Thursday, May 18, 2017

TTCL yadhamini semina ya vijana

SHIRIKA la Trust Care Tanzania Foundation kwa kushirikiana na Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) wameandaa semina ya kuwajengea uwezo wa kifikra wanafunzi wa vyuo vikuu mbalimbali vya jijini Dar es Salaam ikiwa na lengo la kuwabadili wanafunzi kwa ujumla kuwa na mawazo chanya yatakayowawezesha kutumia fursa anuai zinazowazunguka katika jamii mara baada ya masomo yao.
Akizungumzia semina hiyo inayotarajiwa kufanyika Jumamosi ya tarehe 20/05/2017 katika ukumbi wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Dar es Salaam (DUCE) kuanzia majira ya saa tatu asubuhi, Mkurugenzi Mtendaji wa Trust Care Tanzania Foundation, Zambert Mbwafu alisema semina hiyo ni maalum kwa wanafunzi waliopo vyuoni kwa ajili ya kuwajengea uwezo.Alizitaja mada ambazo wanafunzi wanatarajia kufundishwa ni pamoja na Umuhimu wa Kujiamini na Kujijengea Uwezo, Uwezo wa Uthubutu, Vipaji na Jinsi ya Kuviendeleza, Maadili na Nidhamu katika Kazi na Ubunifu katika Kufikia Malengo. “Semina inawaandaa vijana waliopo na ambao wanatarajia kumaliza elimu yao ya juu hivi karibuni kupata elimu na ujuzi utakaowasaidia wakiwa shule na baada ya kumaliza masomo yao ili waweze kwenda sambamba na mahitaji ya ulimwengu wa sasa…” alisema Bw. Mbwafu.
Akifafanua zaidi Mkurugenzi, Zambert Mbwafu, alivitaja vyuo vitakavyoshiriki katika semina hiyo; ni pamoja IFM, CBE, DIT, DUCE, TIA, UDSM, MUHAS, CHUO CHA DIPLOMASIA, KIU, CHUO CHA USTAWI WA JAMII NA CHUO KIKUU CHA TUMAINI.
Kwa upande wa wadhamini wakuu wa semina hiyo Kampuni ya TTCL, Injinia Enocent Msasi Mkurugenzi wa Biashara TTCL alisema kampuni hiyo inaunga mkono kampuni ya Trust Care Tanzania kwa dhumuni lake la kuisaidia jamii katika maeneo mbalimbali, ikiwemo sekta za kiafya, kielimu na kijamii. Aliongeza kuwa lengo hilo linashabihiana na lengo la TTCL kuhakikisha inakuwa na jamii bora zaidi kiteknolojia, kielimu, kiafya na kimaendeleo kwa ujumla.
“TTCL imedhamini semina hii kwasababu inatoa mchango mkubwa katika kujenga taifa lenye vijana wachapakazi, vijana wenye mtizamo chanya, vijana wenye uwezo wa uthubutu, na kupambana na changamoto mbalimbali za kimaisha, ” alisema Msasi na kuongeza kuwa TTCL kupitia huduma zake bora za intaneti, sauti na SMS inawaunga mkono vijana mara zote na itakuwa mstari wa mbele kufanikisha juhudi zao za kuleta mabadiliko chanya katika jamii.
“TTCL kwa miaka mingi tumekuwa tukipokea vijana wanaokuja kufanya mafunzo kwa vitendo kutoka vyuo na taasisi mbalimbali za elimu zinazotoa elimu katika fani tofauti tofauti. Lakini safari hii tumekuja kivingine zaidi, kwa kuja na programu ambayo itasaidia vijana kupata uzoefu baada ya kumaliza masomo yao. Hii itasaidia kuondoa changamoto ya vijana wetu waliomaliza elimu ya juu ambao mara nyingi hupoteza fursa mbalimbali za ajira kwa kukosa sifa ya uzoefu.”
Vijana watakao pata fursa ya kufanya kazi na TTCL watajifunza mengi kawa vitendo huku wakiongozwa kwa wataalamu wabobezi katika fani mbalimbali. Tunaamini watakapomaliza programu hiyo vijana hao watapata fursa kupata ajira kwenye taasisi na makampuni mbalimbali, au kujiajiri wenyewe,” alisisitiza Enocent Msasi akizungumza na wanahabari leo.


No comments: