajili ya kijiji cha Hukiro pamoja na kuboresha baadhi ya miundombinu katika zahanati iliyo jirani na mgodi wa kampuni hiyo Maonesho ya 6 ya Kimataifa ya Vito Arusha yalifunguliwa rasmi tarehe 3 Mei na Mkuu wa Mkoa wa Manyara Dkt. Joel Bendera na kufungwa na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo.
Mshauri Mwelekezi wa SANA Gems Gregory Kibusi, (kulia), akionesha madini ya Almas . Katikati ni Mkurugenzi wa Kampuni hiyo Ravi Hasmukh. Kulia ni Mkurugenzi Mwenza Kishan Bhatti.
Madini ya Almas ambayo bado hayajasanifiwa.
Mkurugenzi wa Uthamini wa Madini ya Almas (TANSORT) kutoka Wizara ya Nishati na Madini Archard Kalugendo (kulia) akimwonesha Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mrisho Gambo (kushoto) namna ya kupima ubora wa Madini ya Tanzanite.
Mjiolojia kutoka Kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) Jumanne Shimba, akiangalia madini kwa kutumia kifaa maalum cha kinachotumiwa na kituo hicho katika mafunzo.
Mnunuzi wa Madini ya Tanzanite (kushoto) akiangalia ubora wa Madini ya Tanzanite katika Banda la Kampuni ya TanzaniteOne. Kulia ni Mwakilishi wa Kampuni ya TanzaniteOne.
Watumishi kutoka Kituo Cha Jemolojia Tanzania (TGC), wakimsikiliza mgeni aliyembelea banda la kituo hicho ili kujua shughuli za mafunzo ya usanifu na unga'rishaji wa madini zinavyofanyika. Mikufu inayoonekana katika picha pamoja na mapambo mengine imetengenezwa kituo hapo. Kituo hicho kiko chini ya Wizara ya Nishati na Madini.
Ujenzi wa kisima cha maji kilichojengwa na Kampuni ya SANA Gems Ltd ikiwa ni sehemu ya kuwezesha jamii inayozunguka mgodi wa kampuni hiyo kunufaika na uwepo wa mgodi husika.

No comments: