Friday, May 26, 2017

Serikali yaanzisha mfumo wa ununuzi wa mbolea kwa pamoja

Kaimu Mkurugenzi Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) Bw. Lazaro Kitandu akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam kuhusu mfumo mpya wa ununuzi wa mbolea kwa pamoja (Bulk Procurement System). Kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kutoka Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi Bw. Richard Kasuga. Picha na Fatma Salum- MAELEZO 



Na Fatma Salum (MAELEZO)

Serikali kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea nchini (TFRA) imeanzisha mfumo mpya wa ununuzi wa mbolea kwa pamoja (Bulk Procurement System) kutoka nje ya nchi utakaosaidia kupunguza bei na kuhamasisha matumizi ya mbolea kwa wakulima.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka hiyo Bw. Lazaro Kitandu alisema uamuzi huo wa kuanzisha mfumo mpya umekuja baada ya Serikali kugundua kuwa kwa muda mrefu matumizi ya mbolea hapa nchini si ya kuridhisha kutokana na bei ya mbolea kuwa juu.

“Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na wadau wa masuala ya mbolea imeanzisha mfumo huu baada kupitia tafiti mbalimbali zilizofanywa na wataalam waelekezi wa ndani na nje ya nchi na kutumia uzoefu wa taasisi nyingine zinazofanya ununuzi wa bidhaa kwa pamoja” Alisema Kitandu.

Kitandu alieleza kuwa katika nchi zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara (SSA), Tanzania ni mojawapo ya nchi zenye matumizi ya chini ya mbolea kwa kutumia kilo 19 za virutubisho hivyo kwa hekta katika ngazi ya wakulima wadogo ambapo kiasi hicho hakiendani na malengo ya azimio la Maputo la nchi za SADC linalotaka kufikia angalau kilo 50 kwa hekta moja.

Alisema kuwa kwa msimu wa mwaka 2017/2018 mfumo huo utaanza na aina mbili tu za mbolea ambazo ni mbolea ya kupandia (DAP) na mbolea ya kukuzia (UREA) na mbolea nyingine zitafuata baadaye kadri itakavyoonekana mfumo huo kuleta manufaa kwa wakulima.

Akifafanua kuhusu faida za mfumo wa ununuzi wa mbolea kwa pamoja, Kitandu alisema utasaidia kuimarisha utaratibu wa usambazaji wa mbolea ambapo wadau wote watakuwa na uhakika wa upatikanaji wa mbolea kwa bei ya ushindani.

Kwa mujibu wa Kitandu pia mfumo huo utawezesha wafanyabiashara wadogo kukua na kushiriki katika biashara ya mbolea na kuimarisha mtandao wa usambazaji hadi ngazi ya mkulima.

“Ununuzi wa mbolea kwa pamoja pia utasaidia kudhibiti bei ya mbolea iwapo kutajitokeza ongezeka lisilokuwa na sababu (soko holela) kwa kuwa bei itatangazwa kwa kuzingatia bei halisi ya mbolea, gharama halisi za usafirishaji wa mbolea, tozo mbalimbali na kiwango stahiki cha faida ya mfanya biashara” alibainisha Kitandu.

Serikali kupitia mfumo huu inatarajia matokeo chanya katika kupunguza bei ya mbolea kwa wakulima hivyo kuongezeka kwa matumizi ya mbolea na uzalishaji wenye tija ili kuchochea maendeleo ya uchumi wa viwanda.

No comments: