Friday, May 26, 2017

Dkt.Semboja amsifu Rais Magufuli kuhusu ripoti ya mchanga, Awataka watanzania kumsaidia katika vita hiyo


Na. Immaculate Makilika- MAELEZO

 Mtafiti wa masuala ya Uchumi na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam  Dkt.Haji Semboja anasema kuwa amefurahishwa na ripoti ya Kamati Maalum iliyoteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  John Pombe Magufuli  ya  kuchunguza mchanga wa madini kwenye makontena 277 yaliyozuiwa na serikali kusafirishwa kwenda nje kwaajili ya uchenjuaji.

Akizungumza Jijini Dar es Salaam  katika mahojiano na mwandishi wa habari hii, Dkt.Semboja alisema kuwa, hatua hiyo ni nzuri na ya kuridhisha  kwa vile Rais Magufuli amefanyia kazi suala hilo ambalo limekua likizungumzwa kwa muda mrefu na baadhi ya wasomi,wanaharakati na hata wanasiasa hapa nchini.

“Mimi ni kati ya Watanzania waliofurahishwa na maamuzi ya Rais, nina furaha kubwa hasa ukizingatia niliwahi kushiriki katika uandaaji wa sera za madini na uwekezaji, na ni wazi kuwa tumekuwa tukiibiwa kwa kiwango kikubwa katika sekta ya madini” alisema  Dkt.Semboja.

Malalamiko haya  ya wizi na utoroshaji wa madini yamekuwepo kwa muda mrefu,  kitu ambacho tulikua tukizungumza    sasa  kimethibitishwa , baada ya Rais Magufuli  kupokea ripoti hiyo ya mchanga”, aliongeza Dkt.Semboja.

Aidha, Dkt.Semboja amemshauri  Rais Magufuli  kuendelea kuwatumia wataalamu mbalimbali waliopo nchini na kuiomba Serikali iwe na utaratibu wa kuwatumia watu wake ambao wengi ni wazalendo na wana uchungu na nchi yao.

Pia ameishauri Serikali kuzipitia upya Sheria, Sera na mikataba inayohusu madini pamoja na kuzisimamia vyema taasisi zilizowekwa kushughulikia  sekta ya madini, ikiwa ni pamoja na nchi kujijengea uwezo wa kuchenjua madini bila kuwepo kwa ulazima wa kupeleka mchanga nje ya nchi. Pia ameishauri  serikali kuweka mikakati ya kuyaongezea thamani madini ili yauzwe hapahapa nchini tofauti na ilivyo sasa ambapo serikali inategemea kuchukua kodi tu na mrabaha.

“Tanzania inapoteza kiasi cha Tsh. Bilioni 829.4 hadi Trilioni 1.439 kwa kusafirisha mchanga nje ya nchi,hivyo ni vyema tukasimamia sekta ya madini kikamilifu kwani kiuchumi inaweza kututoa hapa tulipo na kutuletea maendeleo tunayoyataka”, alisema Dkt.Semboja.

Naye Mtendaji Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya wachimba Madini Wadogowadogo Tanzania (FEMATA), Haruni Kinega alisema kuwa wamefurahishwa  na wanampongeza  Rais  Magufuli kwa  hatua ya kusitisha usafirishaji wa mchanga wa madini kwa vile kuna faida kubwa kutokana na kutosafirishwa kwa mchanga huo.

“Hii ni fursa na faida kwa wadau na wafanyabiashara wa sekta ya madini kuleta mashine za uchenjuaji wa madini pamoja na kuwezesha shughuli za uchakataji wa madini kufanyika hapa nchini”, alisema Bw.Kinega.

Pia Bw. Kinega alieleza kuwa kuna baadhi ya viwanda vyenye uwezo wa kufanya uchakataji wa madini hapa nchini lakini vinakosa malighafi ya kutosha na hivyo vinajiedesha kwa hasara na kuyalazimu makampuni kupeleka mchanga nje ya nchi. 

Aidha Bw.Kinega alisema FEMATA itaendelea kuunga mkono juhudi za Rais Magufuli za kuhakikisha watanzania wananufaika na raslimali zilizopo nchini na kuzitaka kampuni zinazofanya shughuli za madini nchini kuwa wawazi na  kufuata sheria za nchi.

Kwa upande wake, Idrisa Kaloli mkazi wa Jiji la Dar es Salaam, alisema kuwa ripoti ya mchanga wa madini ina manufaa kwa umma kwa vile imesaidia kudhibiti mianya ya uvujaji wa raslimali za Watanzania, kwani fedha zote ambazo zingepotea kwenye madini yaliyokuwa yasafirishwe zitasaidia kuleta maendeleo ya Watanzania kama kujenga barabara, mashule, hospitali na hata kununulia madawa na vifaa tiba.

Alisema nchi yetu inautajiri wa kutosha wa rasilimali hivyo ni vyema zikasimamiwa kikamilifu ili ziwweze kuunufaisha umma wa watanzania na sio watu wachache wenye uchu wa utajiri.
Rais Dkt John Pombe Magufuli

No comments: