Sunday, March 26, 2017

AICC yashauriwa kuwekeza Dodoma

Kamati ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) imeushauri uongozi wa Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC) kuelekeza nguvu ya uwekezji katika mji wa Dodoma ili kuziba kukidhi ongezeko la huduma za kumbi za kufanyia muikutano linalosababishwa na serikali kuhamia katika mji huo.

Akizungumza katika kikao cha majumuisho baada ya Kamati ya PIC kutembelea AICC mwishoni mwa wiki na kukagua miradi miwili, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Albert Obama ameshauri AICC kuupa kipaumbele mkoa wa Dodoma katika mkakati wa kujenga kituo kingine cha kisasa cha Mikutano.

“Tunahitaji kuiona taasisi hii ikipanuka na kujenga vituo vingine vya mikutano huko mikoani na moja ya mikoa ambayo tungependa muipe kipaumbele ni Dodoma maana huko ndio serikali inahamia na mahitaji ya huduma ya kumbi za mikutano yanakwenda kuongezeka”, alisisitiza Obama.

Nae Mjumbe wa Kamati hiyo, Amina Mollel alieleza kufurahishwa na juhudi za uongozi wa AICC kumilisha ujenzi wa mradi wa nyumba za kisasa (apartment) 48 ambapo azote zina wapangaji na kuwa sehemu muhimu ya kuongeza mapato ya shirika.

Aidha ameushauri uongozi wa AICC kuzingati uwekaji wa miundombinu ya walemavu katika miradi mingine inayotekelezwa ukiwemo mradi wa ujenzi wa ukumbi wa kisasa kwa ajili ya maonesho ambao unatarajiwa kukamilika mwezi Mei mwaka huu.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mwendeshaji wa AICC, Elishilia Kaaya aliieleza Kamati ya PIC kuwa Kituo kina mipango ya baadae ya kujenga Kituo kingine cha Kisasa cha Mikutano kitakachojulikana kama Mount Kilimanjaro International Convention Centre (MKICC) ili kukabiliana na ushindani wa biashara ya mikutano kutoka nchi za jirani kama Rwanda ambayo tayari ina Kituo cha kisasa cha Kigali na Kenya ambayo tayari inatarajia kujenga Kituo cha kisasa cha Mikutano huko Mombasa.

Kaaya ameeleza kuwa AICC imefanikiwa kununua ekari 23 katika mji wa Mtwara na pia inatafuta ardhi katika mikoa ya Dodoma, Mwanza na Iringa kwa ajili ya kujenga Vituo vingine vya Mikutano. Aidha alieleza Kamati kuwa mbali na kujenga Vituo vya Mikutano, AICC inatarajia kujenga miundombinu kwa ajili ya Wanajuiya ya Kidiplomasia eneo la Laki Laki nje kidogo ya mji wa Arusha ambapo Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imetenga eneo kubwa kwa ajili ya taasisi mbalimbali za kimataifa kujenga ofisi. 

Mbali na biashara ya mikutano, AICC inajishughulisha pia na upangishaji wa ofisi na nyumba na pia inatoa huduma za afya kupitia hospitali yake. Pia AICC inamiliki Kituo cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) kilichopo Dar es Salaam.
Baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma wakiwa katika mradi wa nyumba za kisasa za kupangisha za AICC ambapo mradi huu umekamilika na tayari nyumba hizo zimeisha pata wapangaji. 
Mkurugenzi wa Miliki na Miradi wa Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), Victor Kamagenge (kushoto) akitoa maelezo kwa Kamati ya Bunge ya Uwekezaji Mitaji ya Umma, juu ya ujenzi wa ukumbi wa kisasa wa maonesho. Kamati hiyo ilitembelea AICC mwishoni mwa wiki kukagua miradi miwili ya ujenzi wa ukumbi wa maonesho ambapo ujenzi wa unaendelea na mradi mwingine wa nyumba za kisasa 48 ambao tayari umekamilika.

No comments: