Tuesday, April 4, 2017

RAIS WA ZANZIBAT DKT SHEIN AKAGUA MIRADIYA MAENDELEO MKOA WA KASKAZINI PEMBA


Na Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ametembelea miradi ya maendeleo kisiwani Pemba ukiwemo mradi wa barabara, umeme na Chuo cha Mafunzo ya Amali na kuitaka Kampuni ya ZECON inayojenga Chuo hicho kuhakikisha mradi wa ujenzi huo unakamilika kwa muda uliopangwa. 
Akiwa katika eneo la chuo hicho huko Daya Mtambwe mara baada ya kupata maelezo kutoka kwa Kampuni ya Ujenzi pamoja na Mshauri Mwelekezi alisisitiza kuwa mradi huo ni wa Serikali na Wizara ya Elimu ni wasimamizi tu, hivyo alieleza umuhimu wa kumalizika mapema mradi huo kwa maslahi ya wananchi. 
Alieleza kuwa changamoto za kiufundi zilizojitokeza katika kutekeleza mradi huo hazina budi kupatiwa ufumbuzi wa haraka ili utekelezaji wa mradi huo uweze kukamilika kama ilivyopangwa. 
Mara baada ya kukagua mradi wa ujenzi wa Chuo cha Amali kilichopo Daya Mtambwe, Dk. Shein alipata nafasi ya kuzungumza na wananchi pamoja na wanafunzi wa Skuli ya Msingi Daya katika viwanja vya skuli hiyo na kusisitiza lengo la Serikali la kujenga chuo hicho. 
Dk. Shein alisema kuwa ujenzi wa Chuo hicho utawasaidia wale wanafunzi waliokuwa hawakupata fursa ya kuendelea na masomo ya juu na kuweza kupata mafunzo ya vitendo yakiwemo mafunzo ya kiufundi. 
Alisema kuwa uwamuzi wa Serikali ni kujenga chuo hicho kama kilivyo chuo cha Amali cha Vitongoji kwa upande wa Pemba na Mkokotoni Unguja na kusisitiza kuwa ujenzi huo utakwenda sambamba na ujenzi wa chuo cha Amali huko Makunduchi. 
Aidha, Dk. Shein alisema kuwa ujenzi wa Chuo hicho ni ahadi aliyoitoa wakati wa Kampeni za uchaguzi mkuu uliopita wakati akiwahutubia wananchi huko Kangagani, na kusisitiza utekelezaji wa ahadi yake hiyo upo pale pale. 
Alisema kuwa licha ya ujenzi huo kusita kutokana na sababu za kiufundi kwa takriban miezi saba kwa hivi sasa na kueleza kuwa si zaidi ya wiki tatu ujenzi huo utaendelea na matarajio ni kumalizika hapo mwakani.

Mapema Dk. Shein alipata fursa ya kukagua ukarabati wa barabara ya Chwale (Madenjani) hadi Mzambarautakao wenye urefu wa kilomita 5 unaoendelea kwa kiwango cha lami ambao unatarajiwa kumalizika baada ya wiki moja. 
Mkuu wa Mradi kutoka Kampuni ya MECCO, Crispin Prosper Mwombeki, alimueleza Dk. Shein kuwa ukarabati huo baada ya miezi saba umefanywa kwa muda wa miezi mitatu ili kwenda na hali halisi ya jiografia ya Pemba.

Pamoja na hayo, Mwombeki alieleza changamoto zilizopo hasa katika suala zima la utaratibu wa upatikanaji wa kifusi kwa ujenzi wa barabara huku akieleza haja ya kuweko na utaratibu wa kudumu wa ukarabati wa barabara hizo ndani ya mwaka mmoja. 

Wakati huo huo, Dk. Shein alifika Ukunjwi kwa ajili ya kuangalia mradi wa umeme unaopelekwa katika kisiwa cha Fundo.

No comments: