Sunday, February 19, 2017

WACHIMBAJI WADOGO KUMILIKISHWA ENEO LA STAMICO, BUHEMBA

Serikali imesema itatoa eneo linalomilikiwa na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) Buhemba, Mkoani Mara kwa wachimbaji Wadogo wa Madini baada ya kufanyika kwa tathmini  na taratibu za kumilikishwa eneo ili wachimbaji hao wafanye shughuli hizo kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu ikiwemo kulipa kodi.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo leo tarehe 18 Februari,2017, wakati wa ziara yake katika mgodi huo ili kuangalia shughuli za uokoaji zinazoendelea katika mgodi huo, kufuatia  ajali ya kufukiwa na kifusi kwa Wachimbaji 18  iliyotokea tarehe 13 Februari,2017, ambapo wachimbaji 13 waliokolewa siku hiyo hiyo

Prof. Muhongo  amesema kuwa, wachimbaji hao hawakuwa na leseni wala vibali halali vilivyotolewa kwao  kufanya shughuli za utafutaji dhahabu na kwamba eneo hilo linamilikiwa kisheria na STAMICO kwa leseni  PL N0. 7132/2011, na kuongeza kuwa, wachimbaji hao walivamia eneo hilo ambapo ni kosa kisheria na wanatambulika kama wavamizi.

Ameongeza kuwa, shughuli za uchimbaji katika eneo hilo zilifungwa tangu mwaka 1971 ambapo awali eneo hilo lilikuwa chini ya wakoloni kabla ya kuwa chini ya uangalizi wa Jeshi  la Kujenga Taifa (JKT), Kampuni ya Meremeta na baadaye kuwa chini ya umiliki wa STAMICO.

Aidha, amezuia shughuli zote za uchimbaji kufanyika katika eneo hilo na kusema kinachofanyika sasa ni kuutafuta mwili wa mchimbaji mmoja ambaye bado haujatolewa. ''Hadi sasa wachimbaji 15 wamekwisha okolewa, bahati mbaya wawili walitolewa wamefariki na sasa tuendelee na zoezi la kutafuta mwili uliobaki,"ameongeza Prof. Muhongo.

Pia Prof Muhongo amewshauri wachimbaji hao kujiunga katika vikundi na kusajili vikundi hivyo ili kuwezesha shughuli zao kufanyika kwa kuzingatia taratibu za uchimbaji. "Jiungeni katika vikundi , lakini ni marufuku kwa familia moja kuwa na kikundi,"amesisitiza Prof. Muhongo


Kwa upande wake Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya Viktori Mashariki Mhandisi Juma Sementa amesema kuwa, tayari Kanda hiyo imeshatoa maeneo yapatayo 35 kwa wachimbaji wadogo katika eneo la Lwabasi, mkoani humo na kueleza kuwa, leseni zote katika eneo hilo zinamilikiwa na wachimbaji  wadogo na hivyo kuwataka kufanya shughuli za uchimbaji kwa kuzingatia usalama na ikiwemo kulipa kodi.
 Mmoja wa wachimbaji waliokolewa katika ajali ya kifusi akimweleza Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kulia) jinsi ajali hiyo ya kufikiwa na kifusi wachimbaji 18 ilivyotokea. Katikakti  anayesikiliza ni Kaimu Kamishna wa Madini Mhandisi Ally Samaje.
 Mmoja wa wachimbaji wadogo akishuka chini ya shimo la kuingilia katika mgodi kwa ajili ya kusaidia shughuli za uokoaji kufuatia ajali ya kufukiwa na kifusi wachimbaji 18 katika eneo la Buhemba mkoani Mara.
 Baadhi ya Wafanyakazi wa Mgodi wa  North Mara (ACACIA)  ambao walishiriki katika zoezi la uokoaji wa wachimbaji wadogo kwa kutoa msaada wa mashine ya kuvuta maji  na tope ili kuwezesha zoezi la ufukuaji kuendelea
 Sehemu ya Wachimbaji wakifuatilia mkutano wa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo wakati wa ziara yake katika mgodi wa Buhemba  unaomilikiwa na STAMICO.
 Mmoja wa wachimbaji wadogo anayeshiriki zoezi la uokoaji katika eneo la Buhemba akimweleza Waziri wa Nishati na Madini , Profesa Sospeter Muhongo na wananchi waliokuwa eneo hilo kuhusu hali ilivyo ndani ya mgodi huo. 
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo akiongea na wachimbaji wadogo katika eneo la Buhemba ambapo ajali ya wachimbaji wadogo walifukiwa na kifusi tarehe 13 Februari,2017.

No comments: