Wednesday, May 24, 2017

MKUU WA WILAYA YA UBUNGO AAGIZA KUANZA UJENZI WA MADARASA MANNE NA VYOO VYA SHULE YA SEKONDARI MBURAHATI

Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe Kisare Makori akizungumza wakati wa ziara yake ya kikazi katika shule ya Sekondari Mburahati iliyopo Katika Mtaa wa Barafu, Kata ya Mburahati Jijini Dar es salaam.Leo Jumatano, Mei 24, 2017
Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe Kisare Makori akisikiliza maelezo kuhusu shule ya Sekondari Mburahati mara baada ya kuzuru shuleni hapo.Leo Jumatano, Mei 24, 2017
Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Mburahati Ndg Bagaya Kashato akielezea changamoto zinazoikabili shule hiyo mbele ya Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe Kisare Makori
Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe Kisare Makori akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuzuru  shule ya Sekondari Mburahati .Leo Jumatano, Mei 24, 2017
Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe Kisare Makori (Kulia) akimsikiliza Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Mburahati Ndg Bagaya Kashato akitoa maelezo kuhusu  kukwama kwa ujenzi wa madara ya shule ya Sekondari Mburahati mara baada ya kuzuru shuleni hapo, Mwingine ni Katibu Tawala wa Wilaya ya Ubungo Ndg James mkubo.Leo Jumatano, Mei 24, 2017
Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe Kisare Makori akisisitiza jambo wakati wa ukaguzi wa madarasa ya shule ya Sekondari Mburahati



Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe Kisare Makori Leo Jumatano, Mei 24, 2017 ameiagiza Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Ubungo inayoongozwa na Ndg John Lipesi Kayombo kuanza mchakato wa ukamilisho wa ujenzi wa Madarasa manne katika shule ya Sekondari Mburahati iliyopo Katika Mtaa wa Barafu, Kata ya Mburahati Jijini Dar es salaam.

Sambamba na Agizo hilo pia ameagiza kujengwa vyoo vya wanafunzi kutokana na uchache wa vyoo vilivyopo ili kukabiliana na wingi wa wanafunzi.

Mkuu wa Wilaya ametoa agizo hilo wakati wa kikao Cha pamoja kilichofanyika Shuleni hapo kwa kuhudhuriwa na Uongozi wa Shule hiyo, Kamati ya Shule, Uongozi wa serikali ya Mtaa na Afisa Mtendaji wa Kata ya Mburahati.

Mhe Makori alisema kuwa kutokana na ongezeko la wanafunzi wanaojiunga na kidato Cha kwanza Kila mwaka kumekuwa na upungufu mkubwa wa madawati Jambo ambalo linachangia wanafunzi shuleni hapo kuanza kusoma kwa kupokezana hivyo mpango mahususi kukabiliana na changamoto hiyo ni pamoja na kuanza kujenga miundombinu ya kutosha itakayowasaidia wanafunzi kupata elimu bora.

Akizungumzia changamoto ya upungufu wa walimu shuleni hapo Mkuu wa Wilaya alisema kuwa wakati serikali inajiandaa na mkakati wa jumla wa kuikabili changamoto hiyo ni vyema uongozi wa shule kutafuta walimu wa muda ili kupunguza kadhia ya wanafunzi kukosa vipindi kwa sababu ya upungufu wa walimu.

Shule ya Sekondari Mburahati ni shule ya kutwa iliyoanzishwa mwaka 2010 ambapo pamoja na kuwa na wanafunzi wengi ina jumla ya vyumba vya madarasa 9 huku mahitaji yakiwa ni vyumba 25 hivyo kupelekea kuwa na upungufu wa madarasa 16.

Hata hivyo Mkuu wa Wilaya Mhe Makori amesema kuwa pamoja na changamoto nyingi zinazoikabili shule hiyo lakini Manispaa ianze na changamoto za utatuzi wa Uhaba wa Madarasa na upatikanaji wa vyoo vya kisasa.

Akitoa neno la Shukrani kwa niaba ya Walimu wenzake, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Mburahati Ndg Bagaya Kashato amempongeza Mkuu wa Wilaya ya Ubungo kwa kazi kubwa anayoifanya ikiwemo utatuzi wa migogoro ya Ardhi na ujenzi wa vyumba vya madarasa katika Wilaya hiyo.

Kashato ametumia nafasi hiyo pia kumuomba Mkuu huyo wa Wilaya kusaidia utatuzi wa changamoto ya Upungufu wa vitabu vya kufundishia masomo ya sanaa kulingana na idadi kubwa ya wanafunzi, Kukamilishwa Mfumo wa gesi katika Maabara ya shule hiyo na ujenzi kwa ajili ya jengo la Utawala.

Imetolewa Na;
Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Ubungo

No comments: