Friday, May 12, 2017

KISHAPU YAZINDUA MASHINDANO YA UMISETA

Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga imezindua mashindano ya Michezo ya Sekondari Tanzania (UMISETA) kwa mwaka 2017 kitarafa katika viwanja vya shule ya sekondari Shinyanga.

Mashindano hayo yamehusisha mpira wa miguu, netiboli, kikapu, wavu na riadha ambapo yatashirikisha shule za tarafa mbalimbali wilayani humo ambapo washindi watashindanishwa kupata timu za wilaya.

Akizungumza na wachezaji kutoka shule za Shinyanga sekondari, Maganzo Songwa, Mwadui ufundi, Idukilo na Mwadui Lutheran kwa niaba ya mkurugenzi mtendaji, Ofisa elimu sekondari, Paul Kasanda aliwataka kuwa wamoja.

Alisema pamoja na kuwa wachezaji hao wanatoka shule mbalimbali wilayani humo wanapaswa kushirikiana na kupata ushindi pindi watakapocheza na wilaya zingine kutafuta wawakilishi ngazi ya taifa.

Kasanda aliongeza kwa kusema kuwa michezo ni upendo, furaha, huleta furaha na pia huweza hata kutoa ajira kama zingine endapo wachezaji watajituma vizuri wataweza kufika mbali.

“Pamoja na kuwa ninyi ni wamoja mnatoka wilaya moja lakini tunataka mtuoneshe ufundi wenu, vipaji na ushindani ili tupate timu bora zitakazoshindana na wilaya zingine,” alisema Kasanda.

Mashindano ya UMISETA kiwilaya yanatarajiwa kuanza kutimua vumbi Mei 21 ambapo kimkoa ni Mei 22 hadi Juni 5 wakati kitaifa ni Juni 6 hadi 15 mwaka huu.
Ofisa Elimu Sekondari Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Paul Kasanda akizungumza na wachezaji wanafunzi kutoka shule mbalimbali washiriki wa mashindano ya UMISETA ngazi ya wilaya katika viwanja vya Shinyanga Sekondari.
Wachezaji wasichana wakionesha vipaji vyao katika kusakata soka (mchezo wa mpira wa miguu) kupata timu itakayowakilisha wilaya katika mashindano hayo.
Timu za netiboli kutoka shule mbalimbali zikitoana jasho kupata washindi kwa ajili ya kushindana ngazi ya mkoa.
Wavulana wakitoana jasho katika mchezo wa mpira wa wavu.
Riadha nayo haikuwa nyuma ambapo washiriki hawa wavulana wakishindana katika mbio ndefu na fupi zikihusisha umbali tofauti tofauti kuanzia mita 100 hadi mita 3000.
Mchezaji wa riadha akiruka wakati wa mashindano ya miruko ya chini ‘low jump’ wakati wa michuano hiyo.
Mwalimu Nassoro Said kutoka Shule ya Sekondari Igaga akitoa maelezo kwa timu ya riadha yam bio fupi maarufu kama wakimbiza upepo kabla ya kuanza kushindana kukimbia. 
Washiriki wasichana wakishindana katika mbio ndefu na fupi zikihusisha umbali tofauti tofauti kuanzia mita 100 hadi mita 3000.

No comments: