Wednesday, May 17, 2017

Serikali Yakusudia Kujenga Magereza Maeneo ya Kilimo

Na Nuru Juma-MAELEZO

Serikali inamkakati wa kuhakikisha inajenga Magereza katika maeneo yenye uzalishaji mkubwa wa kilimo ambayo pia yana ukubwa wa kutosha ili kazi ya kuwarekebisha wafungwa iwe rahisi kufanyika huku shughuli za uzalishaji zikiwa zinaendelea.

Hayo yamesemwa leo Bungeni Mjini Dodoma na Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mhe. Mwigulu Nchemba alipokuwa akijibu swali la Mhe Devotha Minja Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Morogoro. 

“Magereza hayo yatajengwa katika maeneo yenye Kilimo na yatakuwa ni kwa ajili ya watu waliokwisha hukumiwa huku yale Magereza ya mijini yawe kwa ajili ya mahabusu tu ili wawe karibu na Mahakama,”alisema Mwigulu. 

Aliongeza kuwa mkakati huo wa Serikali ni wa muda mrefu na wanahitaji kufanya hivyo ili kurahisisha shughuli za maendeleo zinazofanywa na wafungwa na pia kupunguza msongamano wa wafungwa katika Magereza.

Hili pia linatokana na tamko la Mh.Rais Dkt John Pombe Magufuli alilowahi kulitoa hivi karibuni kuwa wafungwa wako katika kutumikia adhabu hivyo wanatakiwa kufanya kazi hasa za kilimo ili kwanza kujipatia chakula na sio kukaa tu bure na kusubiri kila kitu wafanyiwe na serikali.

Aliongeza kuwa Serikali ina mkakati wa kutumia bajeti inayotengwa na nguvu kazi wanayoipata kutoka kwa wataaalam walionao kwa upande wa askari Magereza na wafungwa ili kukarabati Magereza chakavu na kujenga nyumba za askari.

Aidha alibainisha kuwa suala la kukatwa kwa umeme katika Magereza, nyumba za askari,pamoja na maeneo na maeneo mengine ya kambi za Jeshi la Polisi na Magereza limeshafanyiwa kazi na serikali kwa kupitia hazina imekwishatoa fedha kwa ajili ya kutatua tatizo hilo.

Mheshimiwa Waziri aliliambia Bunge kuwa sheria zimeainisha baadhi ya haki za mfungwa zikiwemo huduma za afya kwa wakati,kupewa chakula, uhuru wa kutembelewa na ndugu zake na kupata mawasiliano kwa kusoma magazeti,kusikiliza taarifa za habari na kuandikiwa barua na ndugu zao,haki ya kukata rufaa ikiwa hakuridhika na hukumu yake, malazi safi na yakutosha pamoja na kushiriki michezo mabalimbali.

No comments: