Saturday, April 22, 2017

WILAYA YA HANDENI YAZINDUA JUKWAA LA UWEZESHAJI WANAWAKE KIUCHUMI

Halmashauri ya Wilaya ya Handeni imezindua jukwaa la uwezeshaji wanawake kiuchumi kwa wanawake wa Wilaya ya Handeni  kwenye ukumbi wa maount Ilulu uliopo Kabuku mjini lenye ujumbe wa “Wezesha wanawake kiuchumi ili kujenga uchumi wa kati na Tanzania ya Viwanda”.

Jukwaa hili linalengo la kuwakutanisha wanawake pamoja na kujadili fursa, changamoto na jinsi ya kushiriki kikamilifu katika biashara na shughuli nyingine za kiuchumi katika Wilaya ya Handeni.

 Akizungumza kwenye uzinduzi wa Jukwaa hilo Katibu Tawala wa Wilaya ya Handeni  Bw. John Mahali aliyekuwa mgeni rasmi akimwakilisha mkuu wa Wilaya ya Handeni Mh. Godwin Gondwe alisema kuwa jukwaa la wanawake hilo  litasaidia  kuongeza uelewa kwa wanawake katika upatikanaji  wa mitaji , sheria za nchi katika masuala ya kiuchumi na jinsi ya kujitegemea.

Aliongeza kuwa wanawake wamekuwa hawapati fursa za kutosha za kiuchumi hapa Nchini hata na duniani kote kutokana na kutokuwa na usawa katika fursa , uwezo wa kupata mitaji.

“jukwaaa litasaidia kuondoa matabaka na sheri ambazo zitasaidia kupunguza ubaguzi wa kiuchumi kwa wanawake, ambalo ni jambo la muhimu sana katika kuleta maendeleo ya usawa katika pato la Taifa, jamii na familia” alisema Bw. John.

Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Handeni Bw. William Makufwe alisema kuwa  jukwaa hili litafanya kazi ya kutambua shughuli za kijasiliamari katika kutoa elimu kuhusu upatikanaji wa mitaji, kusajili biashara, kuwezesha kiuchumi na kutafuta masoko.

Aidha, alisema katika suala la utoaji mikopo vikundi vitakavyopewa kipaumbele ni vile viliyojidhatiti kwa kusajiliwa, vyenye utawala unaoeleweka, miradi inayoonekana na zenye hesabu za kifedha zinazoweza kukaguliwa na kukosolewa inapobidi.

Uzinduzi huo ulipambwa na maonesho ya bidhaa za kijasiliamari ya vikundi mbalimbali kutoka kata mbalimbali. Sekretarieti ya Mkoa wa Tanga itaratibu shughuli zote za uchumi kwenye Wilaya zote ndani ya Mkoa na kuhakikisha kunakuwa na majukwaa ya Wilaya/Halmashauri zote ambayo yatafanya  vikao vyake kila baada ya miezi sita (6).
  
Alda Sadango
Afisa Habari
Halmashauri ya Wilaya ya Handeni

 
 Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni Bw William Makufwe wakwanza kulia akifuatiwa na Katibu tawala Wilaya Bw John Mahali wakitazama Moja ya bidhaa ya vikapu vinavyotengenezwa na kikundi cha wanawake tupendane cha segera
 Katibu tawala Wilaya Bw John Mahali akizungumza na wanawake waiojitokeza kwenye Uzinduzi wa jukwaa Hilo.
 Mkurugenzi Mtendaji Bw William Makufwe akionesha katiba waliyopewa viongozi wa jukwaa la kuwezesha wanawake kiuchumi Wilaya itakayowasaidia Katika Uongozi wao
 Mwenyekiti wa jukwaa la kuwezesha wanawake kiuchumi Wilaya Bi Fatuma Zuberi akipokea katiba kutoka Kwa mgeni rasmi Katibu tawala Wilaya Bw John Mahali.
 Mwenyekiti wa jukwaa la kuwezesha wanawake kiuchumi Wilaya Bi Fatuma Zuberi akishukuru wanawake waliompa dhamana ya kuwaongoza.
 Baadhi ya vikundi vya wanawake waliojitokeza kuonesha bidhaa zao wakati wa Uzinduzi.
 Baadhi ya wanawake wakishiriki wa Uzinduzi wa jukwaa la kuwezesha wanawake kiuchumi Wilaya  ya Handeni
Viongozi wakipata maelezo kutoka vikundi vya kinamama.

No comments: