Wednesday, April 26, 2017

MACHIMBO YA KITUNDA YASIMAMISHWA KWA MUDA MKUU WA MKOA WA TABORA ILI KUEPUKA MAAFA ZAIDI

Na Tiganya Vincent, RS-Tabora

Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw. Aggrey Mwanri kwa kushirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa huo amesimamisha kwa muda uchimbaji wa madini aina ya dhahabu katika machimbo ya Kitunda wilayani Sikonge ili kuepusha maafa zaidi yasije yakatokea.

Hatua hiyo inafuatia maafa yaliyokea hivi karibuni ambapo wachimbaji wadogo wadogo sita walifariki baada ya kufukiwa na kifusi na mmoja kufariki kwa kukosa hewa wakati wa uchimbaji wa dhahabu katika eneo la Kitunda wilayani Sikonge.

Uamuzi huo umetolewa jana wilayani Sikonge na Mkuu wa Mkoa wa Tabaora Bw, Mwanri baada ya yeye na kwa kushirikiana na Kamati na Ulinzi na Usalama mkoani humo kutembelea machimbo yalisababisha maafa hayo kwa ajili ya kujionea na kasha kuwapa pole wafiwa.

Alisema kuwa yeye na Kamati yake wameona ni vema wasimamishe kwa muda ili taratibu zote za kuhakikisha usalama na zile Baraza la Taifa la Mazingira za mpango wa ulinzi wa mazingira(Environmental Protection Plan) zinafuatwa kabla ya kendelea na shughuli za uchimbaji.

Mkuu huyo wa Mkoa alisema kuwa lengo ni kutaka Wachimbaji hao waendele kuchimba katika hali ya usalama bila kuharatisha maisha yao na nguvu kazi ya Taifa.

Kufuatia hatua hiyo , Bw. Mwanri aliwaagiza Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya Kati na Magharibi Salim Salim na Afisa Madini Mkazi wa Tabora Laurent Mayala kuhakisha kuwa umbali kutoka shimo moja la uchimbaji hadi jingine unazingati matakwa ya Sheria na Kanuni kuliko ilivyo sasa ambapo kutoka shimo hadi shimo ni mita 3 hali ambayo ni hatari.

Aliongeza kuwa ni vema Ofisi hizo zikahakikisha kuwa wanawapanga wachimbaji wadogo wadogo hao kulingana na matakwa ya kisheria na sio kuwaacha wachimbo ovyo ovyo ambapo hivi sasa mashimo yako karibu karibu sana na hivyo kuhatarisha maisha yao .

“Mimi siko tayari kuona watu wengine zaidi wanafariki kwa sababu ya uchimbaji usiozingatia matakwa ya kisheria na ambao hauna baraka za NEMC. Hivyo kaeni chini na wamiliki wa mgodi muwapange vizuri kwa kuzingatia sheria na bila upendeleo” aliagiza Mkuu huyo wa Mkoa.

“Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli ilishaahidi kuwa itawashika mkono wachimbaji wadogo wadogo , lakini ni vema tukahakikisha kuwa Mpango wa Ulinzi wa Kimazingira umezingatiwa na kuwepo na wakaguzi watakao hakikisha kuwa taratibu za umbalimbali toka shimo hadi shimo umezingatiwa ili kulinda usalama wao kwanza ” anasititiza Mkuu wa Mko huyo

Alisema kuwa kuwepo kwa madini ya dhahabu katika eneo la Kitunda ni neema , lakini neema hiyo neema hiyo ni vema utafutaji wa neema hiyo ukazingatia taratibu bila kusababisha maafa mengine kama yaliyotokea wiki iliyopita ambapo watu watano walifia mgodini , mmoja alifia hospitalini na mwingine alikufa kwa kosa hewa katika mgodi mwingine.

Aidha ,Mkuu huyo wa Mkoa aliwaagiza Maafisa Madini kuharikisha katika ufuatiliaji wa Kibali cha NEMC na kuandaa Mpango Kazi wa Uchimbaji Mzuri na salama ili vijana wanaojihusisha na uchimbaji wa madini katika eneo la Kitunda wasikae muda mrefu bila kuendelea na kazi yao ya uchimbaji madini.

Alisema kuwa vijana hao hawana kazi nyingine wanayotegemea kujiingizia kipato zaidi ya uchimbaji wa madini katika eneo hilo , hivyo ni vema watendaji hao kwa kushirikiana na wamiliki wa mgodi huo kuhakikisha mambo yafanyika haraka iwezekanavyo.

Aidha alitoa kwa wachimbaji madini hao kukikisha kuwa sehemu ya mapato yao wayatumie katika kuboresha maisha yao na familia zao kwa kujenga nyumba nzuri, kuvaa vizuri kula vizuri na kulipa kodi zinatakiwa ili neema hiyo iwe na tija kwao.

Bw. Mwanri alisema kuwa haitakuwa na maana ya kuwepo kwa neema hiyo kama watapata fedha na kuendelea kuishi maisha duni .

Naye Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoani Tabora Wilbroad Mtafungwa ametoa onyo kwa baadhi ya vijana wanaendesha vitendo viovu katika eneo hilo kama vile uvutaji bangi, uporoaji na ubakaji kwa kisingizio cha uwepo wa madini ya dhahabu kuacha mara mmoja la sivyo hatua kali zitachukuliwa dhidi yao.

Alisema kuwa Jeshi la Polisi Mkoani huo ili kuimarisha ulinzi na kuhakikisha wachimbaji hao wanaendesha shughuli zao katika mazingira rafiki, limeamua kufungua Kituo Kidogo katika eneo hilo.

Hatua hiyo inalenga kuwepo na ulinzi saa 24 siku zote kwa ajili kuwa tayari wakati wote kukabiliana na uvunjivu na amani na sheria ambao unaweza kujitokeza..

Aidha ,RPC huyo pia aliwaonya wachimbaji wadogo hao kutoenda katika machimbo wakati wote wa zuio hadi hapo watakaporuhusiwa la sivyo watakabiliana na Askari watakaokuwa wakilinda machimbo hayo

Katika hatu nyingine , Kamanda huyo ameowanya Polisi wote watakaokuwa wakilinda eneo hilo kutojihusisha na uchimbaji madini kwani kufanya hivyo kutawasababisha migogoro na wao wakuwa wamekiuka kiapo chao.

Eneo la mchimbo ya Kitunda linawachimbaji zaidi ya 10,000 ambao wanaendesha shughuli hizo .

No comments: