Sunday, May 7, 2017

Taasisi ya TradeMark East Africa (TMEA) yazijengea Uwezo bidhaa za Tanzania kuingia masoko ya kimataifa.

Mkurugenzi wa TradeMark Tawi la Tanzania Bw. John Ulanga
Na Pascal Mayalla 
 Taasisi ya TradeMark East Africa inazijengea uwezo bidhaa za Tanzania ili  kuziingiza kwenye masoko ya kimataifa, kwa kuziwezesha kukidhi viwango vya ubora wa kimataifa.
Kwa hatua hiyo bidhaa hizo zitakuwa na uwezo wa kuhimili ushindani wa kimataifa na kuingia kwenye masoko ya Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki, Bara la Afrika na masoko ya kimataifa yakiwemo masoko ya Ulaya na Marekani, amesema Mkurugenzi wa TradeMark Tawi la Tanzania, Bw. John Ulanga kwenye kongamano ukumbi wa Ubungo Plaza jijini Dar es salaam Jumamosi.
Bw. Ulanga amesema zoezi la kuhakikisha bidhaa za Tanzania zinafikia viwango vya ubora wa kimataifa, linafanywa kwa kupitia mafunzo ya viwango vya ubora kwa kuzitumia taasisi za TBC, TFDA na GS 1 kwa ajili ya barcode kwa bidhaa za Tanzania, hivyo bidhaa hizo kuweza kuhimili ushindani katika masoko ya kimataifa kwa kukidhi viwango vya ubora wa kimataifa. 
 Bw. Ulanga amesema mafunzo hayo yanaendeshwa kwa awamu mbalimbali, ni sehemu ya utakelezaji wa mradi mkubwa wa Taasisi ya Trademark East Africa ujulikanao kama “Women in Trade” unaolenga kuwajengea uwezo wafanyabiashara wanawake wa Tanzania, kuhimili ushindani wa kibiashara na kukabiliana na vikwazo vya kibiashara kwa wafanyabiasha wanawake Tanzania kuwawezesha kufanya biashara ya kimataifa ikiwemo kuwezesha bidhaa zao kuyafikia masoko ya nchi za Afrika Mashariki na masoko ya kimataifa ambapo Taasisi ya TradeMark imetenga Dola za Marekani zaidi ya Milioni 5,300,000 ambazo ni zaidi ya Shilingi Bilioni 12 za Kitanzania kugharimia mpango huo. 
 Ulanga amesema walengwa wa mafunzo ya awamu hii ni wafanyabiashara wanawake wa Tanzania, walio chini ya mwamvuli wa Chama cha Wafanyabiashara Wanawake Tanzania , (Tanzania Women Chamber of Commerce, TWCC), ambapo mafunzo ya mwanzo ilikuwa ni kuwajengea uwezo ili kuweza kuvuka mipaka na kuwezesha bidhaa za Tanzania, kuyafikia masoko ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki na hata nje ya bara la Afrika, lakini mafunzo ya sasa ni kuwajengea uwezo wa kukidhi viwango vya ubora wa kimataifa. 
Bwana Ulanga amesema, TradeMark East Africa ni taasisi inayoongoza katika kuleta usawa wa kijinsia katika biashara, kwa sababu utafiti umeonyesha kuwa asilimia 70% ya wanaofanya biashara za mipakani ni wanawake na wanakabiliwa na vikwazo vingi vya kibiashara vikiwemo vikwazo vya kijiografia, vikwazo vya kijinsia, vikwazo vya kisheria, vikwazo vya kimtazamo, hivyo TradeMark  imeamua kuanza kwa kumkomboa mwanamke kupitia  Chama cha Wafanyabiashara Wanawake Tanzania, TWCC, kimepatiwa shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuendesha shughuli zake, ikiwemo kuendesha mafunzo hayo nchi nzima. 
“Ukimuwezesha mwanamke, ni kuiwezesha familia nzima, familia zikiwezeshwa ni kuwezesha jamii nzima na jamii zikiwezeshwa na kuwezesha taifa kwa ujumla, hivyo uwezeshaji huo  kwa wanawake ni uwezeshaji kwa taifa kupata maendeleo” Alisema Bw. Ulanga. 
Kwa upande wake, Mwenyekiti  wa  TWCC, Bibi, Jaquline Mneney Maleko, amewasisitiza wafanyabiashara wanawake wa Tanzania, kuzichangamkia fursa za kuwajengea uwezo, zinazotolewa na TWCC kwa udhamini wa Trademark East Africa, Bi Maleko amewaasa wanawake kutafuta zaidi elimu ya ujasiliamali na sio tuu kujikita kwenye kutafuta pesa, mwanamke aliyeelimika, anakuwa na uwezo wa kufanya biashara kubwa zaidi hivyo kutengeneza fedha zaidi kuliko mwanamke asyeelimikaMkurugenzi wa TWCC, Wakili Nourine Mawalla, amesema wanawake wa Tanzania wanajituma sana katika ujasiliamali wa uzalishaji wa bidhaa bora, lakini bidhaa zao zimekuwa zikikosa masoko ya kimataifa kutokana na kukosa viwango vya ubora  wa kimataifa, hivyo kupitia TWCC na TMEA, wanawajengea wafanyabiashara, wanawake wa Tanzania, uwezo wa kikidhi viwango vya ubora wa kimataifa, hivyo bidhaa za Tanzania kukubalika katika masoko ya Kimataifa.
Bi Mwala ameishukuru TradeMark kwa ufadhili wa mafunzo hayo na kueleza uwepo wa soko la Afrika Mashariki ni fursa, hivyo Chama cha TWCC, kinaishukuru TMEA kuwajengea uwezo wafanyabiashara wanawake wa Tanzania, kuchangamkia fursa za soko hilo, kufuatia wanawake ndio idadi kubwa ya wafanyabiashara, lakini wengi huishia kufanya biashara ndogo ndogo kutokana na kuwa na uwezo mdogo, hivyo chama hicho kinawajengea uwezo na kuwafungulia fursa za kupata mitaji mikubwa, na kuingiza bidhaa zao kwenye soko la Afrika  Mashariki na masoko ya kimataifa.

TradeMark East Africa (TMEA) ni shirika lisilo la kiserikali, la maendeleo kwa lengo la kuongezeka ustawi wa kiuchumi katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa njia ya biashara. TMEA inafanya kazi kwa karibu na taasisi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), serikali za kitaifa, sekta binafsi na asasi za kiraia.
TMEA inachangia ukuaji wa biashara Afrika Mashariki kwa kufungua fursa za kiuchumi kupitia kuongezeka kwa fursa za upatikanaji  wa  masoko, kuboresha mazingira ya biashara, na kuboresha biashara ya ushindani hivyo kuongezeka kwa kiwango cha biashara hivyo kuchangia  ukuaji wa uchumi, kupunguza umaskini nakuleta maendeleo ya taifa la Tanzania.
TMEA ina makao yake makuu mjini Nairobi nchini Kenya, na ina  matawi katika miji ya Arusha, Bujumbura, Dar es Salaam, Juba, Kampala na Kigali.





No comments: