Sunday, May 28, 2017

TRA Watoa Somo la Ulipaji Kodi kwa Wafanyabiashara wa Kichina




Meneja wa Idara ya Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi wa TRA, Gabriel Mwangosi akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu semina juu ya Kodi, Utaratibu na Sheria kwa wafanyabiashara kutoka China iliyoandaliwa kwa ushirikiano wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) pamoja na Kampuni ya Jiteng Consultancy Ltd na kufanyika leo Jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa Makumbusho ya Taifa.
2
Mrakibu wa uhamiaji na Afisa Vibali vya Ukazi, Eliud Ikomba akitoa semina kwa wafanyabiashara kutoka China (hawapo pichani) juu ya sheria za uhamiaji katika semina iliyoandaliwa kwa ushirikiano wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) pamoja na Kampuni ya Jiteng Consultancy Ltd na kufanyika leo Jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa Makumbusho ya Taifa.
3
Baadhi ya wafanyabiashara kutoka China wanaofanya biashara zao nchini wakisikiliza mafunzo mbalimbali juu ya Kodi, Utaratibu na Sheria katika semina iliyoandaliwa kwa ushirikiano wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) pamoja na Kampuni ya Jiteng Consultancy Ltd na kufanyika leo Jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa Makumbusho ya Taifa.

Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.    
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imetoa somo la masuala ya kodi kwa wafanyabiashara kutoka China wanaoishi nchini kwa lengo la kuwaongezea uelewa juu ya sheria na taratibu za ulipaji kodi katika semina kuhusu mafunzo hayo leo Jijini Dar es Salaam.

Akiwasilisha mada wakati wa mafunzo hayo, Meneja wa Idara ya Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi wa TRA, Gabriel Mwangosi amesema kuwa Tanzania ya sasa ina fursa nyingi za uwekezaji hivyo wafanyabiashara hao watakapokuja kuwekeza lazima wafahamu kanuni na taratibu za ulipaji kodi nchini ili waweze kuendana na sheria zilizopangwa na nchini.

“Semina hii mahususi imeandaliwa kwa ajili ya wafanyabiashara wa kichina wanaoishi nchini kupata mafunzo ya kodi zikiwemo za zuio, majengo pamoja na ushuru na forodha ambazo ni lazima wazifahamu kwa manufaa ya Taifa letu na wao pia,”alisema Mwangosi.

Mwangosi ameongeza kuwa hii ni mara ya 6 kufanyika kwa semina hizo kwa wafanyabiashara hao ambapo tangu zianze kufanyika zimewasaidia kutokwenda kinyume na taratibu zilizowekwa nchini.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Uhamasishaji Uwekezaji wa Ndani kutoka Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Dotto Stanley amesema kuelimisha umma hasa kwa wageni kutoka nje ya nchi ni jambo la msingi litakalowarahisishia kufahamu sheria za nchi ambapo kwa namna nyingine itachochea uwekezaji.

“Kwa kawaida wafanyabiashara wakubwa huwa wanahitaji kufahamu sheria na taratibu za nchi husika kabla hawajaamua kuwekeza mahali hivyo mafunzo hayo yatachochea uwekezaji nchini kwa sababu watakuwa na uelewa wa mchakato mzima juu ya sheria za uwekezaji na kodi.”alisema Stanley.

Naye Mkurugenzi wa Uendeshaji kutoka Kampuni ya Jiteng Consultancy Ltd, Anne Werema Maneno amesema kuwa changamoto kubwa inayowapata wafanyabiashara wa kichina ni kukosa uelewa juu ya jinsi ya kuwekeza nchini hasa katika suala la ulipaji kodi.

“Changamoto hiyo inawapelekea wafanyabiashara kukosa muelekeo wa biashara waliyopanga kufanya kwani wengi wao wakifika Tanzania hubadilisha biashara baada ya kufahamishwa sheria na kanuni mbalimbali zinazohusu biashara hivyo semina hiyo itawapa uelewa utakaowawezesha kuchagua biashara watakayoweza kuifanya kulingana na mtaji wa mfanyabiashara husika,”alisema Bi. Anne.

Aidha, katika semina hiyo ya siku moja imeambatana na fursa ya kupata mafunzo kutoka kwa taasisi zingine zinazofanya kazi moja kwa moja katika shughuli ya uwekezaji ambazo ni pamoja na TRA, TIC, Idara ya Uhamiaji, Idara ya Kazi pamoja na Taasisi za Kibenki.

Mafunzo hayo juu ya Kodi, Utaratibu na Sheria kwa wafanyabiashara hao yameandaliwa kwa ushirikiano wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) pamoja na Kampuni ya Jiteng Consultancy Ltd na kufanyika katika ukumbi wa Makumbusho ya Taifa ikiwa ni utaratibu wa kawaida wakukutana na wadau mbalimbali wa Kodi.

No comments: