Saturday, March 25, 2017

WAZIRI MBARAWA AKAGUA MIUNDOMBINU BUKOBA MKOANI KAGERA


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa (kulia), akioneshwa taarifa ya mapato na Meneja wa Kampuni ya Simu Nchini (TTCL), mkoa wa Kagera, Bw. Salum Mbaya, wakati alipotembelea ofisini hapo leo.
ML 1
Fundi Mitambo kutoka Kampuni ya Simu Nchini (TTCL), Eng. Godfrey Mbise, akimpa maelezo Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa (kushoto), kuhusu mfumo wa utoaji huduma katika mkongo wa taifa mkoani humo.
ML 2
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa akitoa maelekezo kwa uongozi wa Kampuni ya Simu Nchini (TTCL), mkoa wa Kagera, leo, mara baada ya kukagua mitambo na mifumo iliyopo ofisini hapo.
ML 3
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa akishuka katika ndege ya Kampuni ya Ndege Nchini (ATCL), katika uwanja wa ndege wa Bukoba, mkoani Kagera alipowasili kwa ziara ya kikazi ya siku mbili mkoani humo.
ML 4
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, akitoa maelekezo kwa Meneja wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA), mkoa wa Kagera Bi. Dorice Uhagile, wakati alipowasili Uwanja wa Ndege wa Bukoba ambapo amekagua uwanja huo na kuangalia changamoto mbalimbali zinazokabili uwanja huo.
ML 5
Meneja wa Shirika la Posta Nchini, mkoa wa Kagera Bi. Mary Nsangila, akitoa taarifa ya utendaji kazi wa shirika hilo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa mara baada ya kukagua  maendeleo ya Shirika hilo mkoani humo.
 ML 6
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa (wa kwanza kulia mbele) akipata maelezo kutoka kwa Meneja wa Wakala wa Ufundi na Umeme Nchini (TEMESA), mkoa wa Kagera Eng. Zephrine Bahyona (wa pili kushoto mbele), wakati alipokuwa akikagua karakana yao na kuona changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
…………..

TTCL KUZALISHA DOLA MIL 50.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano  Profesa Makame Mbarawa ameipa miezi miwili  Kampuni ya Simu Tanzania  (TTCL), kuhakikisha kuwa inapata Dola za Kimarekani milioni 50 ili kuongeza pato kwa Kampuni na Taifa kwa ujumla kupitia Mkongo wa Taifa.

Akitoa agizo hilo leo, wilayani Bukoba mkoani Kagera, Waziri Prof. Mbarawa amesema agizo hilo limetokana na Serikali kuongeza masafa kwa kampuni hiyo kutoka 10 hadi 200 (MHZ) ambayo yana uwezo wa kuunganisha wateja wengi na wakubwa zaidi.

Amesisitiza makampuni ya Simu nchini kuchangamkia fursa ili kupata masafa yenye uwezo mkubwa kupitia mkongo huo.

“Hakikisheni mnajipanga kuipata hiyo fedha ndani ya miezi miwili na kuwapatia masafa ya kutosha wateja mlionao ndani na nje ya nchi na kujitahidi kuongeza wateja wengi zaidi”, amesema Prof. Mbarawa.

Aidha, ameitaka TTCL kusogeza  wigo wa kuwasiliana na wateja wakubwa ili kuwashawishi kununua masafa hayo  kulingana na mahitaji yao na hivyo kutanua wigo wa kibiashara  na kuiwezesha kampuni hiyo kupata faida zaidi.

Kwa upande wake Meneja wa TTCL mkoa wa Kagera Bw. Salum Mbaya amemhakikishia Waziri huyo kuwa wataanza mara moja kazi ya kutembelea wateja wa ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuwapatia taarifa za ongezeko la uwezo wa mkongo na kuwashiwishi kujiunga ili kupatiwa masafa wanayohitaji.

Bw. Mbaya ametaja kuwa mpaka kufikia sasa nchi zilizounganishwa na mkongo wa Taifa  ni Rwanda, Burundi, Uganda, Zambia, Kenya na Malawi.
Katika hatua nyingine, Waziri Mbarawa ametembelea uwanja wa ndege wa Bukoba na kuahidi kutatua changamoto zinazoukabili uwanja wa ndege wa Bukoba ikiwemo kujenga jengo la kuongezea ndege (Control Tower) ili kuongeza ufanisi na usalama katika usafiri wa anga.

 Naye, Meneja wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini mkoa wa Kagera, Bi. Dorice Uhagile, licha ya kuelezea mafanikio mbalimbali kama vile ongezeko la ndege na wateja uwanjani hapo pia amefafanua changamoto mbalimbali zinazoukabili uwanja huo na kuiomba serikali iweze kuwatatulia.

Waziri Mbarawa ameanza ziara ya kikazi wilayani Bukoba, mkoani Kagera ambapo ametembelea miradi mbalimbali inayotekelezwa na Taasisi zilizo chini ya Wizara yake

No comments: